Nyenzo-rejea ya 1: Masuala ya kijinsia

Taarifa za msingi / welewa wa somo wa mwalimu

Jinsia inaeleza zile tabia za wanaume na wanawake ambazo zinatokana na shinikizo la kijamii na wala hazitokani na sababu za kimaumbile.

Hisia zilizooneshwa na wanafunzi wengi zilitokana na jinsi walivyolelewa kijamii, hali ambayo husababisha wawe na mtazamo pogofu wa kijinsia bila kujijua.

Kwa ujumla, katika familia wanaume huchukuliwa kama vichwa,na ufanyikaji wa maamuzi, kwa kiasi kikubwa, umetawaliwa na wanaume.

Kuna hali ya kutofautiana kabisa kijinsia katika upatikanaji wa elimu, fursa za kiuchumi na huduma za afya.

Kuna upendeleo wa kutoa elimu kwa wavulana, pamoja na masuala ya mimba za utotoni, matokeo yake ni kiwango kikubwa cha kuachishwa shule kwa wasichana.

Kuna hali ya kutolingana katika ajira kwa sekta na jinsia. Katika sekta ya kilimo, wanawake ndio wazalishaji wakuu wa mazao ya chakula.

Watu wanazaliwa kama wanawake au wanaume, lakini wanajifunza kuwa wasichana au wavulana ambao hukua na kuwa wanawake au wanaume.

Watu wanafundishwa tabia na mitazamo inayofaa, majukumu na shughuli zinazowastahili, na jinsi wanavyotakiwa kuhusiana na watu wengine. Tabia hii ya kujifunza ndiyo inayojenga utambulisho wa kijinsia na inayoamua kuhusu majukumu ya kijinsia.

Mambo ya kuzingatia katika ufundishaji wa jinsia

Masuala ya kijinsia ni nyeti hivyo kanuni lazima zidhibitiwe kwa msisitizo ili kuhakikisha kwamba mjadala haugeuki kuwa ugomvi kati ya wasichana na wavulana.

Unahitaji kusaidia jinsia zote kutambua vema mitanziko na nafasi za kuchagua walizonazo jinsia nyingine.

Ni muhimu kwa wanafunzi kuelewa jinsi mitazamo pogofu kuhusu jinsia inavyoshadidiwa na tabia za familia, shuleni na katika jamii.

Unatakiwa kuwasaidia wanafunzi wako kuunda mikakati na mbinu za kukabiliana na hali zisizosawa za kijinsia.

Nyenzo-rejea ya 2: Jinsia – unafikiri nini?