Somo la 1

Kila jumuia ina imani na maadili mbalimbali, yanayoongozwa na desturi za jamii ya kijadi. Imani na maadili haya husaidia kuamua mienendo gani inakubalika katika jumuia husika.

Kwanza wanafunzi watajifunza taratibu hizi nyumbani, na mafunzo hayo yaweza kuwa na manufaa kwako. Unaweza kuchukua mfano kutoka katika matarajio ya familia katika kusaidia kubainisha namna ambavyo wanafunzi na walimu wanatarajiwa watende shuleni wanapokuwa:

  • darasani;

  • katika viwanja vya michezo;

  • wanawasiliana na mwalimu;

  • wanawasiliana wao kwa wao.

Kuunda kanuni zihusuzo tabia njema kwa wanafunzi wako kutasaidia umakinifu wao wanapokuwa darasani. Watakuwa na nafasi kubwa zaidi ya kuwa wasikivu wa jambo linalosemwa na kujali kuheshimiana.

Zaidi ya hapo, kwa kupata mawazo toka kwa wanafunzi wako, watajihisi kukubalika kwenye matarajio yoyote ya tabia njema. Watakuwa na nafasi kubwa zaidi ya kuheshimu matarajio haya kuliko kama ungewaambia tu kwamba ni lazima wafuate tabia fulani.

Kufanikisha hili kunahitaji mipango makini ambayo inaweza kuchukua muda mrefu kuitengeneza. Katika kila hatua, ni lazima usikilize mawazo ya wanafunzi wako kwa makini.

Uchunguzi kifani ya 1: Kanuni za darasa

Bibi Aber ni mwalimu wa Darasa la 4 nchini Uganda. Ana wanafunzi 63. Wakati wa wiki ya maelekezo ya mazingira, mwanzoni mwa muhula, aliwauliza wanafunzi wake kuhusu tabia wanazotarajiwa wazioneshe wakiwa nyumbani. Kwa kuwa ana darasa kubwa, aliwaweka wanafunzi katika kikundi cha watu wanane ili kulinganisha matarajio ya familia zao. Aliwataka wanafunzi kuorodhesha kanuni nne ambazo zinakubalika kwa wote.

Darasa lilitoa mifano mingi ya tabia ambazo familia zao zilizitarajia –nyingi kati ya hizo zilikuwa sawa kwa watoto mbalimbali. Bibi Aber aliandika baadhi ya tabia hizo ubaoni.

Halafu aliuliza kama ni lazima kuwepo na kanuni kama hizo za nyumbani kwa ajili ya tabia za darasani. Katika makundi, walichagua kanuni za nyumbani ambazo zingeweza kutumika darasani, na wakatoa sababu kwa nini wangetaka kuzitumia darasani. Baadaye walibadilishana mawazo kama darasa. Bibi Aber alifurahi, na akatumia mawazo haya kuunda sheria za tabia njema shuleni, ambazo zilijumuisha:jinsi tunavyotendeana; tabia zetu tuwapo darasani;tabia zetu wakati wa michezo;jinsi tunavyotunza vitu vyetu.

Walipigia kura kanuni sita ambazo walipenda kuzitumia.

Shughuli ya 1: Kuzifahamu Kanuni

Shughuli hii inweza kusaidia kueleza kwa nini tuna kanuni maalum, na jinsi zinavyomnufaisha kila mmoja.

  • Wapange wanafunzi wako katika makundi. Waambie wabainishe kanuni tano za nyumbani na tano za shuleni.

  • Chukua mfano mmoja wa kanuni ya nyumbani na mmoja wa kanuni ya shuleni kutoka katika kila kundi. Ziandike kanuni hizo ubaoni.

  • Waambie wanafunzi katika makundi wajadili:

  • kwa nini wanafikiri tuna kila kanuni;

  • Ni kwa namna gani kila kanuni inawasaidia.

  • Jadili mawazo yao kwa darasa zima. Andaa utaratibu wa kuuliza maswali ambayo yatawasaidia kutafakari zaidi kuhusu majibu yao.

  • Bainisha sheria mbalimbali toka kwenye kanuni, kwa kuliuliza darasa: k.m. usalama; kuwasaidia wengine; kusaidiana. Waambie waoanishe kila kanuni na sheria moja.

  • Mwambie kila mwanafunzi aandike aya moja kuhusu umuhimu wa kuwa na kanuni. Aya hizi zisomwe mbele ya darasa zima.

Maoni yao yalikuwa faafu kwa kiasi gani?

Sehemu ya 3: Njia za Uwajibikaji