Somo la 2

Unapokuwa na kundi kubwa la wanafunzi kwa pamoja, utakuwa na migogoro ya mara kwa mara itakayotokea baina yao. Hata hivyo, unaweza kupunguza uwezekano wa migogoro kwa kufanya jitihada ya kuwapatia wanafunzi wote mazingira yanayowasaidia. Mgogoro ukitokea ni vizuri sana kuutatua mapema iwezekanavyo. Huu ni wajibu wako kama mwalimu. Mgogoro ukiachwa bila kutatuliwa, unaweza:

  • kusababisha mazingira mabaya;

  • kuvuruga masomo ya kila mtu darasani;

  • kufanya darasa lisiwe mahali pazuri pa kukaa.

Mara nyingi, migogoro yo yote itakuwa baina ya wanafunzi wako, lakini lazima utambue pia kuwa mgogoro unaweza kuwa baina yako na mwanafunzi. Kwa sababu hii, unatakiwa uhakikisha kuwa kanuni nzuri za kimaadili pia zinakuhusu wewe. Jinsi unavyomwadhibu mwanafunzi lazima umwadhibu kwa kumheshimu mwanafunzi kwani kisichotakiwa ni tabia isiyopendeza ya huyo mwanafunzi na siyo mwanafunzi mwenyewe.

Ili kupunguza uwezekano wa mgogoro, lazima uweke kanuni wazi za mwenendo darasani, zinazohusu mahusiano ya kijamii na zinazohusu masomo. Kama wanafunzi watajua kutendeana vizuri, basi kutakuwa na uwezekano mdogo wa wao kupigana.

Pia ni lazima utambue tofauti kati ya wanafunzi wanaobishania hoja na wale wanaogombana au kupigana.

Njia rahisi kabisa ya kushughulikia mgogoro kwa haraka ni kuwatenganisha wale wanaohusika na kuwaweka sehemu tofauti za chumba. Lakini lazima upate sababu ya mgogoro wo wote ule. Waambie wanafunzi wakuelezee sababu za mgogoro. Tafuta suluhisho baina yao.

Uchunguzi kifani ya 2: Kutatua mgogoro

Bibi Kweli ana wanafunzi wa darasa la Tano. Siku moja, aliwapanga kwenye vikundi vya watanowatano kwa ajili ya zoezi la kusoma na kuandika.

Aligundua kuwa wanafunzi wawili katika kikundi kimojawapo walikuwa wakisukumana. Ghafla waliacha, lakini pia waliacha kufanya kazi pamoja. Hii ilimaanisha kuwa wanafunzi wengine katika kikundi chao pia wasingeweza kufanya kazi vizuri, kwani kazi ilikuwa ni ya kikundi. Pia, wanafunzi katika vikundi vilivyokuwa pembeni/jirani vimekizungu kikundi hiki vilisumbuliwa na hali hii.

Kwa haraka Bibi Kweli alimaliza zoezi na kuanza kukagua majibu ya kila mwanafunzi. Kisha alimwambia wanafunzi wote wasimame, watembee na waunde vikundi vipya. Kwa njia hii aliwatenganisha bila tatizo.

Mwisho wa darasa, aliwaambia wale wanafunzi wawili wamwambie kuhusu ugomvi wao. Aligundua kuwa tatizo lilikuwa juu ya nani angesoma kitabu. Aliwaambia warejelee kanuni za darasa za ushirikiano na kuwaeleza kwa nini kanuni hizi ni muhimu kwa kila mtu. 

Pia aliwaambia wale wanafunzi wawili kwamba, waliwasumbua wanafunzi wengine, na kwamba wanatakiwa wawe makini. Aliwaambia wawe marafiki tena, na wakumbuke kwa nini walihitaji kushirikiana.

Shughuli ya 2: Wasilisho la darasa juu ya mgogoro

Wasaidie wanafunzi wako watalii zaidi kuhusu migogoro inayotokea shuleni.

Waambie wanafunzi, kwenye vikundi, kuorodhesha aina mbalimbali za migogoro inayotokea shuleni na kutoa mfano kwa kila mgogoro.

Kusanya mfano mmoja mmoja kutoka kila kikundi na uuandike ubaoni.Kiagize kila kikundi kuzungumzia kuhusu aina mojawapo ya mgogoro, kikibainisha: sababu za mgogoro;ungewezaje kuepukwa;ungewezaje kutatuliwa

Waambie watoe wasilisho kuhusu mawazo yao hayo mbele ya darasa. Baada ya kila wasilisho, viambie vikundi vingine viongezee mapendekezo yao ya njia za kutatua mgogoro.

Mwishoni, kiambie kila kikundi kiandike kwenye kadi njia bora za kuepuka aina ya mgogoro waliouchagua. Kusanya kadi hizi na kisha andaa onesho