Somo la 2

Kuwaheshimu wengine na kutendeana kwa njia zinazofaa kati ya vizazi mbalimbali ni muhimu katika kufungamanisha jumuiya pamoja. Jinsi wanafunzi wako wanavyoongea na kushirikiana na kila mmoja darasani kwako kunaweza kuathiri malengo yao katika shule na katika kujifunza. Igizo kifani linaweza kutumiwa ili kuchunguza jinsi mtu anavyotenda kitabia katika hali mbalimbali. (Kwa mwongozo tazama Nyenzo-rejea Muhimu: Kutumia Igizo kifani/majibizano/tamthiliya darasani).

Utahitaji kutumia muda ili kuandaa maigizo-kifani-kifani yanayofaa. Kumbuka, lengo ni kuwasaidia wanafunzi wako ili wachunguze imani, maarifa na mienendo yao wenyewe, na njia ya kufanya hivyo bila woga ni kwa njia ya igizo.

Uchunguzi Kifani 2 unaonesha jinsi mwalimu mmoja alivyotumia igizo na wanafunzi waliokuwa wadogo zaidi ili kuchunguza kanuni za kimaadili ndani ya familia zao. Shughuli 2 inatumia igizo kifani ili kuchunguza mahusiano ya kijamii.

Uchunguzi kifani ya 2: Kanuni za familia

Bibi Mnagara anafundisha darasa la Tatu katika shule ya Msingi Themi. Aliwaambia wanafunzi wake wazungumze na babu na bibi zao au wanafamilia wengine wakubwa na kuwauliza kuhusu kanuni za kimaadili zinazotumika katika familia zao.

Siku iliyofuata, darasani, walilinganisha kwa pamoja kanuni hizi kutoka familia zao mbalimbali na kukuta kuwa kanuni nyingi zilikuwa zinafanana. Mtoto mmoja au wawili walikuwa na kanuni ambazo wengine hawakuwa nazo, na walizungumzia juu ya sababu za baadhi ya familia kuhitaji kanuni tofauti. Walikuta kuwa nyingi ya kanuni hizi zilikuwa ni kwa ajili ya watoto! ( Nyenzo-rejea 3: Kanuni za familia moja ina baadhi ya kanuni ambazo unaweza kuzijadili na darasa lako).

Bibi Mnagara alichagua vikundi vidogo vya wanafunzi kuigiza kwa vitendo moja ya kanuni hizi. Hii ililisaidia darasa kujadili tabia zilizooneshwa na vikundi hivi pamoja na wakati kanuni hizi zinapotumika.

Waligundua kuwa wakati mwingine kulikuwa na kanuni tofauti kwa ajili ya wavulana na wasichana. Walilizungumzia hili na kukuta kuwa kulikuwa na kazi maalum zilizofanywa na wavulana tofauti na zile za wasichana. Walihisi kwamba, kwa kiasi kikubwa, wasichana, hawakutendewa sawa na wavulana. Mwishowe, darasa zima lilikubali kuwa haikuwa haki na kwamba kanuni hizi lazima ziwe sawa kwa wote.

Mwishoni, Bibi Mnagara alieleza ni kwa nini kanuni hizi ni muhimu. Pia aliweka kumbukumbu katika kitabu chake kwa ajili ya kuandaa somo kuhusu masuala ya kijinsia ili kuendelea kuchunguza na yumkini kupinga tofauti katika makuzi ya wasichana na wavulana.

Shughuli ya 2: Kutumia maigizo-kifani kifani ili kuchunguza mahusiano ya kijumuiya

Andaa maigizo-kifani yanayohusu mazingira mbalimbali ya kijumuiya:

Godfrey anakutana na chifu

Bw. Eliasi muuza dukani

Yahsin na babu yake

(Kwa ufafanuzi zaidi kuhusiana na mawazo haya, angalia Nyenzo-rejea 4: Igizo kifani kuhusu mahusiano ya kijumuiya . Unaweza kuongezea shughuli zako mwenyewe.)

Waambie wanafunzi wako kufanya kila igizo kifani na kisha kuwa na mjadala wa vikundi au darasa kila baada ya kila igizo moja. Bainisha tabia nzuri na mbaya. Liulize darasa jinsi watu katika hadithi wanavyopaswa kuwa kitabia.Waambie wanafunzi, katika makundi, wafikirie hadithi yao wenyewe ya kuigiza. Waelekeze ili kuhakikisha kuwa wanafikiria hali halisi. Kiruhusu kila kikundi kiwasilisha igizo kifani lake, na rudia majadiliano ya kidarasa au ya kikundi ili kutafuta njia za kusuluhisha hali hizi.