Somo la 3

Kadiri wanafunzi wako wanavyokua, ni muhimu sana kuwasaidia ili wajifunze kuheshimu maoni na imani mbalimbali za watu. Hadithi ni njia nzuri za kuanzisha mjadala wa mawazo yanayohusiana na maingiliano ya kitamaduni pamoja na tabia nzuri au mbaya. Hadithi zinaweza kuwasaidia wanafunzi waelewe kanuni zinazotawala tabia za aina mbalimbali.

Ili kutumia hadithi vizuri, lazima uingize wahusika ambao wanatofautiana kitabia. Mjadala mrefu unaweza kutokana na hadithi iliyochaguliwa vizuri, lakini pia unahitaji kutafakari juu ya maswali ambayo unaweza kuwauliza wanafunzi.

Jambo hili pia linahusu maigizo-kifani kifani. Kwa kubuni wahusika na kuigiza kama wao, wanafunzi wanaweza kuchunguza aina za migongano ya kitamaduni inayoweza kutokea katika maisha halisi, lakini bila kuathiriwa na matokeo ya migongano hii. Hadithi na maigizo-kifani kifani yanaweza kuwasaidia wanafunzi wako kukuza welewa wao wa utofauti kwa njia ambayo haitishi. Nyenzo-rejea 5: Jumuiya zenye mwingiliano wa kitamaduni itakusaidia kuendeleza mawazo haya pamoja na wanafunzi wako.

Uchunguzi kifani ya 3: Kutumia usimulizi wa hadithi katika kuchunguza migogoro ya kijumuiya

Bwana Agoro aliamua kufundisha darasa lake kuhusu umuhimu wa watu kuheshimu wanajumuiya na nafasi mbalimbali walizonazo, pamoja na madhara yanayotokana na mgogoro. Alitumia hadithi ya mapigano baina ya makundi matatu ya kitamaduni yaliyoko Mpanga ili kujadili masuala haya. Tazama nakala ya hadithi hii katika Nyenzo-rejea 6: Mgogoro katika jumuiya ).

Kabla ya kusimulia hadithi hii, Bwana Agoro aliwaambia wanafunzi wake wasikilize vizuri na wajaribu kubainisha sababu yenyewe ya mgogoro huu. Baada ya kusikiliza hadithi hiyo, walishirikishana maoni yao na kuyaorodhesha ubaoni.

Kisha, aliwaambia, kwa vi kundi, kuelezana jinsi matukio yalivyojengwa hatua kwa hatua. Baada ya dakika kumi, walizungumza kama darasa na kukusanya hatua hizo mbalimbali na kuziandika ubaoni.

Baadaye Bwana Agoro aliwaambia wajadili jinsi ambavyo wangemaliza tatizo kwa kuangalia kila moja ya hatua hizi mbalimbali na kueleza jinsi ambavyo wangezuia kila moja. 

Mwisho, aliwaambia waorodheshe njia ambazo makundi haya matatu tofauti yanavyo shiriki na pia kushirikiana na jumuiya kwa njia chanya. Hii iliwasaidia kwelewa jinsi kila kundi lilivyokuwa muhimu kwa kundi jingine na jinsi ambavyo lisingeliweza kufanya kazi bila msaada wa makundi mengine.

Wanafunzi walijikuta wakilifurahia somo, na Bwana Agoro aliona jinsi walivyoanza kushughulikia masuala haya kwa umakini.

Katika somo lililofuata, wanafunzi walifanya tena kazi kwa vikundi katika kufikiria eneo lolote lile kwenye jumuiya yao lililokuwa na mgogoro na baadhi ya masuluhisho. Walitumia stadi za jinsi ya kupata ufumbuzi wa tatizo walizokuwa wamezitumia wakati walipokuwa wanashughulikia hadithi.

Shughuli muhimu: Kuigiza juu ya mwingiliano wa kijumuiya

Lipange darasa lako katika vikundi vitatu: kila kikundi kitawakilisha mojawapo ya jumuiya kutoka kwenye hadithi katika Nyenzo-rejea 6 . Waambie kwamba wataigiza kuhusu mgogoro na kisha watafute amani, hivyo wanatakiwa wafikirie jinsi watakavyofanya. Watatakiwa wafikirie kuhusu wajibu wa jumuiya yao, na jinsi ya kuwasilisha wajibu huu katika maigizo-kifani kifani wao.

Baada ya dakika 15 za maandalizi, kiambie kikundi cha wanafunzi sita (watu wawili kutoka kila jumuiya) kuigiza mgogoro, kama walivyouona, mbele ya darasa. Kisha, waambie wakae chini na watafute amani wakati darasa likiwa linawaangalia. Waambie wasikilize kwa makini rai za kila mmoja wao, na washughulikie rai hizi kwa makubaliano yo yote yale.

Kwa kushirikiana na darasa zima, bainisha na jadili:

  • majukumu mbalimbali ambayo kila jumuiya inayo;

  • masuluhisho mbalimbali yaliyofikiwa.

Waambie wabainishe mawazo ambayo wangeweza kuyatumia katika maisha ya kila siku. Ni mawazo gani ambayo unafikiri yalikuwa bora zaidi?

Mwishoni, waambie waandike hadithi kwa kutumia maneno yao wenyewe na waongezee jinsi mgogoro ulivyosuluhishwa.

Nyenzo-rejea 1: Jumuiya ni nini?