Somo la 1

Wanafunzi wako huja shuleni wakiwa tayari na usuli tajiri wa mitagusano ya kibinadamu na tajiriba za ulimwengu. Wanayo pia lugha ya kuelezea ulimwengu wao. Wanapotumia lugha yao ya nyumbani wanaweza kutumia tajiriba yao kusheheneza uneni na uandishi wao kwa maelezo makini na jazanda. Ukiwa mwalimu, unahitaji kuwahimiza wafanye hivi, na kuwafanya watumie maarifa waliyo nayo.

Kuhusu kusema au kuandika katika lugha ya ziada, wanafunzi mara nyingi hawatang’amua kuwa wanaweza kutumia maarifa hayo. Walimu, pia, wanaweza kusahau kwamba kazi yao ni kuwasaidia wanafunzi wahamishe maarifa yao katika/kwa lugha yao ya nyumbani ili yawe katika lugha ya ziada, na sio kuanza na bure.

Katika kisehemu hiki, tunapendekeza kuwa uwasaidie wanafunzi kueleza wanayofahamu na kubuni/kufikiria kwa lugha yao wenyewe, na kisha kufikiria njia za kuhamishia maana hiyo kwenye lugha ya ziada.

Uchunguzi kifani ya 1: Kuandika katika isiZulu kutajirisha Kiingereza

Bi Nonhlanhla Dlamini anafundisha Kiingereza kwa wanafunzi 64 wa darasa la 6 wanaosema isiZulu katika wilaya ya Nongoma katika KwaZulu-Natal, Afrika ya Kusini.

Siku moja, alisoma na kujadili mifano ya mashairi ya sifa na hadithi na wanafunzi wake na kupendekeza kuwa nao waandike yao. Walifurahi sana, lakini jitihadi zao katika Kiingereza hazikuridhisha; kwa hiyo aliamua kuchukua mkabala tofauti.

Bi. Dlamini aliwataka wanafunzi wake kufanya kazi wawiliwawili waelezane kitu wanachotaka kukiandika na kusaidiana waandike hadithi na shairi kwa isiZulu.Kisha wakafanya kazi wawiliwawili kuandika nakala za Kiingereza.

Aliwakumbusha wasifanye tafsiri za neno kwa neon kwa sababu sarufi na msamiati wa lugha mbili hizi vimejengwa kwa namna tofauti.

Jitihadi zilizofuata katika uandishi katika Kiingereza zilivutia zaidi, ingawa hazikusheheni maelezo yenye undani na mvuto kama nakala za Kizulu.

Bi. Dlamini alifanya kazi ya kukuza msamiati na wanafunzi kupanua masafa yao ya vitenzi na vielezi katika lugha ya ziada, kwa kuwa aliona kuwa eneo hili lilikuwa na upungufu. Kisha, akawataka wanafunzi warekebishe uandishi wao, kwa kutumia vitenzi na vielezi vingi zaidi.

Baada ya kuandika majina kwenye kazi zao, wanafunzi waliweka mashairi na hadithi zao kwenye meza nyuma ya darasa. Walifurahia kusomeana kazi zao.

Bi. Dlamini aliona jinsi vitenzi na vielezi vingi zaidi vilivyokuwa sehemu ya msamiati wa kawaida wa wanafunzi kutokana na zoezi hili.

Shughuli ya 1: Picha za maneno katika lugha mbili

Andika ubaoni shairi la matusi ‘Wewe’. Andika ubaoni shairi la ‘matusi’ ‘Wewe’, lililo katika Nyenzo-rejea 1: Shairi .

Lisome na wanafunzi na mjadiliane kila ulinganishi, k.m. ‘kichwa ni kama ngoma tupu’ humfanya mtu afikiri kuwa ni kikubwa na kitupu, n.k.

Watake waandike shairi la sifa, kama darasa, juu ya mtu anayefahamika sana wanayemheshimu.

Amua kwa kushirikiana nao sifa au vipengele ambavyo wataeleza. Kama mtu ni mwanariadha, wanaweza kuchagua sifa za kimwili, miguu, umbo, jinsi anavyotembea, n.k.

Sasa vigawie sifa hizi vikundi au mtu mmojammoja, na watake wafikirie vilinganishi katika lughaya nyumbani.

Watakapotaja vilinganishi vyao, amua, kama darasa, kuhusu kilinganishi bora kwa kila sifa, na viandike katika lughaya nyumbani.

Sasa jadili jinsi wanavyoweza kusema hayo katika lugha ya ziada. Tafsiri ya moja kwa moja (tafsiri sisisi) haifai, lakini jaribu kujenga taswira inayolingana na iliyo katika lugha ya nyumbani.

Kwa njia hii, lijenge shairi lako na darasa lako katika lugha ya ziada.

Watake watunge shairi lao wenyewe –‘matusi’ au ‘sifa’. Wanafunzi wahahakikishe wasisababishe chuki ya kweli. Je, mkabala huu umefaulu kuwasaidia wanafunzi kukuza msamiati katika lugha ya ziada?

Sehemu ya 4: Namna ya kujenga juu ya ujuzi wa lugha ya nyumbani