Muhtasari wa Kipindi cha 8

Katika Kipindi cha 8 cha somo, ulijifunza mambo haya:

  1. Mwanzoni mwa ujauzito, kwa kawaida watoto huwa katika mlalo wa kutanguliza matako. Katika asilimia 95 ya visa hivi, watoto hujigeuza na kutanguliza veteksi kabla ya leba kuanza.
  2. Mlalo mbaya au fetasi kutokuwa katika nafasi yake ya kawaida baada ya muda kamili wa ujauzito kukamilika huongeza hatari ya kuzuiliwa kwa leba na matatizo mengine ya uzazi.
  3. Visababishi vikuu vya milalo mibaya na fetasi kutokuwa katika nafasi yake ya kawaida ni: kiasi kingi cha kiowevu cha amnioni, umbo na ukubwa usio wa kawaida wa pelvisi, tyuma kwenye uterasi, plasenta privia, ulegevu (udhaifu) wa misuli ya uterasi (baada ya ujauzito mwingi hapo awali); au mimba ya zaidi ya mtoto mmoja.
  4. Matatizo yanayotokea sana ni: upasukaji wa mapema wa membreni, leba kuanza kabla ya muda kamili wa ujauzito kukamilika, leba inayoendelea kwa muda mrefu au iliyozuiliwa, uterasi kupasuka, kutokwa na damu baada ya kuzaa, kuathirika kwa fetasi na mama, kunakoweza kusababisha kifo.
  5. Veteksi kutokuwa katika nafasi yake ya kawaida ni ambapo kisogo cha fetasi kimeangalia upande wa nyuma wa mama. Sehemu ya nyuma ya fuvu la kichwa cha fetasi inaangalia upande wa nyuma wa mama badala ya mbele ya pelvisi ya mama. Asilimia 90 ya fetasi zisizokuwa na veteksi katika nafasi yake ya kawaida huzunguka na mama kuzaa kikawaida.
  6. Mlalo wa kutanguliza matako (wenye matako na miguu ya mtoto karibu na seviksi, matako juu ya seviksi, mguu au miguu juu ya seviksi) ni ambapo matako ya mtoto ndiyo kitangulizi katika leba. Mlalo wa kutanguliza matako hutokea katika asilimia 3-4 za leba baada ya majuma 34 ya ujauzito. Mlalo wa kutanguliza matako unaweza kusababisha kuzuiliwa kwa leba, prolapsi (kuchomoza) ya kiungamwana, haipoksia, plasenta kujitenga kabla ya muda wake, na mtoto au njia ya uzazi kupata majeraha.
  7. Mlalo wa kutanguliza uso hali ya kichwa cha fetasi kujikunja sana kuelekea nyuma kiasi kwamba uso ndio kitangulizi katika leba. Mlalo wa kutanguliza uso hutokea kwa takriban mimba 1 kwa kila 500 iliyokomaa. Mlalo wa kutanguliza uso ambapo kidevu kimeangalia upande wa nyuma wa mama (“kidevu nyuma”) huzunguka na kuwa katika hali ya kidevu kuangalia upande wa mbele (pelvisi) wa mama (“kidevu mbele”) na kuzaliwa kikawaida. Huenda mama huyo ahitaji kuzaa kwa njia ya upasuaji iwapo mtoto hatazunguka kwa njia hii.
  8. Mlalo wa kutanguliza paji la uso ni ambapo paji la uso wa mtoto ndicho kitangulizi. Mlalo huu hutokea kwa takribani ujauzito 1 kwa kila 1000 uliokamilisha muda na ni vigumu kuugundua kabla ya leba. Upasuaji unaweza kustahili.
  9. Mlalo wa kutanguliza bega hutokea wakati fetasi imejilaza kingamo katika leba. Ukichunguza uke, baada ya leba kuendelea vizuri, utahisi mbavu za mtoto na pia mkono unaweza kuchomoza. Kuzaa kwa njia ya upasuaji huhitajika isipokuwa daktari au mkunga aweze kumgeuza mtoto ili kichwa kitangulie (“kichwa chini”).
  10. Mimba ya zaidi ya mtoto mmoja huwa katika hatari kubwa ya mlalo mbaya wa fetasi. Kina mama wanahitaji utunzaji zaidi katika ujauzito huu. Pacha wamo katika hatari ya matatizo yanayohusiana na kuzaliwa wakiwa na uzani wa chini na kabla ya muda kamili wa mimba kukamilika.
  11. Mlalo wowote isipokuwa ule wa kutanguliza veteksi, baada ya wiki 34 ya mimba, husemekana kuwa na hatari kubwa kwa mama pamoja na mtoto wake. Usijaribu kumgeuza mtoto aliye katika mlalo mbaya au asiye katika nafasi yake ya kawaida! Mpe mama rufaa ili aweze kupata huduma ya dharura ya uzazi.

8.8 Utunzaji wa wanawake walio na milalo mibaya ya watoto au mimba ya zaidi ya mtoto mmoja

Maswali ya Kujitathmini ya Kipindi cha 8