Kuvuja damu baada ya wiki 28 za ujauzito hukisiwa kuwa kuvuja damu katika awamu za mwisho wa ujauzito. Ulijifunza kuhusu kuvuja damu katika awamu za mwanzo kabla ya wiki 28 za ujauzito katika Kipindi cha 20. Kuvuja damu katika awamu za mwisho za ujauzito pia hujulikana na madaktari na wakunga kama kuvuja damu kabla ya kuzaa. Hali hii ni kisababishi kikuu cha vifo vya kina mama na fetasi, hivyo huhitaji usaidizi wa mtaalamu wa huduma ya afya haraka iwezekanavyo ili kuokoa maisha ya mwanamke na mtoto wake ambaye bado hajazaliwa.
Wewe kama mhudumu wa afya wa kwanza kufikiwa na wanawake wajawazito katika jamii yako, unapaswa kushirikiana nao katika maandalizi ya kuzaa na kufanya mpango unaoshugulikia matatizo yoyote katika ujauzito, kama vile kuvuja damu kwa wingi. Unapaswa kutoa huduma ya kwanza ya kiukunga kisha uhakikishe kuwa mwanamke anayevuja damu katika awamu za mwisho wa ujauzito amefikishwa kituoni cha afya ili apate huduma ya dharura. Hospitali ya Wilaya au Kituo cha Afya chenye uwezo wa kufanya upasuaji wa kiukunga kinaweza kuokoa maisha yake.
Baada ya kukikamilisha kipindi hiki unatarajiwa:
21.1 Kufasili na kutumia kwa usahihi maneno yote muhimu yaliyoandikwa kwa herufi nzito. (Maswali ya Kujitathmini 21.2 na 21.3)
21.2 Kufasili kuhusu dalili za hatari na visababishi vya mara nyingi vya kuvuja damu katika awamu za mwisho za ujauzito. (Maswali ya kujitathmini 21.1, 21.2 na 21.3)
21.3 Kutoa huduma ya kwanza ya ukunga na kutambua wakati wa kupendekeza rufaa kwa mwanamke anayevuja damu katika awamu za mwisho za ujauzito. (Maswali ya Kujitathmini 21.1 na 21.2)
Kuvuja damu katika awamu za mwisho za ujauzito au kuvuja damu kabla ya kuzaa mara nyingi husababishwa na kuvuja damu kutoka kwa plasenta, ingawa kuna visababishi vingine vichache vinavyotokea katika uterasi au sehemu zingine za mfumo wa uzazi. Kwanza, tutaorodhesha visababishi hivi kwa ufupi, kisha kufasili kwa kina kuhusu plasenta kujitenga kutoka pembezoni mwa uterasi, privia ya plasenta na kupasuka kwa uterasi, kwa sababu hizi ni hali zinazohitaji huduma ya dharura ili kuokoa maisha.
Kutengeka kwa plasenta: humaanisha kutengeka kwa kipande cha plasenta au plasenta yote iliyojibandika kwenye sehemu ya thuluthi mbili za juu ya uterasi kabla ya wakati. Kwa kawaida, plasenta hutengana na uterasi baada ya kutolewa kwa fetasi, katika awamu ya tatu ya leba (Utajifunza kuhusu haya yote katika Moduli ya Utunzaji wa Leba na Kuzaa). Mama na mtoto wanaweza kufa ikiwa sehemu ambapo plasenta ilitengana na pembezoni mwa uterasi itaanza kuvuja damu.
Ni kwa nini kuna uwezekano wa kuvuja damu sana ikiwa plasenta itatengana na pembezoni mwa uterasi kabla ya wakati? Ni kwa nini tukio hili huhatarisha maisha ya mama na fetasi? (Rejelea uliyoyasoma kuhusu muundo wa plasenta katika Kipindi cha 5 au uutazame tena Mchoro 5.5 katika Utunzaji kabla ya Kuzaa, Sehemu ya 1.)
Damu ya mama hutiririka hadi kwenye nafasi kubwa katika plasenta; sehemu zinazopakana na mishipa ya damu ya fetasi (Mchoro 5.5). Ikiwa plasenta itatengeka kutoka pembezoni mwa uterasi, damu ya mama itatiririkia kwenye uwazi wa uterasi, hivyo anaweza kufa kufuatia kupoteza damu nyingi. Kiwango cha virutubishi na oksijeni kinachoifikia fetasi kutoka katika damu ya mama kitapunguka, hivyo fetasi inaweza kufa au ubongo wake kuharibika.
Mwisho wa jibu
Damu nyingi inayovuja kwenye sehemu ambapo plasenta imetengana na pembezoni mwa uterasi inaweza kupitia seviksi kisha kutiririkia ukeni. Damu hii kwa kawaida huwa na uweusi kwa kukosa oksijeni ya kutosha. Hii ni dalili kuu ya hatari.
Hata hivyo, katika baadhi ya matukio, damu yote kutoka katika sehemu ambapo plasenta imejitenga inaweza kusalia ndani ya uterasi, kisha kuanza kujaa (Mchoro 21.1) Damu haitaonekana ikitokea ukeni kwa sababu kiasi kidogo sana cha damu hupenyeza na kutokea ukeni. Hata hivyo, mwanamke ataonyesha ishara za kuvuja damu ndani ya uterasi, ziitwazo mshtuko unaohusiana na kuvuja damu. Tulijadili hali hii kwa muhtasari katika Kipindi cha 20 kuhusu kuvuja damu katika nyakati za mwanzo za ujauzito. Tutarudia habari inayofuata hapa (Kitengo 21.2.1) kwa sababu kuna hatari zaidi ya mshtuko huu kutokea ikiwa mwanamke atavuja damu katika awamu za mwisho za ujauzito.
Dalili zingine za kutengeka kwa plasenta ni pamoja na:
Hali zote zinazotokea kufuatia kutengeka kwa plasenta zinakuhitaji uchukue hatua ya dharura: tazama Kitengo 21.5.
Tukio la kutengeka kwa plasenta linaloambatana na kuvuja damu nje au ndani ya uterasi linaweza kusababisha mshtuko unaohusiana na kuvuja damu, ambapo damu huvuja kwa kiasi kikubwa hivi kwamba damu inayosalia katika mishipa ya mwanamke haitoshi kufikisha virutubishi na oksijeni inayohitajika kwenye seli zake.
Dalili za mshtuko unaohusiana na kuvuja damu ni zipi? (Rejelea Kisanduku cha 20.3 katika kipindi cha awali)
Mwanamke mwenye mshtuko ataparara na kulowa jasho huku akiwa na mrindimo hafifu lakini wa kasi (zaidi ya midundo 100 kwa dakika), kupumua kwa haraka, shinikizo la chini la damu au linaloshuka (shinikizo la kidiastoli — kiwango cha chini — halizidi 60 mmHg na wakati mwingine ni la chini sana); anasema ana kizunguzungu; anaonekana kuchanganyikiwa na hata kupoteza fahamu.
Mwisho wa jibu
Unapaswa kutambua dalili kama vile kuparara: kucha, viganja vya mikono na sehemu ya ndani ya kigubiko cha macho huendelea kuwa nyeupe pindi anavyoendelea kupoteza damu. Mwanamke huyu anaweza kukwambia kuwa anachoka au kushindwa kuinua kichwa chake. Yeye pia huonekana kutotulia, pengine anaomba kunywa maji, na anaonekana kuchanganyikiwa. Kuchanganyikiwa hutokea kwa sababu ubongo haupati oksijeni ya kutosha. Madhara ya mshtuko yanayotokea mara nyingi kufuatia kuvuja damu ni pamoja na figo au moyo kushindwa kufanya kazi.
Kufuatia mshtuko huu na kupungua kwa kiwango cha damu inayotiririkia kwenye figo, figo zinaweza kushindwa kufanya kazi. Hivyo basi, mwanamke hutoa kiasi kidogo sana cha mkojo, hivyo taka ambalo lingeondolewa na figo kutoka kwenye damu kisha kuondolewa mwilini kwa mkojo husalia kwenye damu. Kulimbikazana kwa taka katika damu humfanya mwanamke kudhoofika kwa haraka, na kifo hufuata iwapo hali hii haitakabiliwa. Hali hii huitwa hali kali ya kushindwa kwa figo ('kali' humaanisha kuwa hali hii huwa hatari kwa maisha kwa ghafla).
Mwanamke akivuja damu, moyo wake hupiga kwa kasi ukijaribu kufikisha damu ya kutosha kwenye sehemu muhimu za mwili, kama vile ubongo. Ikiwa amevuja damu nyingi, moyo wake hautaweza kupiga kwa kasi ifaavyo hadi kutosheleza kiwango cha damu kinachopotea, hivyo atakumbwa na hali ya kushindwa kwa moyo. Hii ni hali ambapo moyo hushindwa kufikisha damu ya kutosha kwenye tishu, hivyo kifo kinaweza kutokea.
Kisababishi kingine cha kuvuja damu katika awamu za mwisho za ujauzito ni privia ya plasenta. Katika hali hii, plasenta huwa imejibandika karibu sana na seviksi, au hata kuifunika (Mchoro 21.2). Seviksi inapoendelea kupanuka, ncha ya plasenta inaweza kutengeka na kuanza kuvuja damu. Mwanamke mwenye hali hii kwa kawaida huwa na damu yenye rangi ng'avu nyekundu inayovujia ukeni. Kiwango cha damu inayovuja kinaweza kuwa cha chini ikilinganishwa na ile inayovuja kufuatia kutengeka kwa plasenta, lakini katika baadhi ya matukio, hali hii inaweza kuwa kali na hatari kwa maisha. Kuvuja damu mara nyingi huwa hakuandamani na uchungu, hivyo mwanamke anaweza kutotambua kwa muda mrefu, kwa mfano, usiku akilala. Kuvuja damu kunaweza kuanzishwa na ngono na kunaweza kurejea kila mara (kukikoma kisha kuanza tena).
Katika mwanamke aliyevuja damu katika awamu za mwisho za ujauzito kufuatia privia ya plasenta, uterasi mara nyingi huwa laini kwa kumpapasa fumbatio. Hali hii ni kinyume na uterasi iliyo gumu wakati kuvuja damu kumesababishwa na kutengeka kwa plasenta.
Kwa kijumla, kichwa cha fetasi hakiko katika sehemu ya chini ya uterasi, ambayo utahisi ikiwa tupu. Hali hii ya mtoto kutanguliza vibaya inaweza kuwa dalili ya privia ya plasenta. Kwa kawaida, hali ya fetasi ni ya kawaida, hivyo unaweza kuhisi mpigo wa moyo wa fetasi ukisikiliza kwa fitoskopu. Mama pia huhisi fetasi ikicheza kama kawaida — lakini hali hii huwa tofauti wakati mwingine.
Utambuzi wa privia ya plasenta unaweza tu kuthibitishwa kwa kumchunguza mama kwa mtambo wa pichatiba unaoweza kuonyesha hali ya plasenta, au kwa kuchunguza uke katika chumba cha upasuaji. Kwa hivyo, unapaswa kumpendekezea rufaa hadi kituo cha afya kilicho na vifaa vinavyohitajika kufanyia utambuzi.
Wanawake wanaoshukiwa kuwa na privia ya plasenta wanapaswa kuhamishwa hadi katika Hospitali ya Wilaya au Kituo cha Afya chenye mtambo wa pichatiba au chumba cha upasuaji.
Usimchunguze uke wewe mwenyewe iwapo mwanamke anavuja damu katika awamu za mwisho za ujauzito. Hatua hii huzidisha hali hii na kuongeza hatari kwake na fetasi.
Kuvuja damu kufuatia kupasuka uterasi kunaweza kutokea kupitia ukeni, hivyo unaweza kuona damu ikitiririka nje, au uterasi inaweza kuvujia damu ndani ya fumbatio ambapo haitaweza kuonekana. Ikiwa mwanamke mwenye leba iliyodumu kwa muda mrefu ataanza kuhisi maumivu katika fumbatio, (mauvimu yanayoendelea na kuzidishwa na mwendo wowote), au uterasi ikikoma kukazana katika jaribio la kumsukuma mtoto, au damu kuanza kuvuja ukeni ikiandamana na mshtuko, kuna uwezekano kuwa uterasi imepasuka. Ikiwa uterasi itakoma kukazana, fumbatio litakuwa laini na utaweza kuzihisi sehemu za mwili wa mtoto kwa urahisi kwa kulichunguza fumbatio. Ikiwa mtoto amekufa, hutaweza kusikia mpigo wa moyo wake hata kwa fitoskopu.
Utajifunza kwa kina kuhusu hali ya kupasuka uterasi katika Moduli inayofuata katika mtaala huu, kuhusu Utunzaji katika Leba na Kuzaa. Unapomhudumia mwanamke mwenye dalili za kupasuka uterasi, unafaa kuchukua hatua za dharura kama inavyoelezwa hapa chini.
Ukitambua kwamba mwanamke anavuja damu na unashuku kuwa ana plasenta iliyotengeka, privia ya plasenta, uterasi iliyopasuka, au kuvuja damu kufuatia visababishi vingine, chukua hatua hizi:
Kumbuka kuwa damu inayovuja mwanzoni inaweza kuwa nyingi sana na hatari kwa maisha, hivyo mwanamke anaweza kufika katika Kituo cha Afya akibebwa na jamaa zake. Katika hali hiyo, baada ya kufanya uchunguzi wa haraka wa hali ya mgonjwa, andaa mrija wa kudungia dawa mishipani, andaa usafiri kisha umpe rufaa haraka iwezekanavyo hadi katika kituo cha afya kilicho karibu.
Ni hali gani salama zaidi ya kumsafirisha mwanamke? (Rejelea Mchoro 20.3 katika kipindi cha awali)
Mwanamke anapaswa kukilaza kichwa chake bapa — usiweke mto chini ya kichwa chake. Mwinue magoti na umwegemeze miguuni kwa kutumia mto au blanketi iliyokunjwa, ili miguu iinuke zaidi ya kichwa chake.
Mwanamke anapaswa kupendekezewa rufaa kila mara na ni muhimu azalie katika kituo cha hali ya juu zaidi iwapo atavuja damu katika awamu za mwisho za ujauzito, hata ikiwa damu itasita kuvuja bila usaidizi wowote kabla ya leba kuanza.
Mwisho wa jibu
Kwa kawaida, unapaswa kuandamana na mwakamke huyu ili kudhibiti viowevu alivyotiwa na uhakikishe kuwa umeshikilia kifuko cha kiowevu juu yake. Iwapo hutaweza kwenda naye, mweleze mtu atakayeandamana naye umuhimu wa kudumisha hali ya mwanamke na kifuko katika namna iliyoelezwa; pia mweleze mtu huyu jinsi ya kufunga sindano ya kutia viowevu mishipani wakati viowevu vilivyo katika kifuko vitamalizika. Kumbuka kumpa mwanamke huyu barua ya rufaa.
Katika kipindi cha mwisho cha Moduli hii, tunakufunza kwa nadharia jinsi ya kutayarisha viowevu vinavyotiliwa mishipani, na jinsi ya kuingiza katheta ya mkojo kwa mwanamke asiyeweza kukojoa kwa sababu ya matatizo ya ujauzito au leba.
Katika kipindi cha 21, umejifunza kwamba:
Kwa sababu umekamilisha somo hili, unaweza kutathmini ulivyofanikisha Malengo yake kwa kujibu maswali yafuatayo. Andika majibu yako katika shajara kisha ujadiliane na Mkufunzi wako katika mkutano utakaofuata wa Somo saidizi. Unaweza kulinganisha majibu yako na vidokezo kuhusu Maswali ya Kujitathmini yaliyo mwishoni mwa moduli hii.
Jamaa wa mwanamke mmoja wamekuita kumhudumia mwanamke anayevujia damu ukeni katika miezi 8 ya ujauzito.
Mwisho wa jibu
Ni maelezo yapi yafuatayo yasiyo ya kweli? Katika kila kauli, eleza lisilo la kweli.
A si kweli. Haupaswi kamwe kumchunguza uke wa mwanamke anayevuja damu katika awamu za mwisho wa ujauzito.
B si kweli. B Kutengeka kwa plasenta kutoka mahali pake pa kawaida kabla ya wakati kunaweza kusababisha damu kuvujia nje, lakini pia kunaweza kusababisha damu kuvujia ndani.
C ni kweli. Privia ya plasenta hutokea wakati plasenta imejibandika katika sehemu inayokaribia seviksi au kuifunika.
D sio kweli. D Unapaswa kila wakati kumpendekezea rufaa mwanamke anayevuja damu kwa muda mrefu katika awamu za mwisho za ujauzito hata ikiwa damu itakoma kuvuja bila usaidizi wowote.
Mwisho wa jibu
Soma Kauli ya Somo 21.1 kisha ujibu maswali yanayofuata.
Bi X ameletwa katika Kituo chako cha Afya akiwa amebebwa na jamaa zake huku amelazwa kwenye kitanda cha mbao cha kujitengenezea nyumbani. Unafahamishwa kuwa ana ujauzito wa miezi 9. Alianza kwa kuumwa na fumbatio kisha kuvuja damu ukeni. Unapomchunguza, unatambua kuwa nguo zake zimelowa damu. Ana wasi wasi na kiu. Mapigo yake ya moyo ni midundo 120 kwa dakika, na shinikizo la damu ni 80/50 mmHg.
Mwisho wa jibu