Somo la 3

Yumkini utakuwa umegundua kwamba ni vigumu, wakati mwingine, kusahihisha kazi zilizoandikwa na wanafunzi, kwa sababu kuna makosa mengi sana ya lugha ndani yake. Hutakiwi kuwavunja moyo wanafunzi wako kwa kufanya masahihisho mengi kupita kiasi. Lakini pia hutakiwi kuwaacha waendelee na tabia mbaya. Tutatatuaje tatizo hili?

Njia mojawapo ni kuunganisha maana na miundo ya lugha. Andaa zoezi la kuandika ambalo lina maana kwa wanafunzi. Wahimize wahariri kazi zao kabla hawajazikusanya. Unaweza kuwaambia, wawili wawili, waandike ili waweze kusaidiana. Kisha wanaweza kurudishiwa kazi zao bila kuwa na maoni mengi ya kiusahihishaji.

Unaposahihisha kazi zao, zingatia kwenye maana na jambo linalopendelewa. Uzingativu wa pili, kazia kwenye kipengele kimoja cha muundo wa lugha –tahajia au pengine njeo za kitenzi au viunganishi. Kwa njia hii, maoni ya kiusahihishaji huwa si mengi na huelekeza sehemu maalum, na wanafunzi wana uwezekano mkubwa wa kuyaona na kuyazingatia.

Uchunguzi kifani ya 3: Kubadilishana uzoefu katika ‘Gurudumu la Waandishi’

Kozi ya kundi la walimu waliomo kwenye mafunzo kazini mjini Tabora walikuwa wakijaribu kuboresha uandikaji wao wenyewe. Wakufunzi waliwahimiza kuunda ‘Gurudumu la Waandishi’, ambako watasomeana kazi zao na kupeana maoni. Waliandika kuhusu uzoefu wao –kumbukumbu za utotoni, watu na mahali pa ajabu wanapopakumbuka, mambo ambayo hawatayasahau.

Wakufunzi waliwaongoza katika utoaji wa maoni, kwa kutumia vigezo mbalimbali kutegemeana na kitu kilichokuwa kimeandikwa. Hii hapa ni mifano:

Je, mwandishi anakisema akitakacho kwa ufasaha? Je, kuna sehemu ambazo zinahitaji kufafanuliwa?

Sehemu zipi zinavutia? Kitu gani kinazifanya zivutie? Sehemu gani zinachusha? Zinawezaje kuboreshwa?

Je, kila aya ina wazo kuu? Je, kuna baadhi ya mawazo makuu yanayohitaji kuendelezwa zaidi? Je, aya zinahitaji kupangwa tena?

Je, sentensi ni kamilifu? Je, ni ndefu sana au fupi sana? Je, zimewekewa alama za uandishi kwa usahihi? Je, tahajia za maneno ni sahihi?

Kazi hiyo imeandikwa kwa kutumia njeo ipi? Kagua ili kuhakikisha kwamba kila kitenzi kiko katika njeo stahili au kama kuna sababu ya msingi ya kutumia njeo nyingine.

Kitabu kiliwekwa pamoja kwa kujumuisha maandiko ya walimu hawa ambacho kilshirikishwa kwa familia na rafiki. Walimu waliamua kwamba baadhi ya mawazo haya yanaweza kutumika darasani, vikabadilishwa kulingana na umri na uwezo wa wanafunzi wao.

Shughuli muhimu: Uhariri wa kujifanyia mwenyewe na wa kubadilishana na wanadarasa kwa lengo la kuboresha uandishi

Waambie wanafunzi wako waandike kuhusu jambo linalotokana na uzoefu wao wenyewe. Jadili mawazo yatakayojitokeza ili kusisimua ubunifu wao. Kwa mfano, wanaweza kueleza kitu ambacho ni mali yao au mtu wa kuvutia wanayemfahamu. (Kwa kuwa uandishi huu ni wa kutoa maelezo, ni yumkini wakatumia njeo iliyopo.) Wanaweza kusimulia hadithi ya kutisha au tukio la kusisimua, au jambo la kijumuiya. (Kwa vile uandishi huu unajumuisha hadithi au masimulizi, ni yumkini wakatumia njeo iliyopita.) Wanafunzi wengine wanaweza kuona inasaidia zaidi kufanya kazi hii wawili wawili.

Kisha, waambie wafanye kazi katika makundi madogo madogo, kwa kusomeana maandishi yao. Watake watumie mojawapo au zote mbili kati ya seti za maswali zifuatazo ili kutoa maoni kwa kila kundi:

  • A.Sehemu zipi zinavutia? Kitu gani kinazifanya zivutie? Sehemu zipi zinachusha? Hizi zinawezaje kuboreshwa?
  • B.Uandishi huu umetumia njeo gani? Kagua ili kuhakikisha kwamba kila kitenzi kiko katika njeo stahili AU hakikisha kuwa kuna sababu ya msingi ya kutumia njeo nyingine.

Baada ya kupata maoni kutoka kwenye makundi, kila kundi liandike tena kazi yao. Kusanya kazi hizo, na tumia vigezo sawa kusahihisha kazi zote.

Utaratibu huu ulifanikiwa kwa kiasi gani? Je, utaurudia tena?

Je, hali ya uandishi wa wanafunzi wako ilipata ubora? Unajuaje?

Nyenzo-rejea ya 1: Miundo mbadala ya somo – iliyotumiwa na Bwana Gasana