Magonjwa ya kihipatensheni ya ujauzito ni mojawapo ya visababishi vitatu vikuu vya maradhi na vifo (pamoja na kutokwa na damu, na maambukizi) kwa kina mama. Mchango wa hipatensheni (shinikizo la juu la damu) kwa vifo na maradhi ya fetasi na watoto wachanga pia ni mkubwa. Magonjwa ya kihipatensheni yanaweza kutatiza hadi asilimia 10 ya ujauzito wote, huku kiwango kikubwa zaidi cha asilimia hiyo kikitokea katika wanawake walio na ujauzito wa kwanza (primigravida). Hipatensheni hufafanuliwa kama shinikizo la damu zaidi ya 140/90mmHg, ambapo nambari ya juu ndiyo shinikizo la sistoli na nambari ya chini ndiyo shinikizo la diastoli.
Shinikizo la damu hupimwa kwa milimita za zebaki (mmHg)kwa sababu vifaa vya kwanza vilikuwa na zebaki.
Je, unakumbuka kinachomaanishwa na shinikizo la sistoli na la diastoli?
Shinikizo la sistoli ni shinikizo la damu katika mishipa ya damu moyo unaponywea. Shinikizo la diastoli hupimwa moyo unapolegea katikati ya mipigo.
Mwisho wa jibu
Jukumu kuu la huduma yako ya utunzaji katika ujauzito ni kuwafahamisha wanawake wajawazito kuhusu dalili za hatari za magonjwa ya kihipatensheni, kuchunguza shinikizo lao la damu katika kila safari (ulijifunza jinsi ya kufanya hivi katika Kipindi cha 9), na kufanya utambuzi wa hipatensheni kwa wakati unaofaa na kuwapa rufaa wanawake walioathiriwa mapema iwezekanavyo.
Katika kipindi hiki, utajifunza kuhusu mabadiliko katika mwili wa mwanamke kutokana na hipatensheni na jinsi yanavyoathiri mama na fetasi, uainishaji wa hipatensheni, visababishi vikuu, jinsi ya kutambua aina tofauti, na hatua utakazochukua ili kuzuia matatizo yanayokithiri na hata kifo.
Baada ya kusoma somo hili, unapaswa uweze:
19.1 Kufafanua na kutumia kwa usahihi maneno yote muhimu yaliochapishwa kwa herufi nzito. (Maswali ya Kujitathmini 19.1, 19.2 na 19.3)
19.2 Kueleza kwa kifupi kinachotendeka kwenye mishipa ya damu na viowevu vya mwili kwa wanawake walio na hipatensheni, na jinsi kinavyoweza kuidhuru fetasi. (Maswali ya Kujitathmini 19.1 na 19.2)
19.3 Kufafanua aina tofauti za magonjwa ya kihipatensheni ya ujauzito. (Maswali ya Kujitathmini 19.2 na 19.3)
19.4 Kuorodhesha visababishi vikuu vya hipatensheni inayohusiana na ujauzito. (Swali la Kujitathmini 19.3)
19.5 Kueleza dalili za kiafya zinazotokea sana za priklampsia kali. (Swali la Kujitathmini 19.3)
19.6 Kutambua matatizo yanayotokea sana ya magonjwa ya kihipatensheni ya ujauzito kwa mama na fetasi/mtoto mchanga. (Swali la Kujitathmini 19.3)
19.7 Kutoa matibabu saidizi ya kimsingi na kuwezesharufaa ya mapema, hasa kwa wanawake walio na magonjwa makali ya kihipatensheni ya ujauzito. (Swali la Kujitathmini 19.3)
Kisababishi hasa cha hipatensheni inayohusiana na ujauzito bado hakijulikani. Hata hivyo, hipatensheni inajulikana kusababisha magonjwa katika sehemu tofauti za mwili; hasa huathiri ubongo na uti wa mgongo, moyo na mishipa ya damu, damu, figo, na ini.
Tukio linalojulikana sana kwa mwanamke anayepata hipatensheni katika ujauzito ni kuwa kuta za misuli za mishipa ya damu mwilini mwote hunywea, na kwa hivyo nafasi ndani ya mishipa hupungua. (Jina maalum la hali hii ni msongo wa mishipa kote mwilini.) Msongo huu wa mishipa husababisha shinikizo la juu la damu katika mishipa ya damu, na hii ni sababu moja ya kiowevu kutoka kwa damu kusukumwa nje kupitia kuta za mishipa na kukusanyika kwenye tishu za mwanamke huyo.
Je, uvimbe unaotokana na kukusanyika kwa kiowevu kwenye tishu huitwaje, na ni wapi ambapo uvimbe unaoneka sana kwa wanawake wajawazito walio na hipatensheni? (Ulijifunza kuhusu haya katika Kipindi cha 7 na cha 8, hasa Kisanduku 8.2.)
Uvimbe huu huitwa edema na ni ishara ya hatari ya hipatensheni katika ujauzito. Huonekana mara nyingi katika sehemu ya chini ya miguu, vifundo na nyayo; pia mikono, na kwenye uso na mgongo katika hali kali sana.
Mwisho wa jibu
Aina yoyote ya hipatensheni katika ujauzito ina athari kubwa kwa ukuaji na kuishi kwa fetasi. Hii hutendeka kutokana na kupungua kwa kiasi cha damu ya mama, jambo ambalo baadaye hupunguza uletaji wa damu kutoka kwa ateri za endometria hadi kwa plasenta. Ateri za endometria huleta damu ya mama kwa plasenta, na kuleta oksijeni kutoka kwa mapafu na virutubishi kutoka kwa mfumo wake wa umeng'enyaji hadi kwa fetasi. (Unaweza kuyaona ukitazama nyuma katika Mchoro 5.5 katika Kipindi cha 5.)
Je, ukuaji wa fetasi utaathiriwa vipi iwapo kiasi cha damu ya mama inayoingia kwenye plasenta kitapungua?
Upelekaji wa oksijeni, virutubishi, na viowevu kwenda kwa mtoto utapungua na kwa hivyo hatakua kikawaida. Ukuaji wa fetasi unaweza kuzuiliwa (hipatensheni katika ujauzito ni mojawapo ya visababishi vikuu vya uzuiaji wa ukuaji kwenye uterasi).
Mwisho wa jibu.
Kiwango cha kiowevu cha amnioni kinachozunguka fetasi pia kitakuwa kidogo kuliko kawaida kwa sababu damu inayofika kwenye figo za mtoto imepungua na kwa hivyo hutengeneza kiasi kidogo cha mkojo. Mwishoni mwa ujauzito, kiasi kingi cha kiowevu cha amnioni hutoka kwa mkojo wa mtoto. Fetasi inaweza kufariki kutokana na ukosefu wa oksijeni na virutubishi, au kutokana na kupungua kwa kiowevu cha amnioni. Iwapo fetasi itaishi muda mrefu kwenye uterasi huku ikipata oksijeni kidogo, ubongo unaokua unaweza kuathiriwa vibaya sana. Kutokana na hayo, mtoto huyu anaweza kuwa punguani baadaye iwapo atazaliwa akiwa hai na kuongoka katika maisha ya mapema utotoni.
Pia fetasi inaweza kufariki kwa sababu plasenta huzeeka mapema sana na kusababisha usambazaji duni wa damu kwa fetasi, kwa hivyo plasenta inaweza kujitenga mapema na kuta za uterasi. (Mtengo wa mapema huitwa kuachia kwa plasenta na utajifunza kuuhusu katika Kipindi cha 21.) Leba ya mapema inaweza kuanza yenyewe (Kipindi cha 17) na maisha ya mama pia yanaweza kuwa hatarini kutokana na kuachia kwa plasenta ambapo damu nyingi inaweza kupotezwa.
Matatizo ya aina yoyote ya magonjwa ya kihipatensheni kwa mama yanahusiana sana na msongo wa mishipa na usambazaji tena wa viowevu vya mwili (viowevu zaidi nje ya mishipa ya damu na kidogo ndani ya mishipa). Tukio hili husababisha:
Je, mwanamke atapata hali gani ya kiafya iwapo kiasi kikubwa cha seli nyekundu za damu yake kitaharibika?
Atapata anemia.
Mwisho wa jibu.
Matatizo kwa mama | Matatizo kwa fetasi |
---|---|
Eklampsia | Kuachia kwa plasenta |
Kutokwa na damu ndani ya kichwa (kutoka damu ndani ya fuvu la kichwa) | Asifiksia ya ndani ya uterasi (ukosefu mkubwa wa oksijeni kwenye uterasi) |
Anemia | Uzuiaji wa ukuaji ndani ya uterasi |
Idadi ya chini ya pleteleti, ugandaji duni wa damu, na hatari ya kutokwa na damu | Kuzaa kabla ya muda kamili kutimia |
Figo kutofanya kazi | Fetasi kufariki ndani ya uterasi |
Ini kutofanya kazi, au hata kuraruka kwa ini | Ugumu katika kupumua baada ya kuzaliwa (asifiksia ya mapema ya mtoto mchanga) |
Kiowevu kwenye mapafu (edema ya mapafu) | Upunguani |
Moyo kutofanya kazi | |
Upofu kamilifu wa muda |
Hipatensheni katika ujauzito inaweza kuwa ya mara ya kwanza, au inayoendelea au inayozidi kukithiri iliyokuwepo kabla ya ujauzito huo. Iwapo hipatensheni itatambuliwa kabla ya ujauzito au katika majuma 20 ya kwanza ya ujauzito, au ikiendelea kwa majuma sita baada ya mtoto kuzaliwa, hii hufafanuliwa kama hipatensheni sugu.
'Sugu' hueleza hali ya kiafya inayoendelea kwa muda mrefu.
Sababu ya kuainisha hipatensheni katika ujauzito ni kukuwezesha kuamua hatua utakazochukua katika kila aina. Aina zingine (kwa mfano priklampsia ndogo na hipatensheni itokanayo na ujauzito - tazama Kisanduku 19.2 hapa chini) zina matatizo machache na yasiyo makali kwa mama na fetasi: aina zingine (kwa mfano, priklampsia kali na eklampsia) zinaweza kuwa na matatizo mabaya ila zidhibitiwe haraka.
Priklampsia ndiyo aina ya magonjwa ya kihipatensheni inayotokea sana katika ujauzito na iliyoangaziwa sana katika majadiliano ya sehemu hii (tazama Jedwali 19.2 ). Hutokea katika nusu ya pili ya ujauzito (baada ya majuma 20 ya ujauzito, lakini hutokea sana baada ya majuma 28). Kuwepo kwa protini katika mkojo wa mwanamke (protinuria) ni ishara ya hatari. Protinuria nyingi hufafanuliwa kama kipimo chanya cha mkojo cha dipstick chenye matokeo zaidi ya au sawa na +2 kwenye kipimo cha dipstick hizo.
Aina | Shinikizo la juu la damu (lililopimwa mara mbili, saa sita kati ya vipimo hivi) | Protinuria | Dalili za ukali |
---|---|---|---|
Hipatensheni yaujauzito (hutokea katika ujauzito na kuisha baadaye) | Zaidi ya kipimo cha 140/90 mmHg | Hakuna protinuria nyingi | Hakuna |
Priklampsia ndogo | Kati ya 140/90 mmHg na 160/110 mmHg | Hakuna protinuria nyingi | Hakuna |
Priklampsia kali | Zaidi ya au sawa na 160/110 mmHg | Protinuria inayoonekana iwepo au isiwepo (matokeo ya kipimo cha dipstick zaidi ya au sawa na +2) | Maumivu ya kichwa, kiwaa, maumivu ya epigasriamu, kupungua kwa mkojo, kupungua au kutokuweko kwa kucheza kwa mtoto |
Priklampsia zaidi juu ya iliyokuwepo awali | Juu kuliko kabla ya ujauzito kwa mwanamke aliye na hipatensheni sugu | Protinuria inayoonekana nyingi zaidi au inayozidi | Kuwe au kusiwe na dalili za ukali |
Eklampsia ndiyo aina kali sana ya magonjwa ya kihipatensheni. Utambuzi hufanyika mwanamke aliye na priklampsia (mara nyingi sana), au aina nyingine yoyote ya magonjwa ya kihipatensheni anapopata matukutiko (matukutiko, Mchoro 19.1) au koma (kupoteza fahamu kabisa). Tukutiko hili ni kama lile linalotokea kwa mtu aliye na kifafa (katika Kiamhari: Yemitil Beshita). Utajifunza mengi kuhusu aina hii ya tukutiko baadaye katika kipindi hiki.
Katika hali nyingi, kutokea kwa priklampsia au eklampsia hakuwezi kutabirika na kisababishi hakijulikani. Hata hivyo, kuna visababishi vinavyojulikana kuhusiana na matatizo ya kihipatensheni ya ujauzito (Jedwali 19.1).
Kujua visababishi hivi kutakusaidia:
La muhimu pia ni kuwa unahitajika kujua ya kwamba mwanamke yeyote (bila kujali umri na idadi ya uzazi wa hapo awali) anaweza kupata magonjwa ya kihipatensheni katika ujauzito wowote. Kwa hivyo, ingawa ni vizuri kutarajia yatokee kwa wale walio na visababishi hivi, unaweza kuchukulia kuwa wanawake wote wajawazito wana uwezekano wa kupata hipatensheni.
Jinsi ulivyoona kaika Jedwali 19.2, priklampsia ndogo ni matokeo yanayoambatana na shinikizo la juu la damu kwa mwanamke asiye na dalili zingine za kihipatensheni. Hata hivyo, mwanamke aliye na priklampsia kali anaweza kuwa na lalamiko moja au zaidi ya dalili kali. Kutokana na maoni na masomo ya utafiti, hizi ndizo dalili za kiafya zinazotokea sana.
Ingawa kuna visababishi vingi vya maumivu ya kichwa katika ujauzito, hadi itakapothibitishwa kinyume, unapaswa kuchukulia kwanza kuwa maumivu ya kichwa yanaweza kutokana na aina kali ya hipatensheni. Edema ya ubongo (uvimbe kutokana na kiowevu kujikusanya ubongoni) na ongezeko la shinikizo ndani ya fuvu la kichwa (jina la kitiba la fuvu la kichwa ni kreniamu, kwa hivyo, madaktari huliita shinkizo la ndani ya kreniamu) ndivyo visababishi vikuu vya maumivu ya kichwa katika priklampsia kali.
Kiwaa na matatizo ya kuona pia hutokana na ongezeko la shinikizo ndani ya kreniamu, pamoja na edema ubongoni na kwenye retina (kiungo kilicho nyuma ya mboni ya jicho).
Edema kwenye ini inaweza kuwa na maumivu sana kwa sababu ini limefunikwa na kapsuli ambayo hukaza na kuuma ini linapokusanya kiowevu kingi sana kwenye tishu zake. Ini liko nyuma ya sehemu ya epigastriamu ya fumbatio uliyojifunza kutambua katika Kipindi cha 15 (tazama Mchoro 15.4). Visababishi vingine vya maumivu ya epigastriamu ni nadra katika ujauzito, kwa hivyo ujumbe ni: kwanza fikiria hipatensheni kwa mwanamke mjamzito (hasa baada ya majuma 28 ya ujauzito) anayelalamikia maumivu ya epigastriamu.
Kutolewa kwa mkojo hupunguka kwa kiwango kikubwa katika aina kali za hipatensheni inayohusiana na ujauzito. Kupungua kwa kiasi cha damu ya mama (kilichoelezewa katika Sehemu ya 19.1.1) hupelekea kupungua kwa damu inayofika kwenye figo na kutokana na haya, kutakuwa na upungufu mkubwa katika mkojo unaotolewa. Mwanamke huyo anaweza kukoma kutoa mkojo kabisa.
Hii hutendeka kwa sababu fetasi inapokea oksijeni na virutubishi kidogo kutokana na kupungua kwa damu inayopita kwenye plasenta, jinsi ilivyoelezwa hapo juu.
Edema ya mwili wote hujulikana kwa kuenea kwa edema kwa mgongo, fumbatio, mikono na uso wa mwanamke. Edema huchukuliwa kuwa ya patholojia ikiwa mama anaongeza uzani wa zaidi ya kilo 1.0 kwa juma. Ongezeko la kawaida la uzani kwa juma katika ujauzito ni kati ya kilo 0.25 hadi 0.75 (wastani kilo 0.5).
Ekilampsia hutokea mwanamke akikosa matibabu bora akiwa na priklampsia kali. Hili ndilo tatizo hatari sana la priklampsia kali. Inaweza kutokea kabla ya leba, katika leba na baada ya kuzaa. Wakati mwingine eklampsia inaweza kutokea kwa muda wa hadi saa 24 baada ya kuzaa, hata kwa wanawake waliozaa wakiwa na shinikizo la damu la kawaida na bila dalili zozote za hatari kabla na katika leba. Kwa hivyo mwanamke akija kwako na historia ya tukutiko baada ya leba na kuzaa kikawaida na hata wakati mwingine nyumbani, tatizo la kwanza la kiafya unalofaa kuzingatia ni eklampsia. Lakini unapaswa pia kujua kuwa kuna visababishi vingine vya tukutiko, kama vile kiwango cha chini au juu sana cha sukari katika damu (hipo au hipaglisimia), malaria yanayoathiri ubongo, maambukizi ya bakteria kwenye ubongo (kwa mfano meninjitisi), kiharusi, madawa, au kusumishwa.
Jinsi ulivyojifunza hapo juu, utambuzi wa eklampsia hufanywa dalili za kiafya za priklampsia zikiwepo, pamoja na:
Tukutiko katika eklampsia huwa la ghafla mwanzoni lakini katika visa vingine huenda kukawa na ishara na dalili za hatari zinazothibitisha kutokea kwa eklampsia (tazama Kisanduku 19.2).
Tukutiko katika eklampsia ni sawa na tukutiko kwa watu walio na kifafa. Kama tukutiko la kifafa, lina awamu nne:
Awamu ya utulivu
Sifa bainifu ya awamu ya kwanza ni kipindi cha utulivu (huenda kisichukue zaidi ya sekude 20) mtu anapokuwa na udhaifu wa misuli kwenye mwili wote, mkazo na mshtuko wa misuli, na macho yanayokodoa.
Awamu ya toni
Hii inaweza kudumu hadi sekunde 30 na huonyeshwa kwa aina kali ya mikazo ya misuli kwenye mwili wote ambapo misuli ya miguu na mikono hunywea sana na hata kuonekana thabiti kama kijiti kikavu. Katika awamu ya toni, mwanamke hukoma kupumua na kukosa oksijeni. Pia kuna kugeuzageuza macho na unaweza kuona sehemu ya juu ya sklera (sehemu nyeupe ya jicho).
Awamu ya kiklonasi
Awamu ya tatu inaweza kuchukua hadi dakika 2 na hasa ni mwendo wa mshtuko wa mwili wote kutokana na kunywea na kulegea kwa misuli. Katika awamu hii mwanamke anaweza kupumua na pia kutoa mate na mkojo.
Kipindi cha koma
Baada ya awamu ya kiklonasi, katika kisa dhahiri, mwanamke hupoteza fahamu kabisa kwa muda usiojulikana. Hata hivyo, mwanamke huyo anaweza kwenda katika koma mwanzoni kabisa (yaani, bila tukutiko hata moja). Muda wa hali ya koma hutegemea:
Jukumu la kwanza katika udhibiti wa magonjwa ya kihipatensheni ya ujauzito ni utambuzi wa mapema wa ishara na dalili za hatari na utoaji wa mara moja wa rufaa ya kwenda hospitalini au kituoni mwa afya. Ikiwezekana hakikisha usafirishaji wa haraka na mapokezi ya mwanamke huyo kwenye kituo hicho cha afya cha ngazi ya juu. Hatua zako zinapaswa kuzingatia utambuzi wako wa kiafya na ukali wa hipatensheni hiyo.
Wanawake wajawazito wanaotambuliwa kuwa na:
wanapaswa kupewa rufaa bila wewe kujaribu kutatua, hasa siku ya utambuzi.
Je, kwa nini unafikiri rufaa ni muhimu angali hipatensheni hiyo si kali?
Hii ni kwa sababu wakati mwingine aina ya hipatensheni isiyo kali inaweza kuendelea na kuwa aina kali kwa muda wa kipindi kifupi.
Mwisho wa jibu.
Unapaswa kutoa ushauri kwa mwanamke na familia yake kuhusu hatari ya matatizo ya mama na fetasi na umuhimu wa kupata matibabu ya kitaalamu mara moja. Katika visa vya eklampsia, watu katika sehemu nyingi za mashambani huamini kuwa matukutiko yanahusiana na roho za kishetani. Mwanamke mjamzito aliyepata tukutiko kwenye tamaduni hizi huenda asitake kwenda kituoni mwa afya kwa sababu angependelea kwenda kwa maji matakatifu, kasisi au kiongozi mwingine wa dini, au madaktari wa kienyenji. Una jukumu muhimu sana kuhakikisha kuwa mwanamke huyo na familia yake wameelewa kuwa matukutiko hayo husababishwa na shinikizo la juu la damu analopitia. Mhakikishie kuwa matukutiko hayo yatakoma baada ya kuzaa.
Jukumu lako la pili ni kutoa matibabu saidizi ili kuzuia kuzorota kwa hali kabla ya mwanamke huyo kufika kituoni mwa afya. Utambuzi wako wa kiafya unapokuwa kama ilivyofafanuliwa katika Jedwali 19.2 hapo awali:
unapaswa uweze kuzuia kutokea kwa eklampsia kwa kuchukua hatua saidizi zilizo katika Kisanduku 19.2 hapa chini.
Ukigundua mwanamke mjamzito aliye na ekilampsia, unapaswa kuchukua hatua zilizoelezwa katika Kisanduku 19.2. Mpe rufaa mara moja ila akiwa yuko mwishoni mwa leba - katika hali hii unapaswa kuzalisha mtoto na umpe rufaa pamoja na mtoto kwenda hospitalini mara moja baada ya uzazi huo.
Unapomsafirisha mwanamke aliye na eklampsia kwenda katika kituo cha afya, hakikisha kuwa amelala kwa upande njia yake ya hewa ikiwa imefunguka (Mchoro 15.2). Usimruhusu kulala chali kwa sababu anaweza kupata ugumu katika kupumua akipata tukutiko jingine. Kulala kwa upande pia humaanisha kuwa akitapika ana uwezekano mdogo wa kuvuta matapishi kwenye mapafu yake.
Katika kipindi kifuatacho, utajifunza kuhusu hali nyingine inayoweza kuhatarisha maisha: utokaji mimba na kutokwa na damu mwanzoni mwa ujauzito.
Katika Kipindi cha 19 umejifunza kuwa:
Kwa kuwa umekamilisha kipindi hiki, unaweza kutathmini jinsi umeweza kuyatimiza Malengo ya Somo la Kipindi hiki kwa kujibu maswali haya. Andika majibu katika Shajara yako na ujadiliane na Mkufunzi wako katika Mkutano saidizi wa Somo utakaofuata. Unaweza kulinganisha majibu yako na nakala kuhusu Maswali ya kujitathmini mwishoni mwa Moduli hii.
Je, ni gani kati ya kauli hizi si sahihi? Eleza kisicho sahihi kwa kila kauli.
A si kweli. Kuta za misuli za mishipa ya damu za mwili wote wa mwanamke zinaponywea, nafasi ndani ya mishipa hii hupungua, hivyo shinikizo lake la damu hupanda.
B ni kweli. Hipatensheni katika ujauzito hupunguza damu inayotoka kwenye ateri za endometria kwenye uterasi ya mama hadi kwa fetasi kupitia kwa plasenta.
C ni kweli. Hipatensheni hupunguza kiwango cha kiowevu cha amnioni kinaichozunguka fetasi kwa sababu kiasi cha damu inayoingia kwenye figo za mtoto ni kidogo na hivyo hutengeneza kiasi kidogo cha mkojo.
D si kweli. Kuna uwezekano mkubwa wa ukuaji wa fetasi kuzuiliwa kwa mwanamke mjamzito aliye na hipatensheni kwa sababu viwango vya oksijeni, virutubishi na viowevu vinavyomfikia mtoto kutoka kwa plasenta kupitia damu hupungua.
Mwisho wa jibu.
Kamilisha Jedwali 19.3 kwa vipimo ambavyo ungetarajia kupata kwa wanawake walioainishwa kuwa na aina za hipatensheni zilizoonyeshwa katika upande wa mkono wa kushoto.
Aina | Shinikizo la juu la damu | Protinuria | Dalili za ukali |
---|---|---|---|
Hipatensheni ya ujauzito | |||
Priklampsia ndogo | |||
Priklampsia kali | |||
Priklampsia zaidi juu ya iliyokuwepo awali |
Aina | Shinikizo la juu la damu | Protinuria | Dalili za ukali |
---|---|---|---|
Hipatensheni yaujauzito (hutokea katika ujauzito na kuisha baadaye) | zaidi ya kipimo cha 140/90 mmHg | Hakuna protinuria nyingi | Hakuna |
Priklampsia ndogo | Kati ya 140/90 mmHg na 160/110 mmHg | Hakuna protinuria nyingi | Hakuna |
Priklampsia kali | Zaidi ya au sawa na 160/110 mmHg | Protinuria inayoonekana iwepo au isiwepo (matokeo ya kipimo cha dipstick zaidi ya au sawa na +2) | Maumivu ya kichwa, kiwaa, maumivu ya epigasriamu, kupungua kwa mkojo, kupungua au kutokuweko kwa kucheza kwa mtoto |
Priklampsia zaidi juu ya iliyokuwepo awali | Juu kuliko kabla ya ujauzito kwa mwanamke aliye na hipatensheni sugu | Protinuria inayoonekana nyingi zaidi au inayozidi | Kuwe au kusiwe na dalili za ukali |
Mwisho wa jibu.
Soma uchunguzi maalumu ufuatao kisha ujibu maswali yatakayofuata.
Zewditu ni mwanamke primigravida mwenye umri wa miaka 37 na ana ujauzito wa pacha. Yeye ana uzani wa kupita kiasi ikilinganishwa na urefu wake. Mama huyu alikuwa mwenye afya njema hadi ujauzito wake ulipofika juma la 22, alipoanza kulalamikia maumivu ya kichwa na kuvimba nyayo na vifundo.
Mwisho wa jibu.