Somo la 2

Nidhamu ni muhimu kwa kila darasa. Hata hivyo, mada ya VVU na UKIMWI inaweza kuwafanya wanafunzi wakaipokea tofauti na jinsi wanavyokuwa katika masomo mengine. Katika Moduli 1, Sehemu ya 4 uliunda kanuni za darasa. Unaweza kukuta kuwa unatakiwa kupanua kanuni hizo ili kuruhusu majadiliano ya wazi kuhusu VVU na UKIMWI pamoja na tendo la kujamiiana. Kujadiliana na darasa lako sababu za kuhitaji kanuni maalumu na kuwaambia wanafunzi wapendekeze hizo kanuni wao wenyewe inaweza kuwa ni mwongozo wa kukusaidia katika mada yako.

Nyenzo-rejea 2: Hali ya darasa inakupa miongozo ya jinsi ya kuhakikisha kuwa darasa linakuwa na mazingira yanayowaruhusu wanafunzi wako kuweza kutalii mada ya VVU/UKIMWI.

Uchunguzi kifani ya 2: Kushughulika na wanafunzi watundu/wakorofi darasani

Twambo alikuwa amechoka sana - siku ilikuwa imeshakuwa ngumu. Yeye ni mwalimu mwanafunzi wa mazoezi ya ualimu katika shule ya msingi Bulongwa na mkaguzi wake alimwambia afundishe baadhi ya masomo juu ya VVU na UKIMWI kwa darasa la Nne, Tano na Sita. Alikuwa hajiamini sana.

Walikuwa wameshapewa vipindi vichache vya VVU/UKIMWI chuoni (angalia Nyenzo-rejea 2), ambayo ilimsaidia Twambo kujiandaa. Alikuwa anajiamini kuhusu kufanya kazi na wanafunzi wadogo, lakini alikuwa na tatizo kubwa na darasa la sita. Katika darasa hili kuna wavulana wengi wakubwa na Twambo alikuwa na uhakika kuwa wangeingilia kati masomo hayo.

Twambo alikuwa sahihi; kwani alikuwa tu ndiyo ameanza somo la kwanza wakati Thomas alipoanza kumwuliza maswali kuhusiana na maisha yake mwenyewe ya kimapenzi. Kwanza Twambo alishtuka, lakini akawahi kwa kumwambia Thomas kuwa asiwe mbinafsi na akaendelea na somo. Baadaye, kwenye kazi ya kikundi darasa lilikuwa na vurugu na makelele yaliyoambatana na kicheko na yule mshauri/mkaguzi wake akawa amekuja kuangalia kelele hizo zilikuwa zinahusu nini.

Twambo alikivunja kile kikundi cha wavulana wenye kelele, lakini wakati walipokuwa wanatoa maelezo Thomas na rafiki zake waliendelea bado kuelezea kwa uwazi mambo ya ngono hata kuwachekesha wanafunzi darasani na kumfanya Twambo atahayari. Twambo aliwakumbusha wanafunzi kanuni za darasa na alisema kuwa walikuwa kwenye hatari ya kutoshiriki kama wakikosa nidhamu. Aliweza kwenda nao vizuri kwa kutotilia maanani hoja zao nyingi au kwa kubadilisha hoja zao ili kueleza pointi ya ukweli. Lakini hali ilikuwa imeshachosha sana na kengele ya

kwenda nyumbani ilipogongwa Twambo alifurahi. Kipindi kingine kabla ya kuanza somo aliongea na wavulana hawa kuhusu heshima na kile ambacho angekifanya kama wangekosa adabu. Twambo alijaribu kuwasaidia wanafunzi kuelewa umuhimu wa mada.

Shughuli ya 2: Kujenga mazingira yanayoruhusu kujifunza

Kwanza soma Nyenzo-rejea 2

Kuwaandaa wanafunzi wako na pia kujiandaa wewe mwenyewe ni sehemu ya maandalizi yako ya kufundisha darasa lako kuhusu VVU na UKIMWI. Hapo awali ulijifunza kuhusu kuunda kanuni za darasa za kusaidia ujifunzaji kwa ufanisi kwenye mada ambazo ni nyeti. Sasa unahitaji kufanya mambo yafuatayo na darasa lako.

Eleza darasani kwamba mtafanya kazi chache juu ya VVU na UKIMWI.

Durusu kanuni za darasa mlizonazo kwa kuligawa darasa kwenye vikundi ili kujadili kama kanuni hizi zinafaa.

Kiambie kila kikundi kifikirie kanuni za ziada zisizozidi tatu ambazo wanakikundi wangependa ziwepo wakati wa kufanya kazi hii. 

Kila kikundi kipendekeze kanuni zake za nyongeza , na kuziandika ubaoni.

Kama darasa, kubalianeni juu ya kanuni za nyongeza mnazozitaka.

Jadili kanuni zote na darasa, zikiwemo zile kanuni mpya, na hakikisha kuwa kila mmoja anaelewa vizuri sababu za kanuni hizi kuhitajika kwenye mada hii.

Utafanya nini iwapo watazipuuzia kanuni hizi? Kubalianeni na darasa lako kuhusu mipaka au vizuizi gani utakavyotumia.