Somo la 2

Hadithi zote husimuliwa kwa kuzingatia msimamo fulani. Maoni yetu kama waandishi na wasomaji yanaweza kuathiriwa na hali mbalimbali; maoni haya hutegemea kama ni sisi vijana au wazee, wanaume ama wanawake, ni wanachama wa chama fulani cha siasa, ni waumini wa dini Fulani, tunafurahia shughuli fulani, tuna afya njema au afya mbovu, tunafanya kazi au hatufanyi kazi, n.k. Ni muhimu wanafunzi wakajifunza kuwa hadithi zinaweza kuhadithiwa kwa njia mbalimbali kwa kuhusishwa na msimamo fulani au kutohusishwa nao. Ni kweli pia kuwa katika maisha halisi kuwa kuna njia zaidi ya moja ya kulitazama suala fulani na njia mbalimbali za kutatua tatizo.

Unaweza kuwasaidia wanafunzi wakajifunza hili kwa kuwapa nafasi ya kusimulia hadithi ileile au hadithi inayofanana kutokana na mitizamo tofautitofauti au kwa kubadilisha hadithi.

Uchunguzi kifani ya 2: Kumbadilisha ‘mhusika wa nje’ kuwa mhusika mkuu katika hadithi.

Mwanafunzi mmojawapo aitwaye James katika darasa la 6 la Mwalimu Fortunate Mabuso, ameumia sana kutokana na ajali ya gari na angeweza kutembea kwa magongo. Siku moja, alimwambia mwalimu Mabuso kuwa alijisikia vibaya kwa kuwa hadithi zote kuhusu wavulana zilieleza namna walivyofurahia shughuli ambazo hawezi kuzifanya. Mwalimu Mabuso alighadhabika kwa kuwa hakuwahi kulifikiria jambo hili. Alimuuliza alikuwa akifanya nini wakati akiwa nyumbani na akagundua kuwa alikuwa mwanamuziki hodari ambaye alijua kupiga ngoma na filimbi ya chuma. Alimuuliza anaweza kucheza kwa kutumia filimbi hiyo darasani. Kwanza alikuwa na aibu kuhusu jambo hili lakini mwisho akakubali kuwa anaweza.

Katika somo lake lilifuata la Kiingereza, Mwalimu Mabuso aliwaambia kuwa anataka kuwapa mawazo ya kuandika hadithi. Alimwomba James kuwachezea ngoma. Wanafunzi walishangaa na kufurahia uhodari wa James.

Mwalimu Mabuso aliwataka wafikirie hadithi ambapo James, mwanamuziki, alikuwa mhusika mkuu. Darasa zima lilibadilishana mawazo halafu wakafanya kazi wawiliwawili na kuanza kuandika hadithi na/au kuchora

Wakati wa somo, baadhi ya wanafunzi walikwenda kwa James na mwenzake kuomba ushauri wa mambo zaidi ya kuandika hadithi yao. Katika somo lililofuata, wanafunzi katika vikundi vya wawiliwawili, waliendelea na majadiliano yao na kuandika na kuchora hadithi zao binafsi.

Wakati mwalimu Mabuso alipokuwa akisoma hadithi, aligundua kuwa kulikuwa na wanafunzi wengine darasani ambao labda nao walijisikia ‘kutengwa’ katika hadithi katika vitabu vya kiada na vitabu vya hadithi vya darasa. Alianza kupanga njia za kuwashirikisha wanafunzi hawa pia.

Shughuli ya 2: Kuandika hadithi kwa kuzingatia mitazamo tofauti

Tumia hadithi ileile kwa shughuli ya 1 au nyingine uliyochagua.

Isome na wanafunzi na jadili jinsi ambavyo ingesimuliwa tofauti. Kwa mfano, wahusika wapya wangeongezwa au wahusika waliopo wangeshiriki kwa uhusika tofauti. Katika ya familia, baba angebaki nyumbani na kupika wakati ambapo mama angekuwa akifanya kazi katika gereji. Familia ingekuwa na mtoto au mtu mzima ambaye ana ulemavu au upungufu wa akili. Watake wanafunzi wafanye kazi katika vikundi vidogo kuandika na/au kuchora kwa namna mbalimbali za hadithi mliyosoma. Zungukia darasa, ukizingatia mambo yapi yanawafurahisha wanafunzi. Kama kuna kikundi chenye matatizo, kisaidie.

Vikundi vikisha maliza, mtake mwanafunzi mmoja kutoka katika kila kikundi kusoma hadithi hiyo mpya darasani na kuonesha picha. Kusanya hadithi hizo kwa ajili ya kuzitathmini. Unaweza kuzichapisha hadithi hizo katika kitabu kwa ajili ya maktaba ya darasa au ziweke kwenye maonesho darasani. Hadithi zinakuonesha nini kuhusu mawazo ya wanafunzi na hatua yao ya maendeleo ya kuandika.