Skip to main content
Printable page generated Saturday, 25 January 2025, 10:43 PM
Use 'Print preview' to check the number of pages and printer settings.
Print functionality varies between browsers.
Unless otherwise stated, copyright © 2025 The Open University, all rights reserved.
Printable page generated Saturday, 25 January 2025, 10:43 PM

13. Kutoa Huduma ya Utunzaji Maalum katika Ujauzito

Kipindi cha 13 Kutoa Huduma ya Utunzaji Maalum katika Ujauzito

Utangulizi

Katika sehemu ya 1 ya Moduli Utunzaji katika Ujauzito, umejifunza kimsingi kuhusu muundo wa kimaumbile wa mfumo wa uzazi wa mwanadamu na jinsi unavyofanya kazi, awamu za kawaida za ujauzito na mabadiliko ya kuwezesha kubeba mimba, uchunguzi wa kijumla kuhusu jinsi mimba inavyoendelea na jinsi ya kutambua matatizo madogo. Katika sehemu ya 2 ya Moduli yaUtunzaji katika Ujauzito, utajifunza kuhusu kanuni za kimsingi za utunzaji maalum katika ujauzito.

Kipindi hiki kitaanza kwa kueleza dhana na kanuni za utunzaji maalum katika ujauzito na tofauti za kimsingi baina ya huduma hii na mtazamo wa kitamaduni wa utunzaji katika ujauzito. Kipindi hiki kitaangazia vipindi vingine katika sehemu ya 2 ambavyo vyote huwa katika Utunzaji Maalum katika Ujauzito. Pia utajifunza malengo ya kila mojawapo ya ziara nne za utunzaji maalum katika ujauzito. Kipindi hiki kitahitimisha kwa hatua ambazo wewe binafsi na mama mjamzito mnapaswa kutekeleza katika kuzaa; mashauri kuhusu jambo la kufanya iwapo matatizo yataibuka na maelekezo ya jinsi ya kuandika arifa ya rufaa ikiwa mama anapaswa kuhamishwa hadi katika kituo cha afya.

Malengo ya Somo la Kipindi cha 13

Baada ya kuhitimisha kipindi hiki, unatarajiwa:

13.1 Kufasili na kutumia kwa usahihi maneno yote muhimu yaliyoandikwa kwa herufi nzito. (Swali la Kujitathmini 13.1)

13.2 Kujadili kanuni za utunzaji maalumkatika ujauzito na kutaja jinsi unavyotofautiana na mtazamo wa kitamaduni. (Swali la Kujitathmini 13.1)

13.3 Kueleza ratiba, malengo na taratibu zinazofuatwa katika kila mojawapo ya ziara nne za utunzaji maalum katika ujauzito, za wanawake katika kipengele cha kimsingi. (Maswali ya Kujitathmini 13.2 na 13.3)

13.4 Kuwashauri wanawake wajawazito kuhusu maandalizi ya kuzaa pamoja na vifaa watakavyohitaji. (Swali la Kujitathmini 13.4)

13.5 Kutoa muhtasari wa vipengele muhimu vya kujitayarishia matatizo na kupangia matukio ya dharura, ikijumuisha kuwashauri watoaji damu na kuandika arifa ya rufaa. (Swali la Kujitathmini 13.3)

13.1 Dhana na kanuni za utunzaji maalum katika ujauzito

Kihistoria, kielelezo cha kitamaduni cha utunzaji katika ujauzito kilianzishwa miaka ya kwanza ya 1900. Kielelezo hiki huchukulia kuwa ziara za kila mara na kuwaainisha wanawake wajawazito katika viwango vya hatari ya chini na hatari ya juu kwa kutabiri matatizo kabla ya wakati, ndiyo njia mwafaka ya kumtunza mama na fetasi. Utunzaji maalum katika ujauzito ulichukua nafasi ya mtazamo wa kitamaduni wa utunzaji katika ujauzito - huu ni mtazamo wa kimalengo uliopendekezwa na watafiti mnamo mwaka wa 2001 na kuanza kutumiwa na Shirika la Afya Duniani mnamo mwaka wa 2002.

Kusudi la utunzaji maalum katika ujauzito ni kukuza afya ya kina mama na watoto wao kupitia ukaguzi uliolengwa kwa wanawake wajawazito ili kusaidia:

  • Utambuzi na utabibu wa ugonjwa uliothibitishwa
  • Ugunduzi wa mapema kuhusu matatizo na shida zingine zinazoweza kuathiri matokeo ya mimba
  • Proflaksisi na matibabu ya anemia, malaria na magonjwa ya zinaa ikijumuisha VVU, maambukizi ya mfumo wa mkojo na pepopunda. Profilaksisi ni hatua za kuingilia kati zinazolenga kuzuia ugonjwa au matatizo.

Pia, utunzaji maalum katika ujauzito hukusudia kumpa kila mwanamke utunzaji wa kibinafsi ili kudumisha hali ya kawaida ya kuendelea kwa ujauzito kupitia uelekezi na ushauri wa wakati unaofaa kuhusu:

  • Maandalizi ya kuzaa (yalioelezwa baadaye katika kipindi hiki),
  • Lishe, chanjo, usafi wa mwili na upangaji uzazi (Kipindi cha 14)
  • Ushauri kuhusu dalili za hatari zinazoashiria kuwa mwanamke mjamzito anapaswa kupata usaidizi mara moja kutoka kwa mtaalamu wa afya (Kipindi cha 15).

Katika utunzaji maalum katika ujauzito, wahudumu wa afya husisitiza makadirio ya kibinafsi na hatua zinazohitajika ili mhudumu na mama mjamzito waweze kufanya uamuzi kuhusu utunzaji katika ujauzito. Hivyo basi, badala ya kufanya ziara za kila mara za kitamaduni za utunzaji katika ujauzito kuwa desturi kwa wote, na kuwaainisha wanawake kwa kuzingatia kiashiria hatari cha kidesturi, wahudumu wa utunzaji maalum katika ujauzito huongozwa na hali ya kibinafsi ya mwanamke.

Mtazamo huu pia hufanya utunzaji katika ujauzito kuwa jukumu la familia. Mhudumu wa afya hujadili na mwanamke na mumewe kuhusu matatizo ambayo mama anaweza kukumbana nayo; pamoja wanapanga kujitayarishia kuzaa na kujadili utunzaji wa baada ya kuzaa pamoja na maswala ya uzazi wa baadaye. Wanawake wajawazito hupata utunzaji wa asili wakiwa nyumbani na katika kituo cha afya; familia pamoja na wahudumu wa afya hutambua matatizo mapema; na hatua za kuingilia kati huanzishwa kwa wakati unaofaa hivyo kuwa na matokeo bora zaidi kwa akina mama na watoto wao.

Kisanduku 13.1 kinatoa muhtasari wa kanuni za kimsingi za utunzaji maalum katika ujauzito.

Kisanduku 13.1 Kanuni za kimsingi kuhusu utunzaji maalum katika ujauzito

  • Wahudumu wa utunzaji katika ujauzito hufanya utathmini mkamilifu wa mwanamke mjamzito ili kutambua na kutibu matatizo yaliyoko ya kiukunga na kitabibu.
  • Wao huendesha proflaksisi kama ilivyoashiriwa, kama vile hatua za kuzuia malaria, anemia, upungufu wa lishe, magonjwa ya zinaa ikijumuisha kuzuia kusambazwa kwa VVU kutoka kwa mama hadi kwa mtoto (tazama Kipindi cha 16), na pepopunda.
  • Wakiwajumuisha kina mama, wahudumu hawa huamua mahali pa kufanyia ziara fuatilizi za utunzaji katika ujauzito, jinsi ziara hizo zitakavyofuatana, mahali pa kuzalishia na atakayehusika katika utunzaji wa ujauzito na wa baada ya kuzaa.
  • Mradi tu kiwango cha utunzaji kimetiliwa mkazo katika kila ziara na wachumba wanafahamu hatari zinazoweza kutokea wakati wa ujauzito, mimba nyingi huendelea bila matatizo.
  • Hata hivyo hakuna ujauzito unaoweza kuwa 'bila hatari' hadi udhibitishwe, kwa sababu matatizo yanayohusiana na ujauzito, yakiwemo yenye athari mbaya na yasiyo na athari mbaya huwa hayatabiriki pamoja na matukio ya awamu za mwisho ya ujauzito.
  • Mwanawake mjamzito na mumewe huaminika kuwa 'wagunduzi wa hatari' baada ya kupata ushauri kuhusu dalili za hatari na pia 'washiriki' wa huduma ya afya kwa kukubali na kutekeleza mapendekezo yako.

13.1.1 Manufaa ya utunzaji maalum katika ujauzito

Utunzaji maalum katika ujauzito umepata umaarufu kwa sababu ya manufaa yake katika kupunguza vifo vya kina mama na uwezo wa kufa na maradhi(ugonjwa, matatizo au ulemavu) ya kipindi kinachokaribiana na kuzaliwa. Uwezo wa kufa katika kipindi kinachokaribiana na kuzaliwa ni idadi ya jumla ya uzazimfu (watoto wanaozaliwa wafu baada ya wiki 28 za ujauzito) ikijumlishwa na idadi ya jumla ya watoto wachanga (watoto wazawa) ambao hufariki katika siku 7 za kwanza za maisha. Kima cha vifo katika kipindi kinachokaribiana na kuzaliwa ni idadi ya watoto wanaozaliwa wafu na vifo vya watoto wachanga vinavyotokea kwa kila watoto 1000 waliozaliwa hai, na ni kipimo kilichotambulika ulimwenguni kote cha kiwango cha utunzaji katika ujauzito.

  • Ufasili wa uwiano wa kiwango cha vifo vya kina mama ni upi? (Ulijifunza haya katika Kipindi cha 1 cha Moduli hii.)

  • Uwiano wa kiwango cha vifo vya kina mama ni idadi ya jumla ya wanawake wanaofariki kutokana na matatizo ya ujauzito au kuzaa, kwa kila watoto 100,000 waliozaliwa hai.

    Mwisho wa jibu

Utunzaji katika maalum ujauzito ni mtazamo mwafaka kwa nchi zisizo na raslimali za kutosha ambapo wataalamu wa afya ni wachache na miundo msingi ya afya ni duni. Hususani, wanawake wengi wajawazito hawawezi kukimu gharama ya ziara za kila mara kama inavyohitajika katika mtazamo wa kitamaduni wa utunzaji katika ujauzito. Katika mtazamo wa kimipango na kifedha, mtazamo wa kitamaduni wa utunzaji katika ujauzito hauwezi kutekelezwa katika wanawake wengi wajawazito na ni mzigo kwa mfumo wa afya. Kwa hivyo, mataifa mengi yanayoendelea yanachukua mtazamo wa utunzaji maalum katika ujauzito.

13.1.2 Kasoro za mtazamo wa kitamaduni wa utunzaji katika ujauzito

Utafiti (kwa mfano, tazama Kisanduku13.2) umeonyesha kuwa ziara za kila mara za kipindi cha ujauzito kama ilivyo katika mtazamo wa kitamaduni haziboreshi matokeo ya ujauzito. Hususan, wanawake wajawazito unaoitajika kuwa na 'hatari ya chini' au 'wasio na hatari' katika mtazamo wa kitamaduni wa utunzaji katika ujauzito huenda wasipate ushauri kuhusu dalili za hatari. Hivyo, mara nyingi wanawake hawa hawatambui dalili za hatari hivyo hawawaarifu wataalamu wa afya haraka iwezekanavyo.

Kisanduku 13.2 Kukosa kutambua mimba 'zilizo hatarini'

Kwa kuchukua kutokea kwa leba iliyokwama kama mojawapo ya kiashiria, utafiti wa mwaka wa 1984 nchini Zaire katika wanawake 3,614 wajawazito ulionyesha kuwa asilimia 71 ya wanawake walio na leba iliyokwama walikuwa wameainishwa kama 'wasio na hatari' hapo awali, wakati asilimia 90 ya wanawake waliogunduliwa kuwa 'katika hatari' hawakupata leba iliyokwama. Hii ni asili moja ya ushahidi kuonyesha kuwa matatizo mengi ya ujauzito hayawezi kutabirika na hutokea katika awamu za mwisho.

Mifano mingine ya matatizo ya ujauzito yasiyoweza kutabirika ambayo hutokea katika awamu za mwisho zaidi za ujauzito hujumuisha visababishi vitatu vikuu vya vifo vingi vya kina mama:

  • Matatizo ya hipatensheni katika ujauzito (hipatensheni humaanisha shinikizo la juu la damu hasa eklampsia, ambayo kwa kawaida hutokea katika ujauzito awamu za mwisho za ujauzito, wakati wa leba au baada ya kuzaa (utajifunza haya katika Kipindi cha 19).
  • Kuvuja damu (kuvuja damu nyingi) kwa kawaida hutokea katika trimesta ya tatu (Kipindi cha 21 kinaeleza kuvuja damu katika awamu za mwisho za ujauzito) au hasa hali hatari ya kuvuja damu baada ya kuzaa, ambayo hutokea baada ya kuzaa (utajifunza haya katika Moduli ya Utunzaji wa Leba na Kuzaa).
  • Maambukizi yanayohusiana na ujauzito (Maambukizi ya uterasi baada ya kuzaa) ambayo kwa kawaida hutokea baada ya kuzaa (kama ilivyoelezwa katika Moduli ya Utunzaji wa Leba na Kuzaa).

Mtazamo wa kitamaduni wa utunzaji katika ujauzito umeshindwa kutambua kwa hakika wanawake walio ’katika hatari' ya kupata hali hizi zinazotishia maisha. Mtazamo huu hutambua baadhi ya wanawake kama walio na 'hatari ya chini' ambao baadaye hupata dalili za hatari zinazohitaji wataalamu kuingilia kati kwa dharura.

13.1.3 Ulinganishaji wa utunzaji katika ujauzito wa kitamaduni na utunzaji maalum

Jedwali 13.1 kinatoa muhtasari wa tofauti za kimsingi baina ya mtazamo wa kitamaduni wa utunzaji katika ujauzito na utunzaji maalum

Matumizi ya dawa za kulevya hujumuisha tumbaku, vileo, miraa, dawa zilizopigwa marufuku, bangi, kokeini na dawa nyinginezo

Jedwali 13.1 Tofauti za kimsingi baina ya utunzaji wa kitamaduni na utunzaji maalum katika ujauzito.
SifaUtunzaji wa kitamaduni katika ujauzito Utunzaji maalum katika ujauzito
Idadi ya ziara16 - 18 bila kuzingatia hali ya hatari4 kwa wanawake walioainishwa katika kipengele cha kimsingi (kama ilivyoelezwa baadaye katika kipindi hiki)
MtazamoWima: maswala ya ujauzito pekee ndiyo yanayoshugulikiwa na wahudumu wa afya.Huunganishwa na kuzuia kusambazwa kwa VVU kutoka kwa mama hadi mtoto, ushauri kuhusu dalili za hatari, hatari za kutumia dawa za kulevya, kupima VVU, kuzuia malaria, lishe, chanjo na kadhalika.
DhanaZiara za mara nyingi zaidi za wanawake wajawazito na kuwaainisha katika vikundi vya hatari ya juu/chini husaidia kutambua matatizo. Huchukulia kuwa ziara zinapokuwa nyingi, matokeo huwa bora zaidi.Huchukulia kuwa ujauzito wowote unaweza kuwa 'na hatari'. Ziara mahususi na za kibinafsi husaidia kutambua matatizo
Matumizi ya viashiria vya hatariHutegemea viashiria hatari vya kidesturi kama vile urefu wa mama <150cm, uzito wa <50kg, edema ya miguu, hali mbaya ya fetasi kabla ya wiki 36, na kadhalikaHaitegemei viashiria hatari vya desturi. Huchukulia kuwa hatari kwa mama na fetasi inaweza kutambulika muda unavyopita
Hutayarisha familiaKuwategemea wahudumu wa afya pekeeKugawa majukumu ya kujitayarishia matatizo na maandalizi ya uzazi
MawasilianoMawasiliano ya upande mmoja(elimu ya afya) kwa wanawake wajawazito pekeeMawasiliano ya pande mbili (ushauri) kwa wanawake wajawazito na waume zao
Gharama na wakatiMtazamo huu huwagharimu na kufanya wanawake wajawazito pamoja na wahudumu wa afya kutumia wakati mwingi kwani hauteui maswalaHuwa na gharama ya chini na huokoa wakati. Wanawake wachache huhitaji ziara za kila mara au rufaa kwani mimba nyingi huendelea bila matatizo
AthariHutoa fursa ya upuuzi wa wahudumu wa afya na familia ya wale wasio ‘hatarini’ na kufanya familia kutojua na kusita punde matatizo yanapotokeaHutahadharisha wahudumu wa afya na familia kuhusu matatizo yanayoweza kutokea wakati wowote wa ujauzito

13.2 Vipengele muhimu vya utunzaji maalum katika ujauzito

Utunzaji maalum katika ujauzito una awamu tatu zifuatazo:

  • Uchunguzi kamili (kuchukua historia, uchunguzi wa kimwili na upelelezi wa kimsingi)
  • Kuingilia kati (kuzuia/ proflasksisi na matibabu)
  • Uhamasisho (elimu ya afya/ kushauri na kusambaza utunzaji wa afya).

Kisanduku 13.3 kinatoa muhtasari wa hatua za utaratibu huu.

Kisanduku 13.3 Hatua za kimsingi katika huduma ya utunzaji maalum katika ujauzito

  1. Kusanya habari (chukua historia) kwa kuzungumza na mama, kuchunguza mwili wake na wa fetasi (uchunguzi wa mwili na vipimo), kama ulivyojifunza katika Vipindi vya 8-11 vya Moduli hii.
  2. Tafsiri habari uliyokusanya (fanya utambuzi) na utathmini vipengele vyovyote vilivyo vya hatari.
  3. Tengeneza ratiba ya utunzaji wa kibinafsi. Ratiba ya utunzaji italenga ushauri, maandalizi ya kuzaa na kiwango cha kujitayarishia matatizo ikiwa hakuna matatizo yatakayotambuliwa. Ikiwa mama anahitaji utunzaji maalum, ratiba hii itakuwa ya kumpa mama rufaa hadi kwenye kituo cha afya cha juu zaidi.
  4. Fuata ratiba ya utunzaji - katika ziara zinazofuatia, unaweza kumhudumia mwanamke wewe binafsi kwa kutoa matibabu na ushauri au pengine utahitaji kumpa rufaa.

Katika utoaji huduma ya utunzaji maalum katika ujauzito vipengele muhimu vitakavyozingatiwa ni:

  • Kuweka siri na faragha; mawasiliano mwafaka hujenga uaminifu na kukuza ujasiri, hivyo unapaswa kuzungumza na mwanamke na mumewe kwa njia inayochochea mawasiliano kuhusu maandalizi ya kuzaa, kujitayarishia matatizo, kuzuia VVU, utunzaji na matibabu.
  • Utunzaji endelevu hutolewa na mhudumu yule yule kwa wanawake wajawazito katika jamii; katika muktadha wa mtalaa huu, wewe ndiwe mtaalamu wa kutoa huduma ya utunzaji kwa wanawake wajawazito wasio na matatizo yaliyotambulika.
  • Kuhamasisha uhusika wa mwenzi wa mwanamke au msaidizi katika shughuli ya utunzaji katika ujauzito na matayarisho ya kuzalisha.
  • Kutoa huduma ya kidesturi ya utunzaji katika ujauzito kama ilivyo katika itifaki za kitaifa, kama itakavyoelezwa baadaye katika kipindi hiki).
  • Kuunganisha utunzaji katika ujauzito na wa baada ya kuzaa pamoja na kuzuia kusambazwa kwa VVU kutoka kwa mama hadi kwa mtoto na kutoa huduma za upangaji uzazi.

13.3 Vipengele vya kimsingi na maalum vya utunzaji maalum katika ujauzito

Kielelezo cha utunzaji maalum katika ujauzito huwaainisha wanawake wajawazito katika vikundi viwili: wanaostahiki kupata utunzaji wa kidesturi katika ujauzito (kikundi kinachoitwa kipengele chakimsingi), na wanaohitaji utunzaji maalum kulingana na hali yao hasa ya afya au vipengele vya hatari (kipengele maalum). Vigezo vilivyowekwa awali (kama inavyoelezwa hapa chini) hutumika kuamua kuhusu wanawake wanaostahiki kuingia katika kipengele cha kimsingi. Wanawake waliochaguliwa kuwa katika kipengele cha kimsingi huchukuliwa kama wasiohitaji ukaguzi zaidi au utunzaji maalum wakati wa ziara ya kwanza, bila kuzingatia umri wa ujauzito ambao mama alianza ratiba ya utunzaji katika ujauzito.

Wanawake huulizwa maswali na kuchunguzwa katika ziara ya kwanza ili kufahamu iwapo wana vipengele vyovyote vifuatavyo vya hatari:

Mimba ya awali:

  • Ilitokea kuwa uzazimfu au kifo cha mtoto mzawa
  • Historia ya utokaji wa ghafla wa mara tatu au zaidi mfululizo
  • Mtoto mwenye uzito wa chini (<2500 g) au wa juu (>4000 g) wakati wa kuzaliwa
  • Kulazwa hospitalini kufuatia shinikizo la juu la damu, prieklampsia au eklampsia. (Utajifunza kuhusu hali hizi katika Kipindi cha 19.)

Mimba iliyopo:

  • Utambuzi au kukisia kuwepo kwa mimba ya pacha au watoto wengi
  • Umri wa mama ukiwa chini ya miaka 16 au zaidi ya 40
  • Mama ana aina ya damu isiyo na antijeni ya Rhesus:hali hii inaweza kusababisha madhara makubwa kwa fetasi ikiwa damu ya fetasi ina antijeni ya Rhesus, kwa sababu mwili wa mama hutolesha antibodi zinazoweza kupitia kwenye plasenta na kuvamia tishu za mtoto
  • Mama anavuja damu ukeni au ana uvimbe katika pelvisi
  • Shinikizo la damu ya mama la kidiastoli (kiwango cha chini) ni mmHg 90 au zaidi
  • Kwa sasa mama ana kisukari, ugonjwa wa moyo, ugonjwa wa figo, saratani, shinikizo la juu la damu au maradhi yoyote makali ya kuambukiza kama vile tibii, malaria, VVU/UKIMWI au magonjwa mengine ya zinaa.

'NDIO' kwa MOJAWAPO ya maswali yaliyoko hapo juu humaanisha kuwa mwanamke huyo hastahiki kuwa katika kipengele cha kimsingi ya utunzaji katika ujauzito. Mwanamke huyu ataainishwa katika kipengele maalum na anahitaji kuangaliwa kwa makini zaidi na kupewa rufaa kwa utunzaji wa kitaalamu.

Utawapa rufaa wanawake walio katika kipengele maalum ili wafuatiliwe kwa makini zaidi katika kituo cha afya cha kiwango cha juu zaidi na kupewa utunzaji maalum utakaoamuliwa na wataalamu katika nyenzo hizo, hali ukiendelea kufuata hatua zilizoko katika kipengele cha kimsingi.

13.4 Kadi ya utunzaji katika ujauzito

Kielelezo 13.1 ni mwongozo wa habari unayopaswa kukusanya katika kila mojawapo ya ziara nne za utunzaji katika ujauzito. Mwanzoni mwa kila ziara, mwulize mama ikiwa amepata dalili zozote za hatari tangu kuchunguzwa. Mkumbushe kuja kukuona ikiwa ataanza kuvuja damu ukeni, kuwa na kiwaa, maumivu ya tumbo, homa au dalili yoyote ile ya hatari. Utajifunza jinsi ya kumshauri kuhusu dalili za hatari katika Kipindi cha 15.

Kielelezo 13.1 Kadi ya Utunzaji katika ujauzito.

13.5 Malengo na taratibu katika kila ziara ya utunzaji maalum katika ujauzito

Wakati mwingine, mwanamke mjamzito huja kuchunguzwa kwa mara ya kwanza ya utunzaji katika ujauzito wakati ujauzito tayari umeendelea. Hata hivyo, unapaswa kujumuisha hatua zote za ratiba ya utunzaji wa kimsingi na hatuazote za ziara ya kwanza hata kama mama yuko katika trimesta ya pili au ya tatu ya ujauzito.

13.5.1 Ziara ya kwanza ya utunzaji maalum katika ujauzito

Ziara ya kwanza ya utunzaji maalum katika ujauzito inapaswa kutendeka kabla ya wiki 16 za ujauzito. Unapaswa kutimiza malengo yafuatayo:

  • Tambua historia ya mwanamke huyu ya kitabibu na kiukunga (ukitumia mbinu ulizojifunza katika Kipindi cha 8) ili upate ushahidi ikiwa anafaa kufuata kipengele cha kimsingi au utambue iwapo anahitaji utunzaji maalum na/au rufaa katika kituo cha juu zaidi cha afya.
  • Fanya uchunguzi wa kimsingi (mpigo wa moyo, shinikizo la damu, kiwango cha pumzi, joto, kuparara, na kadhalika).
  • Unapokisia kuwa ujauzito umepitisha trimesta ya kwanza, jaribu kutambua umri wa ujauzito kwa kupima urefu wa fandasi kwa kutumia mbinu ulizojifunza katika Kipindi cha 10.
  • Toa ushauri wa lishe na nyongeza ya kidesturi ya madini ya ayoni na foleti (vipimo vyake vimeelezwa katika Kipindi cha 14) Ni muhimu pia kutoa ushauri dhidi ya fikra potofu kuhusu chakula. Kwa mfano, katika baadhi ya sehemu za Afrika, watu huwaza kuwa kula mayai na nyama wakati wa ujauzito husababisha veniksi (unyeso mzito mweupe unaofunika ngozi ya mtoto anapozaliwa), na kwamba veniksi ni chafu. Kwa hakika, mayai na nyama ni asili muhimu za protini kwa mama na fetasi inayokua, na veniksi ni muhimu kwa mtoto kwani huikinga ngozi yake.
  • Toa ushauri kuhusu VVU na huduma za kuzuia kusambazwa kwa VVU kutoka kwa mama hadi kwa mtoto (utajifunza jinsi ya kufanya hivi katika Kipindi cha 16).
  • Toa ushauri wa jinsi ya kuzuia malaria na inapohitajika uwape neti zilizotiwa dawa ya kuua wadudu. Utajifunza mengi kuhusu kuzuia na kutibu malaria katika Kipindi cha 18.
  • Pima kiwango cha sukari kwenye mkojo wake kwa kutumia kijiti cha kupimia kama ulivyojifunza katika Kipindi cha 9, au umpe rufaa hadi kwenye kituo cha afya ukikisia kuwa anaanza kuwa na kisukari.
  • Mshauri yeye na mwenziye kuweka hakiba ya fedha ikiwa utahitaji kumpa rufaa, hasa iwapo jambo la dharura litakalohitaji asafirishwe hadi kwenye kituo cha afya litatokea. Mwanamke huyu anaweza pia kuhitaji fedha zaidi za dawa na matibabu. Usaidizi wa kifedha unaweza kupatikana katika mashirika ya jamii kama vile vikundi vya kina mama.
  • Toa majibu mahususi kwa maswali au mashaka ya mwanamke mjamzito au yale ya mwenziye.
  • Inamaanisha nini ikiwa kuna tofauti ya wiki kadhaa baina ya umri wa ujauzito uliokadiriwa kwa kutumia kipimo cha urefu wa fandasi na kadirio la kipindi cha mwisho cha hedhi ya kawaida?

  • Kama ulivyojifunza katika Kipindi cha 10, hii inaweza kumaanisha kuwa mwanamke hajakumbuka vyema tarehe ya kipindi cha mwisho cha hedhi ya kawaida, lakini inaweza pia kumaanisha kuwa fetasi haikui kwa njia ya kawaida (urefu wa fandasi ukiwa chini ya kadirio la kipindi cha mwisho cha hedhi ya kawaida) au pia inawezekana kuna kiowevu cha amniotiki kingi zaidi kinachoizingira fetasi, au kuna ujauzito wa pacha au mtoto mkubwa zaidi (urefu wa fandasi ni zaidi ya kadirio la kipindi cha mwisho cha hedhi ya kawaida.)

    Mwisho wa jibu

13.5.2 Ziara ya pili ya utunzaji maalum katika ujauzito

Ratibu ziara ya pili ya utunzaji maalum katika ujauzito kati ya wiki ya 24-28 ya ujauzito. Fuata taratibu zilizoelezwa katika ziara ya kwanza. Aidha:

  • Zingatia malalamishi au mashaka yoyote ya mwanamke mjamzito na ya mwenziye.
  • Kwa wale wanaozaa kwa mara ya kwanza au yeyote aliye na historia ya shinikizo la juu la damu au prieklampsia/eklampsia, pima kiwango cha protini katika mkojo wake kwa kutumia kijiti cha kupimia. (Utajifunza jinsi ya kufanya hivi katika Kipindi cha 19 cha Moduli hii.)
  • Durusu, na iwapo itahitajika, ubadilishe ratiba yake ya utunzaji wa kibinafsi.
  • Mpe ushauri kuhusu mahali popote anapoweza kupokea usaidizi wa kijamii au kifedha unaoweza kupatikana katika jamii yake.

13.5.3 Ziara ya tatu ya utunzaji maalum katika ujauzito

Ziara ya tatu ya utunzaji maalum katika ujauzito inapaswa kutendeka karibu na kipindi cha wiki ya 30- 32 ya ujauzito. Malengo ya ziara hii ya tatu ni sawa na yale ya ziara ya pili. Aidha: unapaswa:

  • Kumakinika zaidi kuhusu ishara za mimba ya watoto wengi na umpe rufaa ukikisia kuwepo kwa zaidi ya fetasi moja.
  • Kudurusu ratiba ya kujiandalia kuzaa na ile ya kujitayarishia matatizo (iliyojadiliwa baadaye katika kipindi hiki)
  • Kupima kiwango cha protini katika mkojo wa wanawake wote wajawazito kwa kutumia kijiti cha kupimia (kwani matatizo ya shinikizo la juu la damu hayatabiriki pamoja na matukio ya awamu za mwisho za ujauzito)
  • Kuamua iwapo kuna haja ya rufaa kulingana na ugaguzi wa hivi karibuni wa hatari.
  • Kumshauri kuhusu upangaji uzazi (Kipindi cha 14).
  • Kumhimiza mama azingatie kunyonyesha mtoto bila kumpa chakula kingine chochote (Kipindi cha 14).

Kumbuka kuwa wanawake wengine huenda wakapata leba kabla ya ziara inayofuata. Washauri wanawake wote kukuita mara moja au kuja kwako punde tu wanapoanza leba. Usingoje!

Unapaswa pia kusisitiza umuhimu wa ziara ya kwanza baada ya kuzaa ili kuhakikisha umemhudumia akiwa nyumbani kwake au kituoni cha afya baada ya kuzaa. Kipindi kilicho muhimu zaidi baada ya kuzaa ni saa 4 za kwanza; matukio mengi ya kuvuja damu baada ya kuzaa hutokea wakati huu. (Utajifunza kuhusu kuvuja damu baada ya kuzaa katika Moduli ya Utunzaji katika Leba na Kuzaa.)

13.5.4 Ziara ya nne ya utunzaji maalum katika ujauzito

Ziara ya nne ya utunzaji maalum katika ujauzito inapaswa kuwa ya mwisho kwa wanawake walio katika kipengele cha kimsingi na hupaswa kufanyika kati ya wiki ya 36- 40 ya ujauzito. Unapaswa kuzingatia hatua zote zilizoelezwa katika ziara ya tatu. Aidha:

  • Uchunguzi wa tumbo unapaswa kutambua jinsi fetasi imejilaza na sehemu itakayotangulia katika uterasi, kama ulivyojifunza katika Kipindi cha 10 na 11 na katika masomo ya kiutendaji. Katika ziara hii, ni muhimu kuwatambua wanawake walio na mtoto aliyetanguliza matako au mwenye mkao wa kukingama, kisha umpe rufaa hadi kwenye kituo cha afya kilicho karibu ili apate ukaguzi wa kiukunga.
  • Ratiba ya kibinafsi ya kuzaa (Kisanduku 13.4) inapaswa kudurusiwa ili kutambua iwapo inajumuisha vipengele vyote vya kujitayarishia kuzaa, kujiandalia matatizo na kupangia matukio ya dharura, kama inavyoelezwa katika kitengo kinachofuata.
  • Mpe mama ushauri kuhusu ishara za leba ya kawaida na mambo ya dharura ya nayohusiana na ujauzito (kama ilivyoelezwa katika Kipindi cha 15), jinsi ya kukabiliana na hali hizi, ikijumuisha mahali anapopaswa kutafuta usaidizi.
  • Kutanguliza matako, na mkao wa kukingama humaanisha nini? (Ulijifunza haya katika Kipindi cha 11.)

  • Kutanguliza matako ni hali ambapo kichwa cha mtoto kinaelekea juu katika uterasi, huku matako, miguu au nyayo zikielekea chini kwenye seviksi ya mama wakati ujauzito unapokaribia mwisho. Mkao wa kukingama ni hali ambayo mtoto amejilaza kutoka upande mmoja hadi mwingine katika fumbatio.

    Mwisho wa jibu

Mtoto aliyetanguliza matako huenda azaliwe kupitia uke katika kituo cha afya. Mtaalamu wa kiukunga anaweza kumrekebisha mtoto aliyejilaza kwa kukingama hadi arejelee hali ya kawaida ya kutanguliza kichwa au veteksi, au ni sharti azaliwe kwa upasuaji.

Kisanduku 13.4 Ratiba ya kibinafsi ya kuzaa

Ratiba ya kibinafsi ya kuzaa ni mwongozo wa wahudumu wa afya inayoanzishwa kwa kujadiliana na mwanawake binafsi na mwenzi wake au wasaidizi wakuu. Mwongozo huu huonyesha jinsi wangependa kuzaa. Baadhi ya wachumba huchagua kuzalia nyumbani chini ya utunzaji wako kwa sababu wao huchukulia kuzaa kama jambo la kawaida maishani. Wengine huchagua kuzalia hospitalini au katika kituo cha afya. Ratiba ya kuzaa ya wanawake walio na VVU inapaswa kuwa kuzalisha katika kituo cha afya kama ilivyo katika Mwelekezo wa Kitaifa wa kuzuia kusambazwa kwa VVU kutoka kwa mama hadi mtoto (kama ilivyoelezwa katika Kipindi cha 16).

13.6 Kujitayarishia kuzaa, kujiandalia matatizo na kupangia hali za dharura

Kujitayarishia kuzaa ni utaratibu wa kupangia mwanamke kuzaa kwa njia ya kawaida. Kujiandalia matatizo ni kutazamia hatua zinazohitajika ikiwa jambo la dharura litatokea. Kupangia matukio ya dharura ni utaratibu wa kutambua na kukubaliana kuhusu hatua zote zinazohitaji kuchukuliwa upesi dharura ikitokea, na maelezo yake kueleweka na kila mmoja anayehusika, na mipango inayohitajika kufanywa. Kwanza tutazingatia kujitayarishia mwanamke kuzaa kwa njia ya kawaida.

13.6.1 Kujitayarishia kuzaa kwa njia ya kawaida

Muelimishe mama na familia yake kubaini ishara za kawaida za leba. Mwanamke anaweza kuzaa siku kadhaa au hata wiki nyingi kabla au baada ya tarehe iliyotarajiwa, kulingana na tarehe ya kipindi cha mwisho cha hedhi ya kawaida. Mwanamke anapofahamu maana ya leba, ataweza kufahamu kitakachotokea. Ufahamu huu kisha humsaidia kutulia zaidi na kuwa na ujasiri katika siku au wiki za mwisho za ujauzito.

Toa maagizo dhahiri ya jambo la kufanya leba inapoanza (kwa mfano ikiwa atakuwa na maumivu ya mkakamao wa misuli ya fumbatio au kuvuja kwa kiowevu cha amniotiki). Hakikisha kuwa kuna mtu atakayekuita wewe au mtaalamu mwingine ili kuzalisha haraka iwezekanavyo. Ambatanisha ushauri wako wa kiusemi kwa maagizo yaliyoandikwa kwa lugha asili ya mteja.

Maandalizi ya kuzaa pia yanafaa kuzingatia:

  • Kuheshimu chaguo la mama. Unapaswa kumpa mama habari zote zinazohitajika kuhusu uzalishaji safi na salama, lakini hatimaye unapaswa kuheshimu chaguo lake kuhusu mahali pa kuzalia na mtu angelipenda kuandamana naye.
  • Kumsaidia mama kutambua mahali pa kupata usaidizi wakati wa kuzaa na kipindi cha baada ya kuzaa kinachofuata punde.
  • Kupangia gharama yoyote ya ziada inayohusiana na kuzaa.
  • Kutayarisha vifaa vya kumtunza mama na mtoto wake mzawa.

13.6.2 Vifaa vya kuzalishia ambavyo mama anapaswa kutayarisha

Vifaa vya kuzalishia ambavyo mwanamke mjamzito na familia yake wanapaswa kushauriwa watayarishe kabla ya kuzaa ni (tazama Mchoro 13.2):

  • Nguo safi kabisa za mama kulalia na za kumpangusa mtoto mzawa na kumfunika
  • Wembe mpya wa kukata kambakitovu
  • Uzi safi mpya wa kufungia kitovu
  • Sabuni, burashi ya kusugua na (ikiwezekana) alkoholi ya tiba ili kutakasa
  • Maji safi ya kunywa, kumwosha mama na mikono yako.
  • Ndoo tatu kubwa au bakuli.
  • Vifaa vya kutengenezea vinywaji vya kuongeza maji mwilini, 'atmit’ au chai.
  • Tochi ikiwa hakuna umeme katika eneo lile.
Mchoro 13.2 Vifaa ambavyo mama anapaswa kutayarisha kwa ajili ya kuzaa.

13.6.3 Kujiandalia matatizo na kupangia matukio ya dharura

Kama ilivyodokezwa hapo awali, kujiandalia matatizo ni utaratibu wa kutazamia hatua zinazohitajika ikiwa jambo la dharura litatokea, na pia kufanya mpango wa dharura (Kisanduku 13.5). Matatizo yanayohusiana na ujauzito kama vile shinikizo la juu la damu na kuvuja damu yanaweza kutokea wakati wowote katika ziara za utunzaji katika ujauzito, na ugonjwa wowote unaweza kutokea wakati wa ujauzito. Hali hizi zinapokisiwa katika awamu yoyote ya ujauzito, unapaswa kumpa mwanamke huyo rufaa mara moja na urudie kumshauri aje kukuona au kutafuta huduma ya kitabibu haraka iwapo dalili za hatari zitaonekana.

Kisanduku 13.5 Katika hali ya dharura

Hakikisha kuwa mwanamke na mumewe pamoja na watu wengine katika familia wanajua mahali pa kutafuta usaidizi.

  • Waharifu kupangia usafiri kwa kuwasiliana na wamiliki gari.
  • Wahimize kuweka hakiba ya pesa za usafiri, dawa na matibabu mengine.
  • Amua ni nani ambaye ataandamana na mama hadi kwenye kituo cha afya.
  • Amua ni nani atakayeitunza familia wakati mama hayupo.
  • Mwanamke mjamzito anaweza kuvuja damu kwa wingi wakati wa kuzaa au baada ya kuzaa hivyo anaweza kuhitaji kuongezewa damu. Hakikisha kuwa mama mjamzito au mume wake amewatambua watu wazima wawili wenye afya watakaokubali kumtolea damu ikiwa mama atahitaji. Wahakikishie watu wanaopangia kutoa damu kuwa hawataathirika kwa kutoa damu, na kwamba afya yao ya kijumla itakaguliwa kabla ya kutoa damu.

Sehemu muhimu ya kupangia matukio ya dharura ni kutazamia matukio yanayoweza kusababisha kukawia kunakoweza kuepukwa kwa mipango bora.

13.6.4 Visababishi vya kuchelewa kupata usaidizi wa dharura

Kuna aina tatu ya kuchelewesha usaidizi. Zote zinaweza kuwa hatari kwa mama na mtoto wake:

  • Mazoea ya kuchelewa kutafuta huduma ya kiafya (kukawia kuamua kutafuta huduma ya kimatibabu),
  • Kuchelewa kufika kwenye kituo cha afya
  • Kuchelewa kupata matibabu mwafaka.

Kuchelewa huku husababishwa na vipengele kadhaa, vikiwemo vikwazo vya kimipango na kifedha, na ukosefu wa maarifa kuhusu maswala ya kiafya ya kina mama na watoto wazawa. Kwa mfano, mama, familia yake na hata majirani wanaweza kuhisi kuwa ni mume tu au mtu mwingine wa familia aliyeheshimiwa anayeweza kumpa ruhusa mama akuite au apate huduma ya matibabu ya haraka katika kituo cha afya. Lakini kukawia huku kunaweza kuhatarisha maisha yake na ya mtoto.

Kuchelewa kuamua kutafuta huduma kunaweza kusababishwa na kushindwa kutambua dalili za matatizo, maswala kuhusu gharama, matukio mabaya ya awali kuhusu mfumo wa huduma ya afya na matatizo ya kiusafiri. Kuchelewa kufikia huduma kunaweza kusababishwa na umbali wa nyumba ya mwanamke mjamzito hadi kwenye kituo cha afya au mhudumu wa afya, hali ya barabara au ukosefu wa usafiri wa dharura.

Kuchelewa kupata huduma mwafaka kunaweza kupelekea upungufu wa vifaa vya kimsingi, ukosefu wa wataalamu wa afya na ujuzi duni wa wahudumu wa afya. Visababishi vya kukawia huku hutokea mara nyingi na vinaweza kutabirika. Hata hivyo, wanawake wajawazito, familia na jamii, wahudumu na vituo vya afya vilivyo karibu ni sharti wajitayarishe mapema kuchukua hatua za haraka iwapo dharura itatokea.

13.6.5 Kufanya rufaa

Hatimaye, unapaswa kufahamu hatua ya kuchukua unapofanya rufaa - kumhamisha mgonjwa ili apate huduma zaidi ya kiafya na utunzaji maalum katika kituo cha afya cha kiwango cha juu zaidi. Unapaswa kujaza fomu ya rufaa kikamilifu na utie sahihi na tarehe, kisha uhakikishe inaambatana na mteja kwenye kituo cha afya ulichomhamishia; fomu hii pia ina nafasi ya majibu kutoka kituoni kuhusu matibabu waliyompa mgonjwa.

Ikiwa hauna fomu sanifu ya rufaa, unapaswa kuandika arifa iliyo na taarifa muhimu (Kisanduku 13.6).

Kisanduku 13.6 Arifa ya rufaa
  • Tarehe na wakati wa rufaa
  • Jina la kituo cha afya unachomtuma mteja
  • Jina, tarehe ya kuzaliwa, nambari ya kitambulisho (iwapo inajulikana) na anwani ya mteja
  • Historia muhimu ya kitabibu ya mteja
  • Matokeo ya uchunguzi wa kimwili na vipimo
  • Utambuzi unaokisiwa
  • Matibabu yoyote uliyompa mteja
  • Sababu ya kumpa mteja rufaa
  • Jina lako, tarehe na sahihi.

Hii ndiyo tamati ya mjadala wetu kuhusu utunzaji maalum katika ujauzito. Katika vipindi vinavyofuata katika Moduli hii, utajifunza zaidi kuhusu vipengele maalum vya utunzaji katika ujauzito katika maandhari mahususi, pamoja na maswala ya uhamasisho wa kiafya katika ujauzito, kumshauri mwanamke mjamzito kuhusu dalili za hatari, kuzuia kusambazwa kwa VVU kutoka kwa mama hadi mtoto, utambuzi na udhibiti wa malaria, anemia na maambukizo ya mfumo wa mkojo, shinikizo la juu la damu, huaribikaji wa mimba na kuvuja damu katika awamu za kwanza na za mwisho za ujauzito. Moduli ya Utunzaji katika ujauzito inamalizia kwa kueleza jinsi ya kuingiza kanula na neli ndani ya mishipa ya vena ili kutia viowevu moja kwa moja katika mkondo wa damu na jinsi ya kuingiza katheta ya mkojo ili kumsaidia mama mjamzito kukojoa. Vipindi vya mafunzo ya kiutendaji vitahakikisha kuwa umepata maarifa haya.

Muhtasari wa Kipindi cha 13

Katika Kipindi cha 13 umejifunza kwamba:

  1. Utunzaji maalum katika ujauzito hutenganisha wanawake wajawazito wanaofaa kupata utunzaji wa kidesturi katika ujauzito (kipengele cha kimsingi) na wale wanaohitaji utunzaji maalum katika hali mahususi za kiafya au vipengele vya hatari.
  2. Utunzaji maalum katika ujauzito husisitiza kupanga utunzaji wa kibinafsi na wa watu waliolengwa na kupangia kuzaa.
  3. Utunzaji maalum katika ujauzito humfanya mwanamke mjamzito pamoja na mumewe na familia kushiriki katika utambuzi wa matatizo yanayohusiana na yasiyohusiana na ujauzito, kupangia na kufanya uamuzi kuhusu mwendo wa baadaye wa ujauzito.
  4. Hakuna mimba inayoweza kuwa 'bila hatari' hadi ithibitishwe.
  5. Mwanamke mjamzito ana ziara nne za utunzaji katika ujauzito na kila ziara ina malengo maalum ya kuhamasisha kuhusu utunzaji, afya ya mama na fetasi, kukadiria hatari na kufanya utambuzi wa mapema wa matatizo.
  6. Ziara ya kwanza ya utunzaji maalum katika ujauzito inapaswa kuwa kabla ya wiki ya 16 ya ujauzito; hukagua historia ya kimatibabu na kiukunga ya mwanamke, uchunguzi wa kimwili na matokeo ya vipimo ili kuamua iwapo mama anafaa kufuata sehemu ya kimsingi.
  7. Ziara ya pili ya utunzaji maalum katika ujauzito huwa kati ya wiki ya 24-28 ya ujauzito. Lengo zaidi ni kupima shinikizo ya damu na urefu wa fandasi ili kufahamu umri wa ujauzito.
  8. Ziara ya tatu ya utunzaji maalum katika ujauzito huwa kati ya wiki ya 30-32 ya ujauzito. Lengo la ziada ni kutambua iwapo mama amebeba mimba ya watoto wengi.
  9. Ziara ya nne ya utunzaji maalum katika ujauzito huwa ya mwisho kati ya wiki ya 36 na 40 ya ujauzito. Lengo la ziada ni kugundua ikiwa fetasi inatanguliza matako, iwapo ina mkao wa kukingama, na ishara za matatizo ya shinikizo la juu la damu. Makinika zaidi kuwaeleza wanawake kuhusu kujitayarishia kuzaa, kujiandalia matatizo na kupangia matukio ya dharura.
  10. Kujiandalia matatizo na kupangia matukio ya dharura hutazamia na kutayarishia hatua zinazohitajika iwapo jambo la dharura litatokea, ikiwa ni pamoja na kupangia usafiri, fedha, wasaidizi na watu waa kutoa damu na kupunguza mambo yanayopelekea kukawia kufika kwenye kituo cha afya cha kiwango cha juu zaidi.
  11. Wanawake wanaohitaji rufaa katika awamu yoyote ya ujauzito, au leba inapoanza wanapaswa kuandikiwa arifa ya rufaa iliyo na maelezo ya historia yao, utambuzi na matibabu.

Maswali ya Kujitathmini ya Kipindi cha 13

Kwa kuwa sasa umekamilisha kikao hiki, jibu maswali yafuatayo ili kubaini jinsi ulivyotimiza Malengo ya Masomo ya kipindi hiki. Andika majibu yako katika shajara yako ya masomo na uyajadili na mkufunzi wako katika Mkutano Saidizi wa Somo unaofuata. Unaweza kudhibitisha majibu yako ukilinganisha na vidokezo ulivyoandika katika Maswali ya Kujitathmini yaliyo mwishoni mwa Moduli hii.

Swali la Kujitathmini 13.1 (linatathmini Malengo ya Somo la 13.1, 13.2 na 13.4)

Ni elezo lipi ambalo si kweli?? Katika kila kauli, eleza lisilo la kweli.

  • A.Utunzaji maalum katika ujauzito huwalenga wanawake wajawazito pekee.
  • B.Wanawake katika sehemu ya kimsingi huwa na ziara 4 tu katika utunzaji maalum katika ujauzito isipokuwa wakati ishara na dalili za tahadhari zitatambulika katika awamu yoyote ile.
  • C.Wanawake wajawazito hawafai kutayarisha vifaa vyovyote vya leba na kuzaa.
  • D.Ratiba ya uzalishaji katika utunzaji maalum katika ujauzito ni sawa kwa kila mwanamke, naye hujulishwa kuhusu utunzaji huu katika ziara ya nne.
  • E.Proflaksisi katika utunzaji maalum katika ujauzito hulenga kuzuia magonjwa ya zinaa, ikiwa ni pamoja na kusambaza VVU kutoka kwa mama hadi mtoto, malaria, upungufu wa kilishe, anemia na pepopunda.
Answer

A si kweli. Utunzaji maalum katika ujauzito hauwalengi wanawake wajawazito pekee (hili lilitendeka katika mtazamo wa kitamaduni). Utunzaji maalum katika ujauzito hujumuisha mwenzi wa mwanamke na hata familia yote kumtunza mama wakati wa ujauzito, kuchunguza dalili za hatari na kujiandalia kuzaa, kujitayarishia matatizo na kupandia matukio dharura.

B ni kweli. Wanawake katika sehemu ya kimsingi huwa na ziara 4 tu katika utunzaji maalum katika ujauzito, isipokuwa ishara au dalili za tahadhari zinapogunduliwa katika awamu yoyote.

C sikweli. Mwanamke mjamzito anapaswa kujitayarishia leba na kuzaa kwa kukusanya nguo safi kabisa, wembe mpya, uzi mpya ulio safi, sabuni na burashi ya kusugua, maji safi ya kuosha na kunywa, ndoo na bakuli, vifaa vya kutengenezea vinywaji na tochi.

D si kweli. Ratiba ya kuzaa katika utunzaji maalum katika ujauzito huwa ya kibinafsi kwa kila mwanamke na mwenziwe na huheshimu matakwa na hiari ya mama. Ratiba hii hujadiliwa katika ziara ya tatu na kurudiwa inapohitajika katika ziara ya nne.

E ni kweli. Proflaksisi katika utunzaji maalum katika ujauzito hulenga kukinga magonjwa ya zinaa pamoja na kusambazwa kwa VVU kutoka kwa mama hadi mtoto, malaria, upungufu wa kilishe, anemia, maambukizi katika mfumo wa mkojo na pepopunda.

Mwisho wa jibu

Swali la Kujitathmini la 13.2 (linatathmini Malengo ya Somo la 13.3 na 13.5)

Tuseme kwa mfano kwamba mwanamke mjamzito aliye na umri wa miaka 27 anayeitwa Aster amekuja kukuona. Yeye anakueleza kuwa ana mimba ya kwanza na alipata hedhi ya mwisho wiki 25 zilizopita. Ni hatua gani utakazochukua katika ziara hii ya kwanza? Kwa kawaida, ziara ya pili ya Aster itakuwa lini?

Answer

Kwa vile Aster ana mimba ya wiki 25, unapaswa kufanya huduma zote za ziara ya kwanza na ya pili za utunzaji maalum katika ujauzito. Makinika katika kuchunguza historia yake ya kimatibabu na kiukunga na ufanye uchunguzi kamili wa mwili ikiwa ni pamoja na shinikizo la damu, mpigo wa moyo, halijoto, pumzi, uchunguzi wa tumbo ili kupima urefu wa fandasi, sikiliza mpigo wa moyo wa fetasi, tazama kutanguliza na mkao wa fetasi na ukague matokeo ya vipimo vya mkojo. Kusudi la hatua hizi ni kutambua iwapo Aster anafaa kufuata sehemu ya kimsingi ya utunzaji. Pia mshauri kuhusu lishe, usafi na mapumziko.

Iwapo ana afya njema na mimba inaendelea kwa hali ya kawaida, mweleze kuwa ziara itakayofuata ni kati ya wiki ya 30- 32 ya ujauzito, lakini ni sharti atafute usaidizi mara moja iwapo atapata dalili zozote za hatari, kama vile kuvuja damu, mchozo unaonuka kutoka ukeni, homa, kiwaa au kisulisuli na kuchanganyikiwa.

Mwisho wa jibu

Swali la Kujitathmini la 13.3 (linatathmini Malengo ya Somo ya 13.3 na 13.5)

Tuseme Aster amekuja kwako akiwa na mimba ya wiki 32. Unatambua kuwa shinikizo lake la damu ni mmHg 120/60, ana konjaktiva iliyokwajuka kidogo na urefu wa fandasi ni wa kipimo cha fandasi ya wiki ya 38. Ishara hizi zinaonyesha nini na ni hatua zipi utakazochukua?

Answer

Konjaktiva iliyokwajuka inaonyesha kuwa huenda Aster ana anemia, hivyo mwulize kuhusu lishe yake- anakula nini na ni kiwango kipi cha chakula anachopata kila siku? Chukua vipimo vingi vya mkojo kwa kutumia kijiti cha kupimia ili kujua iwapo mkojo una sukari zaidi au protini. Ikiwa kipimo cha mkojo ni cha kawaida, mshauri kuboresha lishe na umpe tembe za foleti na ayoni.

Kwa vile fandasi ina urefu uliopita matarajio ya kawaida katika wiki ya 32 ya ujauzito, inaweza kuashiria kuwepo kwa pacha au hali ya kipatholojia na Aster anapaswa kupewa rufaa ili achunguzwe katika kiwango cha juu zaidi. Hivyo basi, unapaswa kuandika arifa ya rufaa na umshauri kuenda katika kituo cha afya au hospitali iliyo karibu. Aster anaweza kuhitaji usaidizi katika kupangia usafiri au fedha za kusafiri. Mshauri Aster kuhusu kujiandalia kuzaa, kujitayarshia matatizo na kupangia matukio ya dharura.

Mwisho wa jibu