Somo la 1

Kuwapatia wanafunzi wako fursa za kutumia miundo ya lugha mahsusi tena na tena ili waweze kuimudu, kunahitaji kuwa tendo la kufurahia.

Kuna nadharia isemayo kwamba watu hujifunza lugha kwa kuiga na urudiaji. Hapo zamani, kozi nyingi za lugha zilitumia sehemu kubwa ya urudiaji (mazoezi ya kurudiarudia). Siku hizi inadhaniwa kwamba vitendo vinavyowahusisha wanafunzi katika mawasiliano ‘halisi’ vinawasaidia zaidi kuliko urudiaji usiokuwa na maana. Hata hivyo, urudiaji bado unaweza kuwa wenye manufaa endapo wanafunzi watachomeka maana halisi katika sentensi. Inasaidia kama watawekewa urudiaji katika muziki.

Jaribu mawazo yaliyomo katika Uchunguzi-kifani 1 na Shughuli 1 kupima nadharia hizi.

Uchunguzi kifani ya 1: Urudiaji katika lugha unaohusu hadithi kutoka gazetini

Bwana Gasana anafundisha Kiingereza Darasa la 4 huko Butare, Rwanda. Mauaji yalitokea katika jiji lao, saa 2 usiku, siku mbili zilizopita. Aliwaonesha wanafunzi wake ripoti ya mauaji hayo kutoka kwenye gazeti. Alizungumza na wanafunzi wake (kwa lugha ya nyumbani) kuhusu jinsi askari wa upelelezi wanavyouliza watu wanapojaribu kutafuta mhalifu. Halafu akaweka sampuli ya swali na jibu ubaoni, kwa Kiingereza:

Q: Ulikuwa unafanya nini Jumanne saa 2 usiku, Kigeri?

A: Nilikuwa ninatazama runinga.

Aliwauliza wanafunzi wachache swali hilo hilo, ili kuhakikisha watatoa majibu yao wenyewe kwa utaratibu sahihi. Kisha, aliwaweka wanafunzi katika makundi ya wanafunzi sita sita. Kila mwanafunzi alitakiwa kuuliza swali kwa wanakikundi wake wengine watano, ambao kila mmoja atatoa jibu lake. Bwana Gasana aliwahimiza wanafunzi kusahihishana, na alitembea kuzunguka darasa, kusikiliza na kuongoza makundi.

Alimwambia kila mwanafunzi aandike ‘ripoti ya askari wa upelelezi’ kuhusu kundi lake. Kila moja kati ya sentensi sita zilionekana katika muundo ufuatao:

Saa 2 usiku Muteteli alikuwa anacheza na kaka yake.

Saa 2 usiku Erisa alikuwa anaandaa chakula.

Nyenzo-rejea 1: Miundo mbadala ya somo inatoa sampuli zilizotumiwa na Bwana Gasana akiwa na wanafunzi wake wakubwa wa Darasa la 5.

Shughuli ya 1: Urudiaji katika bei mbalimbali

Tafuta au tengeneza tangazo la mauzo au orodha ya bei za mbogamboga za mahali hapo, ukionesha mapunguzo ya bei (angalia Nyenzo-rejea 2: Tangazo la bei kwa mifano). Kabla ya somo, tengeneza nakala kubwa ya tangazo au orodha ya bei ubaoni, au tayarisha tangazo moja au orodha ya bei kwa kila kundi katika darasa lako.

Andika mfuatano ufuatao wa swali na jibu ubaoni.

Q: .…. ni bei gani ?

A. Kabla ilikuwa shilingi …., lakini sasa ni shilingi …. tu.

Q: Hizo …. ni bei gani?

A: Kabla zilikuwa shilingi …., lakini sasa ni shilingi …. tu.

Wakati wa somo, onesha baadhi ya bidhaa, huku ukiuliza swali kulingana na bidhaa, na kuwaambia wanafunzi wachache wajibu.

Kisha, waweke wanafunzi katika makundi, ili waulizane na kujibizana kwa utaratibu huo huo.

Waambie kila kundi watunge na kuigiza wimbo wenye mistari yenye muundo huu: Kabla, hiyo …. ilikuwa shilingi …., lakini sasa ni shilingi …. tu. 

Wanafunzi wako wamejifunza nini kutokana na shughuli hizi? Unajuaje? Je, utatumia aina hii ya zoezi tena?Kwa nini utalitumia tena, au kwa nini hutalitumia tena?

Sehemu ya 2: Njia zijengazo ufasaha na usahihi