Somo la 2

Moja kati ya ugeuzi wa kawaida ni uhamishaji sambamba. Kuhamisha umbo, kinachofanyika ni kuondoa mahali pake kutoka kwenye ukurasa, juu au chini, kushoto au kulia, lakini usibadilishe umbo kwa namna yoyote ile (angalia Nyenzo-rejea 3: Uhamisho Sambamba ).

Kwa kuwa kuhamisha umbo ni kazi rahisi, hata wanafunzi wadogo sana wanaweza kuelewa dhana hii, hususan kama watakuwa na maumbo halisi ya kufanyia kazi.Kwa wanafunzi wakubwa, shughuli hii inaweza kufanywa kuwa changamoto zaidi kwa kutumia viwianishaji vya x-y na ukokotoaji, kuliko kufanyia kazi maumbo halisi.

Uchunguzi-kifani na Shughuli ya 2 vinashughulikia uhamishaji sambamba na jinsi ya kutofautisha kazi kulingana na umri na kiwango.

Uchunguzi kifani ya 2: Kupanua welewa wa uhamishaji sambamba

Bibi Kiboa anafundisha darasa changamani ambamo ana kundi la watoto wakubwa wanaofanya vizuri katika hisabati. Alipoona kazi wanayoifanya sasa haiwashughulishi kiasi cha kutosha, Bibi Kiboa aliamua kuwapa fursa ya kuwafanya wafurahie changamoto halisi. (Kwa taarifa zaidi kuhusu ufundishaji wa madarasa changamani, angalia Nyenzo-rejea Muhimu: Kufanya kazi katika madarasa makubwa au/changamani.) Bibi Kiboa tayari ameshatambulisha viwianishaji vya x-y kwa darasa zima. Siku moja wakati sehemu kubwa ya darasa ilikuwa inashughulikia uhamishaji sambamba wa pembetatu kwa kutumia maumbo yaliyokatwa, Bibi Kiboa aliwapa wanafunzi wake wane msaada zaidi (angalia Nyenzo-rejea 4: Uhamishaji na uakisi wa pembetatu ).

Ili kuchora pembetatu na kuzitambulisha kwa mihimili ya x-y kwenye karatasi yenye fito miraba, Bibi Kiboa aliwauliza wanafunzi viwianishi vya kona tatu (vipeo) ni nini –walijibu kwa wepesi, na waliandika majibu yao. Kisha aliwauliza, ‘Kitatokea nini kama nikihamisha umbo hilo nafasi sita upande wa kulia? Viwianishi x-y vitakuwaje?’ Bibi Kiboa aliendelea kwa mtindo huu mpaka alipojiridhisha kwamba wanafunzi wameelewa vizuri kilichokuwa kikitokea.

Halafu, aliwaambia, ‘Sasa, kila mmoja ampe mwenzake swali –toa viwianishi vya pembetatu, na uhamishaji utakaotumika kwa pembetatu. Andika swali hili, kasha chora pembetatu unayoiandaa, kokotoa viwianishi vilivyohamishwa, na chora mwonekano mpya. Ukifanya hivi kwa usahihi, hapo unaweza kujaribu maumbo mengine zaidi ya pembetatu ya kufanyiana majaribio.’

Wanafunzi walifurahia uzingativu wa mwalimu wao, pamoja na fursa ya kufanya kazi kwa uhuru zaidi na kupeana changamoto za kihisabati.

Shughuli ya 2: Kuchunguza uhamishaji kwa vitendo

Hakikisha kwamba wanafunzi wanafahamu jinsi ya kutengeneza viwianishi vya x-y, kwa njia ya ufundishaji wa darasa zima. Ili kutofautisha kazi kwa ajili ya wanafunzi wakubwa, tazama maangalizo kuhusu upambanuzi katika Nyenzo-rejea 4 .

Waambie wanafunzi wachore na kukata pembetatu, mraba na mstatili kutoka kwenye karatasi ya mraba: Sisitiza kwamba kila kona (au kipeo) cha maumbo yao lazima kiwe kwenye ‘misalaba’ kwenye karatasi zao za fito mraba kwa kuchora mfano ubaoni. Kusiwe na upande wenye zaidi ya urefu wa miraba 10.

Kwenye upande wa pili wa karatasi ya fito mraba, waambie wanafunzi wachore na kutia alama za mihimili ya x-y axes yenye urefu wa angalau miraba 20 (angalia Nyenzo-rejea 4 ). Ili kuweka mojawapo kati ya maumbo yaliyokatwa kwenye karatasi kwa kusudi la kuzifanya kona zake ziwe kwenye ‘misalaba’ ya fito mraba, lazima waoneshe vipeo (a, b, c na d kama inavyostahili), kisha wachore umbo hilo na kuandika viwianishi vya kila kipeo.

Waambie wahamishe umbo lao kwenda nafasi nyingine (huku wakiliweka kwa upande huo huo juu) na warudie mchakato huu.

Waulize wanafunzi wako: ‘Kinatokea nini kwa viwianishi vya x katikati ya nafasi mbili? Je, inatokea hivyo hivyo kwa kila kiwianishi? Kitu gani kinatokea kwa upande wa viwianishi vya y?’

Sehemu gani ya shughuli hii ilileta ugumu kwa wanafunzi wako? Utawasaidiaje wakati mwingine?