Skip to main content
Printable page generated Friday, 26 April 2024, 1:09 AM
Use 'Print preview' to check the number of pages and printer settings.
Print functionality varies between browsers.
Unless otherwise stated, copyright © 2024 The Open University, all rights reserved.
Printable page generated Friday, 26 April 2024, 1:09 AM

17. Kupasuka kwa Tando kabla ya Wakati (KTW)

Kipindi cha 17 Kupasuka kwa Tando kabla ya Wakati (KTW)

Utangulizi

Katika Kipindi hiki utajifunza kuhusu ufafanuzi, uainishaji na hatari za KTW.Tutaeleza matatizo yanayoweza kusababisha ugonjwa na hata kifo kwa mama.

Kipindi hiki pia kinakujulisha kuhusu matatizo yanayoweza kuhatarisha maisha ya fetasi na mtoto mchanga. Utajifunza jinsi ya kutambua dalili za KTW na hatua ambazo unaweza kuchukua unapokuwa na wanawake walio na shida ya KTW, ukizingatia unayoyajua kuhusu kutokwa na kiowevu kutoka ukeni kama mojawapo ya dalili hatari katika Kipindi cha 15.

Malengo ya Somo la Kipindi cha 17

Baada ya somo hili lazima uweze:

17.1 Kufafanua na kutumia kwa ufasaha maneno yote muhimu yaliyoandikwa kwa herufi nzito. (Swali la Kujitathmini17.1, 17.2 na 17.3)

17.2 Kueleza uainishaji wa KTW. (Swali la Kujitathmini 17.1 na 17.3)

17.3 Kueleza hatari tofauti zinazohusishwa na KTW. (Swali la Kujitathmini 17.2)

17.4 Kufafanua dalili za kutambua KTW. (Swali la Kujitathmini 17.2)

17.5 Kujadili matatizo ya KTW yanayoweza kutokea na kuathiri mwanamke na fetasi. (Swali la Kujitathmini 17.2 na 17.3)

17.6 Kuelezea hatua unazohitajika kutekeleza kwa mwanamke aliye na shida ya KTW. (Swali la Kujitathmini 17.2 na 17.3)

17.1 Kupasuka kwa Tando kabla ya Wakati (KTW)

KTW inafafanuliwa kama kutokwa na kiowevu cha amniotiki kutoka mfuko wa amniotiki ambapo mtoto huogelea; kiowevu hupitia kwenye tando za fetasi zilizopasuka, hii hutokea baada ya wiki 28 za kipindi cha ujauzito na angalau saa 1 kabla ya kuanza kwa leba. KTW unaweza kutokea kabla au baada ya wiki 40 ya kipindi cha ujauzito kwa hivyo ‘kabla ya wakati ‘haimaanishi kuwa umri wa fetasi katika kipindi cha ujauzito haujakamilika.

Kabla ya wakati inamaanisha kupasuka kwa tando za fetasi kabla ya leba kuanza. KTW ni tatizo kwa sababu sio kawaida na huhusishwa na matatizo mengi (zitakazoelezwa baadaye katika Kipindi hiki.) Katika leba ya kawaida, tando za fetasi hupasuka baada ya leba kuendelea kwa muda, wakati kichwa cha fetasi kimeshirikishwa na kupanuka kwa seviksi bila tatizo kwa wanawake waliopo katika leba. (Utajifunza kwa kina kuhusu maendeleo ya leba katika Moduli inayofuata, (Utunzaji wa leba na kuzaa)

Unapaswa kufahamu kuwa watu wengi barani Afrika hawajui kwamba KTW ni shida. Bali hudhania kutokwa na kiowevu ni dalili nzuri ya leba inayokuja. Kama utakavyoelewa baadaye katika kipindi hiki, matatizo mengi ya hatari yanaweza kutokea kutokana na KTW. Kwa hivyo, unapaswa kumshauri mwanamke, mume wake na famillia yake kuhusu hatua wanazopaswa kuchukua tando zake zikipasuka na kiowevu kutoka ukeni kabla ya leba kuanza.Wajulishe hatari za kukaa nyumbani baada ya kupasuka kwa tando. Tunaanza kwa kueleza jinsi unavyoainisha hali za KTW, zinazokusaidia kuzishughulikia hali hizo.

17.2 Uainishaji wa Kupasuka kwa Tando kabla ya Wakati (KTW)

KTW huainishwa kulingana na umri wa kipindi cha ujauzito wakati tando hupasuka na muda kati ya kupasuka kwa tando la fetasi na mwanzo wa leba.

KT W unaotokea kabla ya muda hufanyika baada ya wiki 28 za umri wa kipindi cha ujauzito na kabla ya wiki 37.

KTW unaotokea katika muda halisi hufanyika baada ya wiki 37 zilizokamilika za umri wa kipindi cha ujauzito zikiwemo hali za baada ya kipindi zinazotokea baada ya wiki 40.

Kupasuka kwa tando kabla ya muda na katika muda halisi unaweza kutenganishwa zaidi:

  • KTW unaotokea mapema (masaa 12 hayajapita tangu kupasuka kwa tando za fetasi.)
  • KTW unaoendelea kwa muda mrefu (masaa 12 au zaidi yamepita tangu kupasuka kwa tando ya fetasi.)

Sababu kuu za kuainisha KTW katika muda halisi, kabla ya muda, mapema na unaoendelea kwa muda mrefu ni kwa sababu ya kutekeleza uamuzi wa kudhibiti. Jinsi kunavyotokea mapema (KTW unaotokea kabla ya muda.) na jinsi muda ulivyo mrefu kati ya kupasuka kwa tando za fetasi na kuanza kwa leba, ndivyo kulivyo na uwezekano wa matatizo mengi zaidi. Tutaeleza hatua unazopaswa kuchukua ili kudhibiti hali za KTW katika kitengo cha 17.6 cha kipindi hiki. Kwanza tujadili vipengele vya hatari vya KTW na matatizo yanayoweza kutokea kwa mama na fetasi.

17.3 Vipengele vya hatari ya KTW

Kupasuka kwa tando za fetasi unaweza kutokea wakati seviksi imefungwa au imepanuka. Wakati mwingine inaweza kutokea katika ujauzito wa mapema (baada ya wiki 28 - hii husababisha utokaji wa mimba usioweza kuepukika, ambayo utajifunza katika Kipindi cha 20), au katika awamu ya tatu (kati ya wiki 28 na wiki 34). Haijulikani nini husababisha kupasuka kwa tando za fetasi kabla ya kuanza kwa leba. Hata hivyo, kunavyo vipengele vya hatari vinavyohusishwa sana na KTW.

Zingatia kaviti ya amniotiki kuwa kifuko (au mfuko) ambacho kuta zake zimetengenezwa na tando za fetasi, zinazofungia fetasi na kiowevu cha amniotiki. Sehemu iliyodhaifu ya mfuko hupasuka, ambapo ni sehemu ya tando ambazo zimeshikana moja kwa moja na ‘mdomo’ wa seviksi. Upasukaji hutokea wakati mfuko umeharibiwa na maambukizi au jeraha la nje, au kupanuka zaidi (kuvimba) na kushindwa kustahimili shinikizo. Vipengele hivi vya hatari vimemeelezwa kwa ukamilifu hapo chini.

17.3.1 Maambukizi yanaweza kusababisha KTW

Bakteria inaweza kusababisha maambukizi katika mkondo wa chini wa viungo vya uzazi (maambukizi ya seviksi au ukuta wa uke) zinaweza kupanda juu kupitia seviksi na kuambukiza tando za fetasi. Hili linaweza kudhoofisha tando hadi zipasuke.

Kisanduku 17.1linatoa muhtasari wa dalili za kutambua maambukizi ya KTW kwa mwanamke.

Kisanduku 17.1 Thibitisho la maambukizi kwa mwanamke aliye na shida ya KTW.
  • Joto jingi: mwanamke anaweza kulalamika kuwa anahisi joto au unaweza kunakili halijoto yake ya sentigredi 38 au zaidi.
  • Mchozo kutoka ukeni unaoweza kuwa na harufu mbaya na rangi inaweza kubadilika kutoka hali ya majimaji na kuwa yenye mawingu.
  • Anaweza kuwa na ongezeko la mpigo wa moyo (zaidi ya mipigo 100 kwa dakika)
  • Mpigo wa moyo wa fetasi unaweza kuongezeka hadi mipigo 160 kwa dakika au zaidi.
  • Anaweza kuhisi maumivu katika sehemu ya chini ya fumbatio lake, hasa linapoguswa.

17.3.2 Mlalo mbaya wa fetasi

Kupasuka kwa tando za fetasi huhusisha sana mlalo mbaya wa fetasi katika awamu ya tatu. Hasa hatari ya KTW zinahusisha uzazi wa miguu kukaa vibaya (miguu kutangulia) na kulala vibaya (kutoka upande mmoja wa fumbatio hadi mwingine) huku mgongo wa mtoto ukijisimamisha juu na mikono na miguu ikielekea juu, ikigusa sehemu iliyodhoofika ya tando.

17.3.3 Ujauzito ya watoto wengi na kiowevu kingi cha amniotiki

Ikiwa uterasi imeshikilia watoto wawili au zaidi, au mkusanyiko wa kiowevu kingi cha amniotiki (polihidramniosi), tando za fetasi huvutika zaidi na kupasuka. Tando zinaweza kupasuka ikiwa kiwango cha kiowevu cha amniotiki ni kidogo, ikiwa kuna njia nyingine ya kusababisha kama zilizoelezwa hapo chini.

‘Poli’ inamaanisha kingi, ‘hidra’ inamaanisha maji, na ‘amniosi’ inarejelea kiowevu cha amniotiki. Hivyo ‘polihidramniosi’ inamaanisha kiowevu kingi cha amniotiki.

17.3.4 Seviksi dhaifu

Bila mikazo ya uterasi, seviksi inaweza kupanuka mapema katika kipindi cha ujauzito na hii inaweza kuwa sababisho la utokaji wa mimba (kuharibika kwa mimba). Seviksi inaweza kupanuka hata baadaye katika kipindi cha ujauzito kabla ya kuanza kwa leba. Sehemu ya tando za fetasi zitaruhusiwa kupita, wakati seviksi inaendelea kupanuka. Kwa hivyo, tando zinaweza kupasuka kwa urahisi na kufanya kiowevu cha amniotiki kutoka.

17.3.5 Jeraha la fumbatio

Jeraha lolote butu au linalopenya kwa kuta za fumbatio linaweza kusababisha kupasuka kwa tando za fetasi. Majeraha butu hutokana na: daktari au mkunga kugusa uterasi ili kubadili mlalo wa fetasi kutoka hali ya miguu kutangulia au mlalo unaomkinga mama ili alale kwa hali kawaida ‘kichwa chini’ au kulala kwa veteksi; ukandaji wa uterasi na daktari wa kiasili; na majerahi butu ya fumbatio (kwa mfano, kutokana na pigo au kuanguka). Mfano wa jeraha la fumbatio linalopenya ni kuingiza sindano tupu kwa kaviti ya amniotiki kupitia kuta za fumbatio, au kupitia seviksi, ili kutoa kiowevu cha amniotiki au tishu ya plasenta ili kuifanyia uchunguzi.

17.4 Utambuzi wa KTW

Wakati kuna mpasuko katika tando za fetasi, mwanamke hugundua utokaji wa kiowevu ambacho huwa ni kingi sana na majimaji, kutoka ukeni bila uchungu wowote. Hata hivyo, wakati kiowevu cha amniotiki ni kidogo, kiowevu kinachotoka kinaweza kulowesha nguo za ndani, na utakuwa na uhakika wa kutekeleza utambuzi wa KTW kutokana na malalamishi ya mwanamke.

Mama anaweza kuwa na wasiwasi, lakini hana uhakika kama utokaji wa kiowevu ni kawaida au sio kawaida. Ni kawaida kwa mchozo kutoka ukeni na kuongezeka kwa kiasi kidogo mwanamke anapokaribia mwisho wa ujauzito, na hili linaweza kutatanishwa na utokaji wa kiowevu cha amniotiki. Kwa hivyo unapaswa kumpa rufaa mwanamke yeyote anayelalamika kuhusu utokaji wa mchozo ukeni kwa utathmini zaidi katika kituo cha afya cha juu, iwapo mwanamke anaonyesha ishara za KTW.

Kisanduku 17.1 linafupisha dalili za ugonjwa ambayo unaweza kukusaidia kutekeleza utambuzi wa KTW.

Kisanduku 17.1 Dalili za ugonjwa ya KTW

  • Mwanamke hulalamika kuhusu utokaji wa kiowevu kutoka ukeni (kidogo sana au kingi zaidi.)
  • Aligundua kupungua kwa ukubwa wa fumbatio lake baada ya kutokwa na kiowevu.
  • Unaona kiowevu cha majimaji kinachotoka ukeni, au nguo za ndani zimelowa kiowevu cha majimaji.
  • Unapopima umbali kati ya simfisis ya mfupa wa kinena na urefu wa fandasi (kama ilivyoelezwa katika Kipindi cha 9), unapata kuwa mtoto ni mdogo katika kipindi cha ujauzito. (Fahamu ya kwamba kuwa ‘udogo wa kipindi cha ujauzito’ inaweza pia kusababishwa na uhaba wa kiwango cha kiowevu cha amniotiki na tando zisizoharibika, kizuio cha uvimbe wa ndani ya uterasi, na tarehe ambayo si sahihi kwa umri wa kipindi cha ujauzito uliyotajwa.)
  • Katika KTW, kiowevu cha amniotiki kilichobakia kwenye mfuko kitakuwa kidogo. Kwa hivyo unaweza kuhisi (chunguza kwa kugusagusa) sehemu za fetasi kwa urahisi kupitia fumbatio la mama.
  • Hata kama si dhairi, mwanamke anaweza kuwa na harufu mbaya inayosababishwa na mchozo ukeni, na kuwa na joto jingi mwilini (tazama Kisanduku 17.1 hapo juu); dalili hizi zinaashiria maambukizi ambayo tayari yamedhibitishwa, yanaweza kuwa sababisho la KTW.
  • Unaweza kumpatia pedi iliyokauka au Goth na uiangalie baada ya masaa fulani kama ni majimaji au bado ni kavu. Fahamu kuwa ikikauka haimaanishi kuwa hakuna uwezekano wa KTW.

17.5 Matatizo ya KTW

KTW inahusishwa na matatizo kadhaa zinazoweza kutisha maisha, kama tutakavyoeleza.

17.5.1 Maambukizi baada ya KTW

Kupasuka kwa tando za fetasi kabla ya wakati huruhusu bakteria kuingia katika kaviti ya uterasi, kama ilivyoelezwa hapo awali, Huzaana haraka katika maeneo yaliyovuguvugu, majimaji na kutokana na hayo, mama pamoja na fetasi wanaweza kupata maambukizi yanayotisha maisha.Yanaweza pia kuendelea hata baada ya kuzaa kama uterini au maambukizi yaliyoeneaa kwa upana kwa mama, na kusababisha nimonia, sepsis (maambukizi ya damu) au meninjitisi (maambukizi ya ubongo) katika mtoto mchanga.

Maambukizi ni mojawapo ya matatizo ya KTW yanayohofiwa sana kwa sababu, yasipotibiwa haraka, yanaweza kusababisha kifo kwa mama na fetasi au mtoto mchanga. Lakini habari njema ni kuwa ukitibu haraka kwa kutumia antibiotiki mara nyingi hufaulu.

Lazima ifahamike kuwa hali za KTW zinazoendelea kwa muda mrefu isipotibiwa na antibiotiki ya kukinga, zinaweza kusababisha maambukizi ya uterasi.

  • KTW inayochukua muda mrefu inaweza kusababisha maambukizi kwa nini?

  • Masaa 12 yamepita tangu tando za fetasi zipasuke, kwa hivyo bakteria yoyote inayoingia katika uterasi inayo muda wa kutosha kuzaana na kujishikilia.

    Mwisho wa jibu

17.5.2 Kushuka kwa kambakitovu

Mchoro 17.1 Kushuka kwa kambakitovu ni tatizo la hatari ya KTW.

Kushuka kwa kitovu ni mojawapo ya matatizo ya KTW zinazoweza kusababisha kifo cha mtoto. (Jina ‘prolapse’ linamaanisha ‘kusukuma kutoka mahali panapokaa’.) Tando zinapopasuka, kambakitovu inaweza kusukumwa kuelekea chini na mkurupuko wa kiowevu cha amniotiki na kuanguka ikielekea kwenye uke. Inaweza kusukumwa mbele ya mtoto mpaka kwenye seviksi (tazama Mchoro 17.1) kupitia mpasuko katika tando. Katika hali hii kambakitovu iliyoshuka hubanwa kwa urahisi, na hivyo kuzuia usafirishaji wa damu kwa fetasi na hili linaweza kusababisha kifo cha ghafula ya fetasi.

17.5.3 Upungufu na ukosefu wa hewa kwa fetasi

Tando za fetasi zilizopasuka zinapotoa viowevu vingi vinavyomfanya mtoto ‘kuelea’katika uterasi, tando zinapasuka zikimzunguka mtoto, na mtoto anaweza kujifinyilia kwa ukuta wa uterasi. Anaweza kulala na kubana kitovu, kwa hivyo fetasi inapungukiwa na oksijeni na uchafu wa doksidi ya kaboni unabaki kwa mwili.

Upungufu wa oksijeni na mkusanyiko wa doksidi ya kaboni katika mwili unaitwa haipoksia (hasa ‘kiwango cha chini cha oksijeni’), ambacho husababisha asifiksia (haipoksia uharibu ubongo na tishu) inayosababisha kifo ikiwa oksijeni haitarejeshwa haraka.

Fetasi pia inaweza kupata asifiksia na kufa kwa sababu ya kuachana kwa sehemu ya kondo la uzazi au kondo lote.

17.5.4 Kukatika kwa plasenta

Ikiwa sababisho la kupasuka kwa tando za fetasi ni uterasi iliyovutika, kunao uwezekano wa kuachana kwa plasenta kutoka ukuta wa uterasi kabla ya wakati (hali inayoitwa kuachana kwa plasenta ambapo utajifunza zaidi katika Kipindi cha 21). Hii inaweza kutokea wakati ambako mbubujiko wa kiowevu hutiririka kwa ghafula, kisha kupasua sehemu ya plasenta kutoka kwa ukuta wa uterasi.

17.5 Leba inayoanza kabla ya muda

Mara tu kuta za fetasi zinapopasuka, kwa kawaida leba huanza kabla ya wiki moja. Ikiwa KTW itatokea wiki kadhaa kabla ya ujauzito kufikia mwisho, leba inayotokea pia itakuwa kabla ya muda halisi, na hii inaweza kuleta hatari kwa mtoto mchanga. Kukua kwake kunaweza kuwa hakujakomaa ya kutosha kustahimili uhai - kwa mfano mtoto aliyezaliwa kabla ya muda halisi hawezi kudumisha halijoto yake kama mtoto aliyezaliwa kwa kawaida, uvutaji pumzi wake utakuwa na shida, na anaweza kuwa na shida ya kulishwa na pia mfumo wa kingamwili unaweza ukashindwa kumkinga kutokana na maambukizi.

17.5.6 Ulemavu wa viungo vya fetasi

Wakati mwingine leba haianzi baada ya KTW. Hali huwa ni hatari na waweza kupata maambukizi na ulemavu wa fetasi, ikiwa itatokea mapema wakati wa ujauzito na ujauzito kuendelea kwa muda mrefu baada ya tando kupasuka.

Pasipo na kiowevu cha amniotiki cha kuifanya fetasi ‘kuelea’, kuta zenye misuli ya uterasi huzingira fetasi kwa karibu na kuibana. Mifupa isiyokomaa ya fetasi tayari haina nguvu za kutosha za kukinga shinikizo, na kuna uwezekano wa kupata ulemavu wa miguu, nyayo, mikono au viganja ikiwa ujauzito utaendelea katika hali hii kwa muda wa zaidi ya wiki 3.

17.6 Hatua za kuchukuwa ikiwa KTW itatokea

Ukimwona mwanamke unayedhania au aliye katika hali ya KTW, unapaswa kujibu maswali haya:

  1. Je mwanamke anayo leba iliyodhibitishwa au la?
  2. Ikiwa mwanamke anayo leba iliyodhibitishwa:
    • Je, ni KTW unaotokea kabla ya muda au katika muda halisi?
    • Je, amekuwa nyumbani kwa muda upi baada ya kupasuka kwa tando?
    • Je, leba imeendelea kwa kiwango kipi.
  3. Je, fetasi iko hai au imekufa?
  4. Bila kuzingatia hali yake ya leba, je, mwanamke anayo maambukizi yaliyodhibitishwa au la?

17.6.1 Je, ni wakati gani ambapo unatakiwa kuendesha uzalishaji kabla ya rufaa?

Unapaswa kujibu maswali yaliyo hapo juu kwa sababu yanaonyesha ni hatua gani unazopaswa kuchukua, kama tutakavyoeleza sasa hivi.

  • Je, unaweza kueleza kwa nini la?

  • Inaongeza kwa wingi hatari za maambukizi kuingia katika uterasi.

    Mwisho wa jibu

Unapaswa kumsaidia kupitia leba kabla ya rufaa ikiwa:

Usifanye uchunguzi katika uke ya mwanamke aliye katika hali ya KTW, hata ikiwa umevaa glavu!

  • Tayari leba iliyodhibitishwa (ndio kwa Swali 1)
  • Alikueleza historia ya KTW unaotokea muda halisi wa ujauzito, baada ya wiki 37 zilizokamilika za kipindi cha ujauzito na kutokwa na kiowevu uliotokea kabla ya kuanza kwa leba (Swali 2)
  • Na huoni thibitisho lolote la maambukizi (la kwa Swali 4).

Ikiwa leba na uzalishaji ulitekelezwa kawaida na mama na mtoto wanaendelea vyema, wachunguze kwa muda wa masaa 24 yanayofuata. Eleza familia wakuite na umpeleke kwenye kituo cha afya mara moja ikiwa kunayo dalili yoyote ya maambukizi kwa mama au mtoto mchanga.

Ikiwa mwanamke atakuja kwako akiwa na hali ya KTW na yuko katika leba ambayo tayari imedhibitishwa imeendelea sana (awamu ya kwanza iliyo kamilifu, au awamu ya pili wakati mwanamke anajisikia kusukuma), hata kukiwa na thibitisho la maambukizi, au leba iliyotokea kabla ya muda, au unadhani fetasi inaweza kuwa imekufa, bado ni heri kuendeleza uzalishaji pale mwanamke alipo na umpatie rufaa kwa kituo cha afya mara tu mtoto anapozaliwa.

17.6.2 Je, ni wakati gani unapaswa kumpatia rufaa kabla ya kutekeleza uzalishaji?

Mpe mwanamke aliye katika hali ya KTW rufaa mara iwezekanavyo kwenye hospitali iliyo na kifaa cha kufanyia upasuaji ikiwa hayuko katika leba, au bado yuko katika awamu ya kwanza ya leba ya mapema na kunao muda wa kumpeleka katika kituo cha afya kabla ya leba kuendelea sana. Kumbuka kuwa ikiwa hali yake ni ya KTW uliotokea kabla ya muda, mtoto mchanga atahitaji utunzaji wa kipekee katika hospitali.

Muhtasari wa Kipindi cha 17

Katika Kipindi cha 17, ulijifunza kuwa:

  1. KTW ni kupasuka kwa tando za fetasi na kutokwa na kiowevu kutoka ukeni baada ya wiki 28 za kipindi cha ujauzito au angalau saa moja kabla ya kuanza kwa leba.
  2. KTW imeainishwa kama KTW unaotokea kabla ya muda wakati ambapo kutoka kwa kiowevu unatokea baada ya wiki 37.
  3. Wanawake walio na hali ya KTW unaoendelea kwa muda mrefu (masaa 12 au zaidi yamepita tangu kupasuka kwa tando za fetasi) wanao uwezo wa kupata maambukizi katika uterasi isipokuwa watapata matibabu ya antibiotiki ya haraka.
  4. Kipengele cha hatari kinachojulikana sana cha KTW ni pamoja na maambukizi katika mkondo wa uzazi, mlalo mbaya wa fetasi (uzazi wa kukaa au kulala vibaya kwa mtoto tumboni mwa mama), mimba ya zaidi ya watoto wawili, kiowevu kingi cha amniotiki, seviksi dhaifu, na jeraha la fumbatio.
  5. Utambuzi wa KTW unazingatia historia ya kutokwa kwa ghafula na kiowevu cha kiasi au kingi kutoka ukeni bila kuhisi uchungu. Unaweza kupata nguo za ndani zimelowa maji, kuhisi kugusika kwa sehemu za fetasi kupitia ukuta wa fumbatio lake, na kupima ukubwa wa uterasi kama ‘mdogo wa umri wa kipindi cha ujauzito’ kwa sababu fumbatio lake limepunguka.
  6. Matatizo ya kawaida yanayojulikana ya KTW ni maambukizi kwa mama na/au fetasi/mtoto mchanga, kushuka kwa kambakitovu, na ulemavu wa viungo vya fetasi.
  7. Joto jingi mwilini, mchozo ukeni ulio na harufu mbaya, ongezeko la mpwito wa ateri wa mama, ongezeko la mpigo wa moyo wa fetasi na maumivu ya sehemu ya chini ya fumbatio ni dalili ya maambukizi katika kaviti ya uterasi, ambayo yanapaswa kutibiwa haraka kwa antibiotiki.
  8. Ili kupunguza hatari za maambukizi, uchunguzi wa pelvisi kwa kutumia glavu na tarakimu unatakiwa kuepukwa kwa kina mama walio na hali ya KTW.
  9. Zalisha mtoto kisha upeane rufaa kwa hali za KTW unaotokea katika muda halisi au kabla ya muda kwa mwanamke amabaye tayari yuko katika leba inayoendelea hata ikiwa kuna uwezekano wa maambukizi au katika kesi za KTW ikiwa leba imeanza kwa kawaida na hakuna uwezekano wa maambukizi.
  10. Peana rufaa haraka iwezekanavyo kwa wanawake wote wanaokuja kwako kabla ya kuanza kwa leba au leba ya mapema, wakiwa na maambukizi yaliyodhibitishwa kwa mama au mtoto; peana rufaa kwa watoto wote wanaozaliwa kabla ya muda.
  11. Hakikisha kuwa mwanamke aliye na hali ya KTW na familia yake wanajua vyema hatari za kutotafua matibabu; washauri kuwa wakuite mara moja na waanze kuelekea katika kituo cha afya.

Maswali ya Kujitathmini ya Kipindi cha 17

Kwa kuwa umekamilisha Kipindi hiki, unaweza kutathmini jinsi ulivyotimiza malengo ya somo kwa kujibu maswali yafuatayo. Andika majibu yako katika shajara yako na uyajadili na mkufunzi wako katika somo lifuatalo la Usaidizi. Unaweza kuangalia majibu yako ukitumia muhtasari wa maswali ya Kujitathmini katika mwisho wa moduli hii.

Maswali ya Kujitathmini17.1 (yanathmini Malengo ya Somo 17.1 na 17.2)

Jaza pengo lililoachwa katika Jedwali 17.1

Jedwali 17.1
Uainishaji wa KTWUmri wa Kipindi cha uajuzito
KTW unaotokea kabla ya muda
KTW unaotokea muda halisi
Muda tangu kupasuka kwa tando
KTW ya mapema
KTW inayochukuwa muda mrefu
Answer
Jedwali 17.1
Uainishaji wa KTWUmri wa Kipindi cha uajuzito
KTW unaotokea kabla ya mudaBaada ya wiki 28 na kabla ya wiki 37
KTW unaotokea muda halisiBaada ya wiki 37, ikijumuisha baada ya muda halisi (baada ya wiki 40)
Muda tangu kupasuka kwa tando
KTW ya mapemaChini ya masaa 12
KTW inayochukuwa muda mrefuZaidi ya masaa 12

Mwisho wa jibu

Maswali ya Kujitathmini 17.2 (yanathmini Malengo ya Somo 17.1, 17.3, 17.4, na 17.5)

Je, kati ya kauli zifuatazo ni gani si kweli? Kwa kila hali, eleza ni nini ambacho si sahihi.

  • A.Maambukizi katika uterasi yanaweza kusababisha KTW na pia yanaweza kuwa tatizo linalotokana na KTW.
  • B.KTW inaweza kutokea ikiwa uterasi imepanuliwa zaidi na mlalo mbaya wa fetasi, mimba ya watoto wengi, au kuna kiowevu kingi cha amniotiki.
  • C.KTW ikishirikishwa na hali ya seviksi kutokuwa na uwezo inaweza kusababisha kushuka kwa kambakitovu.
  • D.Tando za fetasi ni dhabiti kiwango cha kuwa jeraha butu la fumbatio si rahisi kusabibisha KTW.
  • E.Upungufu na ukosefu wa hewa kwa fetasi kwa mwanamke aliye katika leba ni tatizo la kawaida la KTW unaoendelea kwa muda mrefu.
  • F.Kutokwa kwa ghafula na kiowevu cheupe majimaji kutoka ukeni kwa kawaida huonekena kwa hali za KTW.
Answer

A ni sahihi. Maambukizi katika uterasi yanaweza kusababisha KTW na pia yanaweza kuwa tatizo linalotokana na KTW.

B ni sahihi. KTW unaweza kutokea ikiwa uterasi imepanuliwa zaidi na mlalo mbaya wa fetasi, mimba ya watoto wengi au kuna kiowevu kingi cha amniotiki.

C ni sahihi. KTW ikishirikishwa na hali ya seviksi kutokuwa na uwezo inaweza kusababisha kushuka kwa kambakitovu.

D si sahihi. Jeraha butu kwa fumbatio ni sababisho la kawaida la KTW.

E si sahihi. Upungufu na ukosefu wa hewa kwa fetasi (si kwa mama aliye katika leba) ni tatizo la kawaida la KTW unaoendelea kwa muda mrefu.

F si sahihi. Hali zingine za KTW hutokea bila kutokwa kwa ghafula na kiowevu cheupe majimaji kutoka ukeni, kwa hivyo lazima uchukue hesabu ya dalili za utambuzi kama vile kupungua kwa ukubwa wa fumbatio na uguse sehemu za fetasi kwa udhairi.

Mwisho wa jibu

Soma uchunguzi maalum 17.1 kisha ujibu maswali yafuatayo.

Uchunguzi maalum 17.1 Kisa cha Zufan

Familia ya Zufan wanakujulisha kuwa maji yake yalipasuka masaa 24 yaliyopita, lakini wanawasiwasi kwa sababu leba yake bado haijaanza. Wanadhani mtoto alipaswa kuzaliwa wiki iliyopita. Unapomgusa ana joto na kukosa utulivu na analalamika kuwa anahisi maumivu katika sehemu ya chini ya fumbatio lake.

Maswali ya Kujitathmini 17.3 (yanathmini Malengo ya Somo 17.1, 17.2, 17.5 na 17.6

  • a.Je, utaainisha vipi hali ya Zufan ya KTW?
  • b.Je, anazo dalili za matatizo yoyote?
  • c.Je, kunalo jambo lolote ungelifanya ili kuzuia hali yake isi zidi?
  • d.Je, ni hatua gani ya haraka unayopaswa kuchukua?
Answer
  • a.Hali ya Zufan inafaa kuainishwa kama KTW unaoendelea kwa muda baada ya kutokea, kwa sababu umri wa kipindi cha ujauzito tayari imepita wiki 40 na tando zake zilipasuka zaidi ya masaa 12 yaliyopita.
  • b.Anazo dalili mbili zilizodhihirika za maambukizi ya fumbatio: joto jingi mwilini na maumivu katika sehemu ya chini ya fumbatio.
  • c.Ungelizuia hali yake kuwa isi zidi ikiwa ulikuwa umemshauri Zufan na familia yake kwa udhairi zaidi kuhusu hatari za kutotafuta matibabu baada ya kupasuka kwaTando.
  • d.Unapaswa kumpa rufaa haraka kwenye hospitali iliyoko karibu au kituo cha afya kilicho na vifaa vya kufanyia upasuaji; pia atahitaji antibiotiki haraka za kutibu maambukizi.

Mwisho wa jibu