Skip to main content
Printable page generated Wednesday, 24 April 2024, 4:28 AM
Use 'Print preview' to check the number of pages and printer settings.
Print functionality varies between browsers.
Unless otherwise stated, copyright © 2024 The Open University, all rights reserved.
Printable page generated Wednesday, 24 April 2024, 4:28 AM

11. Kutathmini Fetasi

Kipindi cha 11 Kutathmini Fetasi

Utangulizi

Katika kipindi hiki tunazingatia uchunguzi wa mwili wa mama ili kujua kuhusu mkao na afya ya mtoto wake. Utajifunza jinsi ya kuchunguza fumbatio la mama ili kubaini iwapo mtoto amelala kichwa juu, kichwa chini au kingamo kwenye uterasi yake. Kusikiza mpigo wa moyo wa fetasi pia kunaweza kukufahamisha kuhusu mkao na hali njema ya mtoto. Mwishoni mwa kipindi hiki tunakupa mwongozo kuhusu la kufanya ukishuku kuwa mkao wa mtoto unaweza kusababisha ugumu au hatari katika kuzaa, au ukishuku kuwa mwanamke huyo ana pacha.

Malengo ya Somo la Kipindi cha 11

Baada ya kipindi hiki, unapaswa uweze:

11.1 Kufafanua na kutumia kwa usahihi maneno yote muhimu yaliyochapishwa kwa herufi nzito. (Swali la kujitathmini 11.1)

11.2 Kujua jinsi ya kutambua mkao wa kawaida na usio wa kawaida kwa utomasaji na oskalitesheni. (Maswali ya kujitathmini 11.1 na 11.2)

11.3 Kujua jinsi ya kutathmini hali njema ya fetasi kwa oskalitesheni na kucheza kwa fetasi. (Maswali ya kujitathmini 11.1, 11.3 na 11.4)

11.4 Kutambua hali za fetasi zinazohitaji kupewa rufaa kwenda katika kituo cha afya kilicho karibu. (Swali la kujitathmini 11.4)

11.1 Kujua mkao wa mtoto kwenye uterasi

Mkao wa mtoto kwenye uterasi huitwa mlalo wa fetasi. Lengo la kujua mlalo wa fetasi ni kutambua iwapo kuna dalili zozote za hatari zinazoweza kuleta ugumu katika leba na kuzaa, na kumweka mama na mtoto hatarini.

Dalili bora

  • Kuna mtoto mmoja tu kwenye uterasi.
  • Kichwa cha mtoto kiko upande wa chini wakati wa kuzaa.

Dalili za hatari

  • Mtoto ametanguliza miguu au matako wakati wa kuzaa.
  • Mtoto amelala kingamo wakati wa kuzaa.
  • Mama ana pacha wawili au watatu. Tayari unajua jinsi ya kusikiza mipigo miwili ya mioyo ya fetasi (Kipindi cha 10).

Kuna mbinu mbili za kujua mkao wa mtoto - kuhisi fumbatio la mama (utomasaji), na kusikiza (oskalitesheni) ambapo sauti ya mpigo wa moyo wa fetasi ni kubwa. Unaweza kuhitaji kutumia mbinu zote mbili ili kuwa na uhakika wa mkao wa mtoto.

11.2 Kuhisi fumbatio la mama

Inaweza kuwa vigumu kujua mkao wa mtoto kabla ya miezi sita au saba ya ujauzito, na si muhimu hadi majuma 36 (miezi minane) kwa sababu ni kawaida mtoto kuzunguka hadi mwezi wa mwisho. Mara tu ujauzito unapotimiza miezi sita au saba, itakuwa rahisi kuhisi mtoto na kujua mkao wake kwenye uterasi.

Kwanza, msaidie mama kulala chali na umwekee viegemeo chini ya magoti na kichwa chake. Hakikisha ametulia. Maswali unayojaribu kujibu unapomchunguza ni:

  • Je, mtoto yuko wima (juu na chini)? Huu huitwa mlalo wima.
  • Au je, amelala kingamo kutoka upande mmoja hadi mwingine wa fumbatio lake? Huu ni mlalo wa kingamo.
  • Je, mtoto ameangalia upande wa mbele au wa nyuma wa mama?
  • Je, kichwa cha mtoto kiko chini (mlalo wakutanguliza kichwa) au matako yako chini (mlalo wakutanguliza matako)?

11.2.1 Je mtoto yuko wima ?

Watoto wengi huwa wamelala wima kufikia mwezi wa saba, kichwa kikiwa kimeelekea kwenye seviksi ya uterasi. Huu ndio mkao salama kabisa kwa uzazi wa kawaida. Ili kujua iwapo mtoto yuko wima, weka mkono bapa kwa kila upande wa fumbatio la mama. Finya kwa upole lakini kwa uthabiti, kwanza kwa mkono mmoja na kisha huo mwingine (Mchoro 11.1a). Chunguza umbo kwa makini. Je, miisho ya mtoto inaonekana kuwa kwenye pande za mama (Mchoro 11.1b)? Ikiwa ni hivyo, mtoto anaweza kuwa amelala kingamo. Watoto wengi hulala kingamo katika miezi ya kwanza lakini wengi hujigeuza kichwa chini kufikia miezi minane au zaidi. Watoto hawawezi kuzaliwa kupitia ukeni wakiwa katika mlalo wa kingamo. Mtoto aliyelala kingamo, na hawezi kugeuzwa leba inapoanza lazima azaliwe kwa upasuaji wa kuzaa hospitalini.

Mtoto akilala kingamo baada ya miezi minane ya ujauzito, mpe mwanamke huyo rufaa aende katika kituo cha afya.

Mchoro11.1 (a) Hisi fumbatio la mama kwa mikono yako kwa kila upande, ukisukuma pole pole kwa kila mkono kwa zamu. Unapaswa uweze kuhisi mtoto akiwa amelala wima - yaani kichwa chini. (b) Iwapo mtoto amelala kingamo, unaweza kuhisi kichwa na matako yake kwenye pande za mama.

Inaweza kuwa vigumu kuhisi mkao wa mtoto kwenye uterasi iwapo mama ana misuli yenye nguvu sana au iwapo ana mafuta mengi kwenye fumbatio lake. Iwapo itakuwa vigumu kuhisi nafasi ya mtoto mwambie mama avute pumzi nzito kisha aachilie polepole na alegeze mwili wake huku ukitomasa fumbatio lake.

11.2.2 Je, mtoto ameangalia upande wa mbele au wa nyuma wa mama?

Kisha hisi fumbatio la mama kupata umbo kubwa gumu (mgongo wa mtoto). Iwapo utalihisi (Mchoro 11.2a), mtoto ameangalia upande wa mgongo wa mama. Iwapo huwezi kuhisi mgongo wa mtoto, tafuta vibonge vingi vidogo (Mchoro 11.2b). Iwapo unahisi vibonge vingi vidogo badala ya umbo kubwa gumu, huenda unahisi mikono na miguu ya mtoto, inayokuonyesha kuwa mtoto ameangalia upande wa mbele wa mama.

Mchoro 11.2 (a) Iwapo unahisi umbo kubwa gumu, mtoto ameangalia upande wa mgongo wa mama. (b) Iwapo unahisi vibonge vingi vidogo, mtoto ameangalia upande wa mbele wa mama.

11.2.3 Je, mtoto yuko katika hali ya kichwa chini au matako chini?

Mchoro 11.3 (a) Mlalo wa kutanguliza kichwa. (b) Mlalo wa kutanguliza matako.

Kufikia mwezi wa mwisho kabla ya kuzaliwa, watoto wengi huwa wamelala kichwa kikielekea kwenye seviksi ya uterasi (Mchoro 11.3a). Hali ya kichwa chini huitwa mlalo wa kutanguliza kichwa, na iwapo sehemu ya fuvu la kichwa iitwayo veteksi itatangulia kwenye njia ya uzazi, huu ndio mlalo bora zaidi kwa uzazi wa mtoto. Madaktari na wakunga huiita sehemu ya mtoto inayotangulia kwenye seviksi ya uterasikitangulizi. Katika Mchoro 11.3a, kitangulizi ni kichwa cha mtoto na katika Mchoro 11.3b, kitangulizi ni matako ya mtoto. Utajifunza kuhusu milalo mingine (uso, paji la uso, bega) katika Moduli kuhusu Utunzaji katika Leba na kuzaa.

  • Je, veteksi ni sehemu ipi ya fuvu la kichwa? (Kumbuka Kipindi cha 6. Unaweza kutaka kutazama tena Mchoro 6.5 unaoonyesha mifupa ya fuvu la kichwa cha fetasi).

  • Veteksi ndiyo sehemu ya fuvu la kichwa cha fetasi kati ya utosi wa mbele (nafasi kati ya mifupa kwenye sehemu ya mbele ya kichwa cha mtoto), na utosi wa nyuma (nafasi kati ya mifupa kwenye sehemu ya nyuma ya kichwa cha mtoto).

    Mwisho wa jibu

11.2.4 Kuhisi kichwa cha mtoto

Mchoro 11.4 Kutafuta mfupa wa kinena wa mama kwa vidole vyako.

Kufikia mwezi wa saba au wa nane, kichwa cha mtoto kimeteremka chini kwenye pelvisi ya mama. Hii ndiyo jinsi ya kuhisi kichwa cha mtoto:

  1. Tafuta mfupa wa kinena wa mama kwa vidole vyako. Unaweza kuuhisi chini ya ngozi iliyo chini ya vuzi za mama (Mchoro 11.4).
  2. Anapopumua nje, finya ndani juu ya mfupa wa kinena (tazama Mchoro 11.5). Finya kwa upole na uachilie iwapo unamwumiza. Ukihisi umbo gumu la mviringo unaloweza kusongesha kidogo kutoka upande mmoja hadi mwingine, huenda ni mgongo au upande wa kichwa cha mtoto.

Usipohisi chochote kwenye upande wa chini wa fumbatio la mama, huenda mtoto amelala kingamo.

Mchoro 11.5 Finya kwa uthabiti kwa vidole vyako juu ya mfupa wa kinena ujue ikiwa unaweza kuhisi kichwa cha mtoto.
  1. Ikiwa umbo hilo si la mviringo hasa, huenda ni uso au matako ya mtoto. Au wakati mwingine matako ya mtoto yako juu lakini kichwa si wima kwenda chini (Mchoro 11.6 na b) Huenda kichwa kimejikunja kuelekea upande, au kidevu kiko juu (Mchoro 11.6c). Hizi zinaweza kuwa ishara kuwa mtoto hatatoshea kupita kwenye pelvisi ya mama akizaliwa.
Mchoro 11.6 Ikiwa mtoto amelala wima na kichwa kiko chini lakini huwezi kuhisi kichwa cha mtoto, huenda kimejikunja kuelekea upande (a) kikiwa kimeangalia upande wa nyuma wa mama, (b) kimeangalia upande wa mbele wa mama, au (c) kidevu kikiwa juu.
  1. Iwapo sehemu ya chini ya mtoto haijaingia sana kwenye pelvisi ya mama, jaribu kusongesha sehemu hiyo kutoka upande mmoja hadi mwingine kwa kuitikisa polepole kwa mikono yako kila upande wa sehemu ya chini ya fumbatio lake. (Mchoro 11.7). Iwapo kusongesha sehemu ya chini ya mtoto kunaufanya mgongo wote kusonga, huenda mtoto ametanguliza matako. Ikiwa mgongo hausongi, huenda mtoto ametanguliza kichwa.
Mchoro 11.7 Ikiwa mgongo wa mtoto hausongi unapotomasa sehemu ya chini ya fumbatio, huenda kichwa cha mtoto kiko upande wa chini.
  1. Kisha hisi sehemu ya juu ya uterasi ya mama (fandasi), chini ya mbavu zake. Je, inahisi kuwa ngumu na ya mviringo, kama kichwa? Au ni umbo tofauti - kama matako, mgongo, au miguu? Ikiwa sehemu ya juu ya uterasi inahisi kama kichwa kuliko ulivyohisi kwenye sehemu ya chini ya fumbatio la mama, huenda mtoto ametanguliza matako.
  2. Weka mkono mmoja kwa mgongo wa mtoto. Wakati huo huo, kwa mkono wako mwingine, sukuma upande mwisho wa sehemu ya juu ya mtoto polepole (Mchoro 11.8). Ikiwa mgongo wote wa mtoto unasonga unaposongesha mwisho wa sehemu ya juu, huenda mtoto ametanguliza kichwa (Mchoro 11.8a). Ikiwa mgongo utabakia pale ulipo unaposongesha sehemu ya juu ya mtoto (Mchoro 11.8b), huenda unasongesha kichwa. Hii ni kwa sababu shingo linaweza kujikunja huku mgongo ukibakia mahali pake. Iwapo unasongesha kichwa kwenye sehemu ya juu ya uterasi, huenda mtoto ametanguliza matako.
Mchoro 11.8 (a) Ikiwa mtoto ametanguliza kichwa, unapaswa uweze kusongesha mgongo wake wote kwa kusukuma polepole sehemu ya juu ya mtoto upande. (b) Iwapo unaweza kusukuma sehemu ya juu ya mtoto bila kusongesha mgongo wake, huenda ametanguliza matako.
  1. Unapochunguza mkao wa mtoto, unaweza kufikiri kuwa umehisi vichwa viwili au matako mawili. Huenda mama huyo ana pacha.
  • Kumbuka Kipindi cha 10. Je, unapaswa kufanya nini ukishuku kuwa mwanamke ana pacha?

  • Mpe mama huyo rufaa aende katika kituo cha afya mara moja.

    Mwisho wa jibu

11.2.5 Kumwuliza mama kuhusu kucheza kwa mtoto

Madaktari na wakunga huchukulia kucheza kwa fetasi kama ishara ya hali njema ya fetasi na pia inaweza kuashiria mlalo wa fetasi.

Huku ukihisi fumbatio la mama, jaribu kuwazia milalo tofauti ya mtoto kwenye uterasi. Wazia sehemu ambapo huenda mikono na miguu ya mtoto ipo. Wazia jinsi kila mlalo unavyoweza kumuathiri mama mtoto anapocheza. Kisha mwulize mama anakohisi mtoto akicheza kwa nguvu sana na anapohisi akicheza polepole. Je, hii ndiyo sehemu unayodhani miguu na mikono inaweza kuwa (tazama Mchoro 11.9)?

Mchoro 11.9 Sehemu ambapo mama anahisi mtoto akicheza kwa nguvu zaidi inaweza kukuonyesha ilipo miguu ya mtoto.

Mpe mwanamke rufaa aende katika kituo cha afya ikiwa hahisi mtoto akicheza ndani yake.

Mtoto akiwa na afya na anapata virutubishi vya kutosha kutoka kwa mama, yeye hucheza katika uterasi kwa njia ambayo mwanamke atamhisi. Kucheza kwa mtoto mara nyingi huhisika vizuri baada ya mama kula na baada ya kupumzika vizuri sana na amelala kwa upande.

Mwanamke akikuambia kuwa mtoto hasongi kama hapo awali, au hasongi kabisa, anaweza kuwa mgonjwa au amefariki.

11.3 Kusikiza mpigo wa moyo wa mtoto

Mpigo wa moyo wa mtoto hukufahamisha kuhusu mlalo wa mtoto ndani ya mama na kuhusu afya ya mtoto. Sikiza mpigo wa moyo katika kila safari yake ya utunzaji katika ujauzito kuanzia miezi mitano. Mara nyingi madaktari na wakunga hurejelea mpigo wa moyo.

Kufikia miezi miwili ya mwisho ya ujauzito, unaweza kusikia mpigo wa moyo wa fetasi mara nyingi ukiwa katika chumba kisicho na kelele kwa kuweka sikio lako kwenye fumbatio la mama (Mchoro 11.10a). Ni rahisi kusikia mpigo wa moyo kwa stethoskopu (Mchoro 11.10b) au fetoskopu (Mchoro 11.10c na d). Iwapo huna fetoskopu, unaweza kujitengenezea moja kutoka kwa mbao, mchanga au mwanzi.

Mchoro 11.10 Kusikiza mpigo wa moyo wa fetasi kwa (a) sikio lako kwenye fumbatio la mama, au (b) kwa stethoskopu, au (c) na (d) kwa fetoskopu.

Mpigo wa moyo wa fetasi ni tulivu na wa haraka. Unaweza kusikika kama mpigo mwepesi wa saa chini ya mto, ingawa kwa kasi. Mpigo wa moyo wa fetasi ni takriban mara mbili zaidi ukilinganishwa na wa moyo wa mtu mzima - kwa kawaida mipigo 120 hadi 160 kwa dakika. Hamna haja ya kuhesabu mipigo ya moyo hadi mwanamke atakapoanza leba. Kusikia mpigo dhahiri wa moyo wa fetasi wakati wa safari ya utunzaji katika ujauzito hudhibitisha kuwa mtoto yuko hai.

Ukisikia sauti ya mtindo fulani (shee-oo, shee-oo, shee-oo), huenda unasikia mpwito wa ateri wa mtoto kwenye kiungamwana. Sauti kwenye kiungamwana hukuonyesha jinsi moyo wa mtoto unavyopiga haraka, bali hazikusaidii kujua mkao wa mtoto kwenye uterasi.

Mpigo wa moyo ukiwa polepole, huenda unasikia mpwito wa ateri wa mama badala ya ule wa mtoto. Jaribu kusikiza kwenye sehemu tofauti kwa fumbatio lake.

11.3.1 Kujua mkao wa mtoto kwenye uterasi kwa kusikiza mpigo wa moyo

Mchoro 11.11 Sauti ya mpigo wa moyo wa mtoto ni kubwa kwenye sehemu ya juu ya kifua au ya mgongo kulingana na upande ambapo mtoto ameangalia.

Wazia upande ambao huenda mtoto amelalia. Kisha uanze kusikiza mpigo wa moyo karibu na sehemu unapofikiria moyo wa mtoto unapaswa kuwa. Unaweza kuhitaji kusikiza katika sehemu nyingi kwenye fumbatio la mama kabla ya kupata sehemu ambapo sauti ya mpigo wa moyo ni mkubwa na dhahiri (Mchoro 11.11).

Je, sauti ya mpigo wa moyo ni kubwa zaidi juu au chini ya kitovu cha mama? Ukisikia sauti kubwa zaidi ya mpigo wa moyo chini ya kitovu cha mama, huenda mtoto yuko katika hali ya kichwa chini (Mchoro 11.12a). Ukisikia sauti kubwa zaidi ya mpigo wa moyo juu ya kitovu cha mama, huenda mtoto yuko katika mlalo wa kutanguliza matako (Mchoro 11.12b).

Mchoro 11.12 (a) Iwapo sauti ya mpigo wa moyo ni kubwa zaidi chini ya kitovu cha mama, huenda mtoto yuko katika mlalo wa kutanguliza veteksi. (b) Iwapo ni kubwa zaidi juu ya kitovu cha mama, huenda mtoto yuko katika mlalo wa kutanguliza matako.

Wakati mwingine, mtoto akiwa ameangalia upande wa mbele wa mama, ni vigumu kupata mpigo wa moyo kwa sababu mikono na miguu ya mtoto huzuia. Sikiza karibu na pande za mama, au moja kwa moja katikati mwa fumbatio lake ili kuusikia mpigo wa moyo wa fetasi.

11.4 Cha kufanya ukipata dalili za hatari

11.4.1 Mtoto ametanguliza matako

Watoto waliotanguliza matako mara nyingi huzaliwa bila matatizo yoyote, hasa ikiwa mama amewahi kuzaa watoto wengine na alizaa kwa urahisi. Lakini watoto waliotanguliza matako wana uwezekano mkubwa wa kukwama, au kuwa na matatizo mengine hatari.

Iwapo mtoto ametanguliza matako kufikia juma la 36 (miezi 8), mpe mwanamke huyo rufaa aende katika kituo cha afya. Usijaribu kumgeuza mtoto aliyetanguliza matako (tazama Kisanduku 11.1).

Kisanduku 11.1 Usijaribu kumgeuza mtoto aliyetanguliza matako!

Ni mkunga, afisa wa afya au daktari aliyefunzwa kugeuza mtoto aliyetanguliza matako anayepaswa kujaribu kufanya hivyo na inapaswa kufanyika hospitalini. Kujaribu kugeuza mtoto kwa kufinya uterasi ni hatari sana. Hata mkunga, afisa wa afya au daktari asijaribu kumgeuza mtoto ikiwa kiowevu cha amnioni cha mama hakijatoka, au ikiwa ametokwa na damu ukeni, amekuwa na shinikizo la juu la damu, upasuaji kwenye uterasi yake, au upasuaji wa kuzaa.

Iwapo mtoto hayuko katika hali ya kichwa chini leba inapoanza, ni salama zaidi kwa mama kuzalia hospitalini. Mkunga, afisa wa afya au daktari anaweza kutumia fosepu (vifaa vya kuvuta) mtoto akikwama. Au wanaweza kufanya upasuaji wa kuzaa.

11.4.2 Mtoto amelala kingamo

Watoto waliolala kingamo hawawezi kutoshea kwenye pelvisi ya mama ili kuzaliwa (Mchoro 11.13). Ukijaribu kuzalisha mtoto bila upasuaji, uterasi ya mama itapasuka wakati wa leba, na yeye pamoja na mtoto watafariki bila huduma ya matibabu. Mtoto akigeuka na kutanguliza kichwa wakati wowote - hata siku ambapo leba ya mama itaanza - ni SAWA kwake kuzalia nyumbani au kwenye kituo cha afya.

Mtoto aliyelala kingamo lazima azaliwe kwa upasuaji wa kuzaa hospitalini. Usijaribu kumgeuza mtoto aliyelala kingamo kwa mkono. Hii ni hatari kama kujaribu kumgeuza mtoto aliyetanguliza matako, na inapaswa kufanywa tu na daktari hospitalini.

Mchoro 11.13 Iwapo mtoto amelala kingamo kufikia mwezi wa nane, unapaswa kupanga uzazi wa hospitalini kwa upasuaji wa kuza.

11.4.3 Pacha

Kumbuka uliyojifunza katika Kipindi cha 10 kuhusu ujauzito wa pacha.

  • Je, dalili tatu za ujauzito wa pacha ni zipi?

  • Uterasi hukua haraka au kubwa kuliko kawaida. Unaweza kuhisi vichwa viwili au matako mawili unapohisi tumbo la mama. Unaweza kusikia mipigo miwili ya moyo (hii si rahisi, lakini inawezekana katika miezi michache ya mwisho).

    Mwisho wa jibu

  • Je, njia mbili za kujaribu kusikia mipigo ya mioyo ya pacha ni zipi?

  • Tafuta mpigo wa moyo wa mtoto mmoja. Mwambie msaidizi kusikiza sehemu zingine ambapo mpigo wa moyo ni rahisi kusikia, na nyote mgonge mipigo ya mioyo. Tumia saa kukusaidia kuhesabu mipigo hiyo miwili ya moyo.

    Mwisho wa jibu

11.5 Baada ya uchunguzi katika ujauzito

Baada ya kumaliza kuchunguza fetasi na mama, na kufuata maagizo ya ishara zozote za hatari, chunguza iwapo mwanamke huyo ana maswali mengine, au anahitaji kuzungumzia kingine chochote. Iwapo ana ishara zozote za hatari, mweleze kwa makini kuhusu ishara hiyo ya hatari na atakachofanya kujitunza. Iwapo alikuwa amerudi kwa uchunguzi katika ujauzito, tathmini ulichomfanyia katika uchunguzi wa awali. Amua kingine chochote ambacho ungehitaji kumfanyia. Iwapo anahitaji rufaa ya kwenda katika kituo cha afya cha ngazi ya juu, hakikisha anajua kwa kwenda na wakati mwafaka wa kwenda.

11.6 Hitimisho

Katika kipindi hiki, umejifunza jinsi ya kuchunguza fumbatio la mwanamke mjamzito ili uweze kutambua mkao wa mtoto kwenye uterasi, kitangulizi (kichwa au matako au ikiwa amelala kingamo), na jinsi ya kuchunguza hali njema ya fetasi kwa kusikiza mpigo wa moyo wa fetasi na kumwuliza mama kuhusu kucheza kwa fetasi.

Muhtasari wa Kipindi cha 11

Katika Kipindi cha 11, umejifunza:

  1. Ni jambo la kutuliza kupata mtoto mmoja kwenye uterasi na kichwa chake kuwa upande wa chini katika mwezi wa mwisho wa ujauzito. Kufikia miezi saba ya ujauzito watoto wengi huwa wamelala wima kichwa kikielekea kwenye seviksi ya uterasi. Kufikia mwezi wa saba au wa nane, kichwa cha mtoto kwa kawaida huwa kimeteremka chini kwenye pelvisi ya mama. Huu ndio mkao salama zaidi kwa uzazi wa kawaida.
  2. Katika hali nyingine yoyote, yaani matako kuwa upande wa chini (kutanguliza matako), au amelala kingamo, mpe mama rufaa aende katika kituo cha afya kilicho karibu. Usijaribu kumgeuza mtoto aliyetanguliza matako au aliyelala kingamo.
  3. Sehemu katika fumbatio la mama anapohisi mtoto akicheza inaweza kukusaidia kutambua mkao wa mtoto huyo kwenye uterasi. Kucheza kwa fetasi pia ni ishara ya afya njema ya fetasi. Mtoto akiacha kucheza anaweza kuwa ni mgonjwa au amefariki, na mama anahitaji rufaa ya haraka.
  4. Mpigo wa moyo wa mtoto hujulisha kuhusu mkao wa mtoto kwenye uterasi ya mama na iwapo yuko hai. Kusikia mipigo miwili ya moyo ni ishara ya pacha. Sikiza mpigo wa moyo katika kila safari yake ya utunzaji katika ujauzito kuanzia miezi mitano.
  5. Kufikia miezi miwili ya mwisho ya ujauzito, unaweza kusikia mpigo wa moyo wa fetasi mara kwa mara ukiwa katika chumba kisicho na kelele kwa kuweka sikio lako kwenye fumbatio la mama. Ni rahisi kusikia mpigo wa moyo kwa stethoskopu au fetoskopu.
  6. Kiwango cha kawaida cha mpigo wa moyo wa fetasi ni takriban mipigo 120 hadi 160 kwa dakika.

Maswali ya Kujitathmini ya Kipindi cha 11

Kwa kuwa umekamilisha kipindi hiki, unaweza kutathmini jinsi ulivyotimiza malengo ya masomo haya kwa kujibu maswali haya. Andika majibu katika shajara yako ya masomo na ujadiliane na mkufunzi wako katika Mkutano Saidizi wa Masomo yatakayofuata. Unaweza kulinganisha majibu yako na muhtasari juu ya Maswali ya Kujitathmini mwishoni mwa Moduli hii.

Swali la kujitathmini 11.1 (linatathmini Malengo ya Somo 11.1, 11.2 na 11.3)

Je, ni kauli ipi kati ya hizi isiyo sahihi? Eleza kisicho sahihi katika kila kauli.

  • A.Kusikiza mpigo wa moyo wa fetasi kwa stethoskopu huitwa oskalitesheni.
  • B.Kichwa cha fetasi kikiwa upande wa chini na matako ya fetasi yawe upande wa juu kwenye fandasi, huitwa mlalo wima.
  • C.Katika mlalo wa kutanguliza veteksi, kitanguizi ni matako ya mtoto.
  • D.Kiwango cha mpigo wa moyo wa fetasi huwa takriban mipigo 120 hadi 160 kwa dakika.
  • E.Iwapo sauti ya mpigo wa moyo wa fetasi ni kubwa zaidi chini ya kitovu cha mama, huenda mlalo wa fetasi hiyo ni wa kutanguliza matako.
Answer

A Sahihi. Kusikiza mpigo wa moyo wa fetasi kwa stethoskopu huitwa oskalitesheni.

B Sahihi. Kichwa cha fetasi kikiwa upande wa chini na matako ya fetasi hiyo yawe upande wa juu kwenye fandasi, huitwa mlalo wima.

C Si sahihi.Katika mlalo wa kutanguliza veteksi kitangulizi ni kichwa cha mtoto.

D Sahihi. Kiwango cha mpigo wa moyo wa fetasi huwa takriban mipigo 120 hadi 160 kwa dakika.

E Si sahihi. Katika mlalo wa kutanguliza matako, sauti ya mpigo wa moyo wa fetasi ni mkubwa zaidi juu ya kitovu cha mama.

Mwisho wa jibu

Soma kwa makini uchunguzi maalum ufuatao kisha ujibu maswali ya kujitathmini 11.2 hadi 11.4.

Uchunguzi maalum 11.1 Bekelech

Bekelech alikuja kwa uchunguzi katika ujauzito akiwa na ujauzito wa miezi minane. Ulipotomasa fumbatio lake, ulipata umbo gumu la mviringo kwenye fandasi ya uterasi na umbo laini kubwa karibu na kinena simfisisi. Bekelech alikuambia kuwa kucheza kwa mtoto kulikuwa kumepungua katika juma lililopita na uliposikiza kwenye fumbatio lake kwa fetoskopu hukusikia mpigo wa moyo wa fetasi.

Swali la Kujitathmini 11.2 (linatathmini Lengo la Somo 11.2)

  • a.Je, mtoto amelala wima au kingamo katika kisa cha Belekech? Eleza jinsi ulivyofikia uamuzi wako.
  • b.Je, ni nini kitangulizi katika utafiti huu?
  • c.Je, unaitaje utangulizi kama huu wa fetasi ?
Answer
  • a.Umbo gumu la mviringo kwenye fandasi ya uterasi unaweza kuwa mgongo wa mtoto na umbo kubwa laini karibu na kinena simfisisi ni mikono na miguu yake. Huu ni mlalo wima.
  • b.Matako ndiyo kitangulizi.
  • c.Huu huitwa mlalo wa kutanguliza matako.

Mwisho wa jibu

Swali la Kujitathmini 11.3 (linatathmini Lengo la Somo 11.3)

Je, ni wapi utakaposikiza mpigo wa moyo wa fetasi kuthibitisha utambuzi wako wa jinsi mtoto wa Bekelech alivyojilaza, na kwa nini?

Answer

Utasikiza mpigo wa moyo wa fetasi juu ya kitovu cha Bekelech kwa sababu iwapo mtoto ametanguliza matako, sauti ya mpigo wa moyo wake itakuwa kubwa zaidi hapo. (Tazama tena Mchoro 11.12 ikiwa huna uhakika.)

Mwisho wa jibu

Swali la kujitathmini 11.4 (linatathmini Malengo ya Somo 11.3na 11.4)

Je, unadhani mtoto wa Bekelech yuko katika hali gani, na ni hatua ipi unayopaswa kuchukua?

Answer

Huenda mtoto huyo ni mgojwa au hata amefariki, kwa sababu Bekelech anasema hachezi na huwezi kusikia mpigo wa moyo wa fetasi. Unapaswa kumpa rufaa aende katika kituo cha afya mara moja.

Mwisho wa jibu